Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana nami kwa kunipa nafasi nichangie Wizara hii muhimu ya Kilimo, Wizara ambayo ni uti wa mgongo wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba uniruhusu nitoe pole nyingi sana kwa wananchi wangu wa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki hususan wananchi wa Kata ya Kinole, Tegetelo na Mkuyuni kwa athari kubwa ya mvua iliyowapata ambayo imesababisha uharibifu mkubwa wa barabara hasa ile ya Madam – Kinole na Bigwa – Kisaki. Niwaambie kwamba suala hili tumeshalifikisha kwa Serikali na naishukuru sana Serikali kwa kuanza kutengeneza, kurudisha miundombinu, ile ya barabara ya Bigwa - Kisaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu kwa Serikali ni kwamba kutokana na hali halisi ya Kinole, leo ni siku ya 15 watu hawana mawasiliano ya barabara. Zaidi ya kilometa 30 watu wanatembea kwa miguu. Naomba na hii barabara itolewe jicho ili iweze kurudisha mawasiliano haraka iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo, kwanza naishukuru sana Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa hotuba yao nzuri ingawa tutatoa mchango kwa ajili ya kuboresha tu, lakini kila kitu kimekamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, niende moja kwa moja kwenye matatizo. Nianze na Jimbo langu kuhusu matatizo ya migogoro ya wakulima na wafugaji. Naipongeza sana Serikali kwa hatua ambazo imezichukua za kuunda Kamati za Wizara tano ili kutafuta suluhu la tatizo hili. Kama ulivyoshuhudia mwenyewe Mheshimiwa Waziri, kwenye kitabu chako kuhusu migogoro mingi, leo mauaji mengi ya mifugo kwa ajili ya ukame ni Morogoro; mapigano mengi ya wakulima na wafugaji ni Morogoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawe unafahamu Morogoro kiasili ulikuwa kwamba siyo Mkoa wa wafugaji, leo neema hii iko Morogoro, maana yake kuna wafugaji ambao wamekuja, hawakuzingatia taratibu na Kanuni za Kisheria kufika pale Morogoro. Ndiyo maana migogoro imekuwa mingi na ndiyo maana mifugo iliyokufa imekuwa mingi kutokana na ukame na uvamizi wa ardhi bila kufuata taratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ombi langu kwa Serikali, wakati tunasubiri hii taarifa kufanyiwa kazi, lakini tuliona Serikali hii ya Awamu ya Tano imewatoa kwa nguvu kubwa sana wafugaji waliovamia mbuga za wanyama katika Hifadhi za Serikali. Kwa sababu hizo hizo, basi tunawaomba wawatoe kwa nguvu wale wafugaji wavamizi wasio halali, walioingia katika maeneo ambayo sio yao. Isiwe na kisingizio cha kusema hakuna pa kuwapeleka. Kama wale waliotolewa kwenye misitu walipatikana pa kuwapeleka na hawa wavamizi watafutiwe sehemu ya kwenda ili kumaliza tatizo hili la wakulima na wafugaji katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili kuhusu madeni ya Mawakala wa Mbolea, huu ni mwaka zaidi ya wa pili na nusu sasa tunazungumza kwamba Serikali inafanya uhakiki. Nami naiunga mkono sana Serikali yangu kwa sababu sishabikii na siko tayari Serikali iwalipe watu ambao ni
wababaishaji na wadhulumaji ambao hawakutoa huduma Serikalini, walipwe kwa jasho ambalo hawajalitumikia. Niko pamoja na Serikali yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ucheleweshaji huu umeleta athari kubwa sana kwa watoa huduma hizi. Watu wameuziwa nyumba zao, ndoa zao zimesambaratika, yaani maana yake watu wameachana na wake na waume zao kutokana na migogoro kwamba hakuna kipato ndani ya nyumba, lakini pia watu wamefilisiwa. Wengine wamejiua na kupoteza maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ombi langu kwa Serikali leo hii, kwa mfano, mtu aliyekopa shilingi milioni 100 benki, miaka miwili anadaiwa na benki zaidi ya shilingi milioni 40 kama riba aliyochukua asilimia 20. Itakuwa ni kuwaonea. Kwa wale watakaokuja kugundulika ambao ni halali na wametoa huduma kuja kuwalipa kiasi kile kile kama wanachoidai Serikali, kwa sababu siyo kosa lake kwa kuchelewa, ni kosa la mtu mwingine. Ni vizuri mkalichukulia hili kuwalipa pamoja na fidia na gharama za riba walizochukua mikopo kule benki ili kuwarudisha watu hawa katika sehemu tuliyowakuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, bila kufanya hivyo, maana yake tumewapeleka kwenye umaskini mkubwa sana. Leo hii kuna watu wangu kule walikuwa wanatoa ajira ya kujiajiri kwa wenzao, lakini leo wamekuwa ombaomba, wameshafika zaidi ya mara nne hapa kufuatia madai haya Wizara ya Fedha, kwa Waziri Mkuu na Waziri wewe mwenyewe, mpaka leo hawajapata. Wanashindwa kujilipatia mpaka nauli. Leo huyo mtu aliyejiajiri mwenyewe anatakiwa asaidiwe! Jua kwamba tatizo hili ni kubwa na limesababisha ombaomba wengi miongoni mwa watu wengi waliokuwa na uwezo mkubwa wa kujihudumia.

Mheshimiwa Naibu Spika, la nne, kwenye wabanguaji wa korosho, yaani kama Taifa mpaka sasa hivi ninachanganyikiwa; tunataka Tanzania ya viwanda au tunataka Taifa la kuzalisha malighafi kwa ajili ya viwanda vya wenzetu? Kwa nini ninasema hivi?

Mheshimiwa Naibu Spika, leo ni zaidi ya mwaka wa 20 tangu tuanze kuingia kwenye private sector, lakini zaidi ya asilimia 90 ya korosho inayozalishwa nchini inapelekwa nje ya nchi huko India au Vietnam kubanguliwa. Wakati mwingine Mheshimiwa Waziri mwenyewe anasifia kabisa, tumeuza korosho tani 4,000 imeenda Vietnam. Tunaona kama sifa! Naona kwamba hatujaelewa mustakabali au nia kubwa ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais alisema anataka viwanda na alisema hakuna mtu yeyote atakayemzuia ndoto zake; yule atakayemzuia atakwama mwenyewe. Nimuulize Mheshimiwa Waziri, nani anayemkwamisha katika uwekezaji wa ndani wa Viwanda vya Korosho kubanguliwa? Maana korosho hizi kwenda katika raw form India ama Vietnam maana yake tunahamisha utajiri na ajira kwenda kwenye Mataifa mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii kuwashindanisha wawekezaji wa ndani au wabanguaji wa ndani wadogo na wakubwa kwenye mnada na wanao-export kwa raw form, hakuna mwekezaji yeyote wa ndani ataweza kushinda mnada wowote ule. Kwa sababu nchi hizo za India na Vietnam, export levy yoyote wanayoiweka wenyewe wanaenda kurudishiwa. Nani ambaye atashinda mnada kwa hapa?

Mheshimiwa Naibu Spika, ushahidi upo wazi na ndio maana 90% za kusafirisha raw form na viwanda vilivyokuwepo; natolea kwa mfano mdogo, kwamba tulisema Wahindi wanyonyaji; wamekuja Wachina, Sun Shine Group kampuni kubwa kuliko zote kule China imewekeza leo Lindi ina uwezo wa ku-process zaidi ya tani 5,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mnada wa mwaka 2016 tumezalisha korosho zaidi ya tani 264,000MTS, imenunua ni 180 tu, tena za mwisho wa mnada baada ya wanunuzi ma-giant kuondoka, unategemea huyo ni nani atakuja kuwekeza Tanzania kwenye korosho kwenye processing? Mtu wa nje anakuja baada ya kuona mafanikio kwa mtu wa ndani kwamba amefanikiwa vipi au mwenzie aliyetangulia kwenye biashara hiyo amefanikiwa nini; naye ndio atavutika kuja.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu katika hili kwa Serikali, la kwanza ni vizuri kuendesha minada miwili tofauti, tukaiga model kama ya Msumbiji. Korosho ukianza msimu, kipaumbele cha kwanza, mnada wa kwanza, wanaletwa Local Processors watupu washindane kwa ajili ya kuhakikisha wanapata raw materials kwa ajili ya ku-process ndani, kutoa ajira kwa wananchi wetu; lakini pia kuongeza thamani kwenye korosho zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii tunavyo-export raw, maana yake Wahindi ndio wanaingiza foreign currency nyingi zaidi kuliko Watanzania. Mfano mdogo tu, korosho hapa leo wameuza Sh.4,000/= lakini ikibanguliwa zaidi ya Sh.25,000/= kwa kilo. Sasa nani anapata korosho bei kubwa zaidi? Ninyi au Vietnam? Sisi au Wahindi?

Mheshimiwa Naibu Spika, ni vizuri tuhakikishe tunawavutia wawekezaji, tuweke mazingira, wawekezaji wa ndani wapate korosho kwanza kama raw material kabla ya mtu mwingine yeyote. Wakishajaza ndiyo turuhusu ku-export, watu wa nje waje watoe. Katika kufanya hivyo tusije kumlalia mkulima. Serikali iangalie namna gani kwa zile bei watatoa kwa Local Processors ili twende sambamba.

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.