Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia, lakini pia namshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya njema aliyotujalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijasema jambo, nianze kwa kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, kwa maamuzi mazito na makubwa aliyoyafanya kwa kwa sisi wakazi wa Dodoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeomba ardhi ya Manispaa ya Dodoma iwe mikononi mwa wananchi na tumeomba Wabunge wamepita, Wabunge wamekuja wamepita, lakini mwisho wa siku Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Awamu ya Tano imetupa ardhi yetu ya Manispaa ya Dodoma. Sina lugha ya kusema, sina namna ya kushukuru kwa niaba ya wananchi wa Dodoma hasa Manispaa ya Dodoma. Tunaishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu ambacho naiomba Serikali hii, iweke mipango mizuri kuhakikisha kwamba wananchi ambao walishalipia ardhi na hawajaoneshwa viwanja vyao, wakaoneshwe viwanja vyao sasa. Uwekwe utaratibu ambao wale ambao walikuwa wanalipia kidogo kidogo wamalizie kulipia na kupata viwanja vyao. Mpango uwekwe wakati mikakati inaendelea, basi liwepo dirisha kwa ajili ya kuhudumia watu ambao walikuwa wanalipia viwanja, hawajaoneshwa viwanja vyao na wale ambao wanalipia kidogo kidogo huduma ziendelee kama ilivyokuwa CDA.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie bajeti hii ya Wizara ya Kilimo sasa, kwamba kilimo ndiyo uti wa mgongo wa Taifa hili, karibu asilimia 75 ya Watanzania wanategemea kilimo; na kilimo wanachotegemea ni kilimo cha kusubiri mvua, bila kujali tabianchi, bila kujali kwamba zipo mvua za kutosha. Asilimia 4.9 tu ya bajeti ya Serikali ndiyo imetengwa kwa ajili ya kilimo. Kwa hiyo, tunaona jinsi ambavyo kilimo hakijapewa msukumo mkubwa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitegemea kwamba Benki ya Kilimo ingepata fedha za kutosha kwa ajili ya Watanzania ili waweze kukopa; wakulima wa kati, wakulima wadogo na hata wakulima wakubwa. Mabenki ya biashara yanashindwa kuwakopesha wakulima wa kati na wadogo kwa sababu ya riba kubwa na kwa sababu hawana dhamana, wanategemea mvua inayotoka kwa Mungu. Hakuna mabwawa makubwa kwa ajili ya kilimo, hakuna makinga maji kwa ajili ya kilimo. Kwa hiyo, wakulima tulio wengi tunategemea kilimo cha mvua. Kwa hiyo, naomba kwamba Serikali ione namna ya kuchimba mabwawa ya kutosha ili wananchi walime kwa kutegemea kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo tatizo la mbegu. Mbegu asilimia 65 inaagizwa nje ya nchi. Hatuwezi kutegemea mbegu kutoka nje ya nchi kwa asilimia 65, ASA wanafanya kazi gani? Kama ni fedha, wapewe wazalishe mbegu. Sasa hivi wakulima wanategemea mbegu kutoka sokoni. Mbegu ya sokoni iliyozalishwa miaka 20 iliyopita, haiwezi kumsaidia mkulima kujiinua kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna Kambi za JKT, tuna Magereza; tungeweza kutumia Magereza na Kambi za JKT kuzalisha mazao ya kutosha kulisha nchi hii. Wana maeneo makubwa. Kama hawana maeneo makubwa, Serikali iwape maeneo JKT walime. Tunao vijana wengi, tunaweza kuanzisha mashamba darasa kwa ajili ya vijana na vijana wakalima na wakajitegemea na wakazalisha kiasi kikubwa sana kwa ajili ya nchi hii na tukauza na tukapata fedha nyingi sana za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kupanga ni kuchagua. Tunaweza tukapanga kwamba kwa kuwa mikoa ya Kanda ya kati hatuna mvua za kutosha, basi tupate Maafisa Ugani watakaotusaidia kuwashauri wakulima juu ya kilimo cha alizeti, karanga, ufuta, mtama kutokana na hali ya tabianchi. Ukimwacha mkulima alime anavyojua, hawezi kujua mvua itanyesha lini.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi hapa Dodoma mvua inanyesha mwezi wa 12, mwezi wa Kwanza, wa Pili mvua inakatika. Mwaka huu mvua imenyesha mwezi wa Pili mwishoni na mwezi wa Tatu. Wakulima waliopanda mwezi wa 11 hawakuambulia kitu. Hivyo, kuna haja ya kuwa na Maafisa Ugani wa kutosha ili wawashauri wakulima namna ya kukabiliana na tabianchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala ununuzi wa pamoja. Nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa jambo hili la ununuzi wa pamoja, lakini hapo....

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.