Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia Wizara hii. Kabla ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu, kwa kuendelea kunipa afya njema, lakini kwa namna ya pekee kabisa, nashukuru kiti chako kwa kuendelea kutenda haki hasa katika upande wetu huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtaalam mmoja anaitwa Kunzi mwaka 1988/1989 aliandika kitabu chake cha Managerial and Planning ambacho aliweza kueleza kwamba “failure to plan is planning to fail,” yaani siku zote wewe ukishindwa kupanga jambo maana yake ni kwamba unapanga kufeli. Alizungumza Kunzi maneno haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma kitabu hiki cha hotuba hapa, kwa kiasi kikubwa naomba niishukuru Wizara hii kwamba imeweza kuondoa tozo nyingi sana katika zao ambalo kwa kiasi kikubwa linalimwa Mikoa ya Mtwara na Lindi; zao la korosho. Tozo nyingi sana zimeondolewa. Tunashukuru sana Wizara hii kwa sababu kupitia kuondoka ama kuondolewa kwa hizo tozo, hivi sasa bei ya korosho iko juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru pia Wizara hii kwa kuhamasisha wanunuzi wengine kwamba mwaka wa 2016/2017 wanunuzi wa korosho waliweza kuongezeka. Miaka yote tulikuwa na Wahindi tu, lakini mwaka 2016 tumeweza kuona Vietnam na watu kutoka Uturuki wamekuja kununua korosho Mikoa hii ya Mtwara na Lindi na Tanzania kiujumla; na bei sasa imekuwa kubwa kwa sababu kuna ushindani huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo yote, naomba nizungumzie changamoto kadhaa ambazo zipo katika zao hili la korosho hasa mwaka 2016 kwa maana kwamba msimu wa mwaka 2016/2017.

Mheshimiwa Naibu Spika, wapo wakulima wameweza kutueleza Wawakilishi wao, sisi Wabunge; kwa mfano, pale kwangu Mtwara Mjini tuna AMCOS mbili; kuna AMCOS ya Mikindani na kuna AMCOS ya Naliendele. Hivi Vyama vya Msingi vimechukua korosho za wakulima lakini kwa bahati mbaya wameweza kuchukua hizo korosho kupitia minada. Imefanyika, minada zaidi ya minne; mnada wa kwanza mpaka wa nne.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la ajabu sana, la kushangaza ambalo naomba Mheshimiwa Waziri akija atuletee majibu ya kina kwa wananchi hawa, kwamba hizi AMCOS zimeweza kulipa minada miwili ya mwisho, yaani mnada wa tatu na mnada wa nne na wakaacha mnada wa kwanza na wa pili, ambao bei zake zilikuwa ni kubwa kuliko hii minada miwili ya mwisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba akija Mheshimiwa Waziri atupe taarifa, kwa nini hawa wanunuzi wa korosho kupitia hivi vyama vya msingi? Wameruka bei zile kubwa ambazo zilikuwa ni Shi.4,000/= na ilitangazwa kupitia vyombo vya habari kwamba korosho sasa mwaka huu zimepanda, zinauzwa Sh.4,000/= kwa kilo, lakini hawakulipa bei hiyo ya Sh.4,000/= wakaja kulipa minada ya mwisho ambayo imekuja kununuliwa na Wahindi kwa bei ya Sh.3,700/= na Sh.3,600/=.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa anipe maelezo ya kina katika hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo naishukuru Wizara hii, imeelezwa hapa kwamba mwaka huu 2017/2018 kutatolewa pembejeo za sulphur bure kwa wakulima wa Korosho. Nimesoma kitabu chote hiki mpaka kwenye bajeti yenyewe ambayo ni shilingi bilioni 266, sijaona hata eneo moja hilo ambapo wameweza kueleza kwamba pesa hiyo ya kununua sulphur ambayo itaenda kugawiwa bure kwa wakulima wa korosho, imekuwa indicated kwenye hiki Kitabu cha bajeti. Sasa isije ikawa tunazungumza tu lakini kwenye bajeti humu hakuna.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili suala la kugawa pembejeo bure, ni suala kubwa sana kwa sababu wakulima wa korosho ni wengi; na kama likifanikiwa hili kwa kweli Wizara hii itakuwa imefanya jambo kubwa sana. Kwa hiyo, naomba maelezo ya kina, hizi pesa zimewekwa katika fungu gani? Kama hazijawekwa zinapatikana sehemu gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala hili la Taasisi ya TFC, Taasisi hii ya kushughulikia pembejeo na mbolea Tanzania. Ni Taasisi ambayo wakati tunapitia kwenye Kamati yetu ya PIC ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma, tuliweza kupitia documents zake. Ni Taasisi mfu, yaani wanapewa ruzuku kila mwaka, wanapewa pesa nyingi na Serikali, lakini wana madeni kweli kweli! Hawana hata kiwanda kimoja cha kuzalisha mbolea Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashangaa sana, kwa nini tunaendelea kuienzi na kuilea TFC? Kwa nini isifutwe? Naomba Mheshimiwa Waziri aje atueleze, kwa nini hili Shirika linaendeshwa kihasara? Halileti tija kwa Taifa letu, halisaidii wakulima lakini bado tunaendelea kulilea. Naomba maelezo ya kina kutoka kwa Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na Mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze pia suala hili la uvuvi. Tunashukuru hivi sasa pale Mtwara Mjini kuna jengo lile ambalo inasemekana kwamba litakuwa ni Chuo cha Uvuvi. Ni muda mrefu hivi sasa, lile jengo limejengwa, hakuna vifaa, hatuoni mkakati wowote wa kuhakikisha kwamba kile chuo kweli kinaanza, wanafunzi wanaanza kusoma pale. Mwaka 2016, tuliongea kwenye bajeti hapa, walieleza katika bajeti yao pia kwamba hiki Chuo kitaanza. Sasa naomba kujua hiki Chuo cha Uvuvi Mikindani pale kitaanza lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, maeneo yale ya Kusini mwa Tanzania lakini maeneo yale ya Magharibi kule, tuna bahari hii ambayo ni bahari ya Hindi ambayo ina samaki wengi sana. Nilieleza hapa mwaka 2016 kwamba Waingereza wanasema maeneo yale ya Kusini yanaitwa, tunasema it is just virgin sea; yaani ni bahari bikira ambayo ina samaki ambao hawajawahi kuvuliwa tangu tupate uhuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujua kwamba Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba inanunua vifaa vya uvuvi kwa wavuvi wa maeneo haya ya Kusini? Pia hata kule Ziwa Tanganyika kuna samaki wa kila aina; kule Kigoma ukienda kuna samaki wa kila aina, lakini hawana vifaa vya kisasa vya uvuvi. Naomba Wizara itueleze kwamba mkakati wao wa kusaidia wavuvi ukoje katika kuwasaidia kununua zana za kisasa za uvuvi?

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kusema kwamba wakati tupo katika RCC pale Mtwara tuliweza kupewa taarifa na TAKUKURU kwamba mwaka 2015/2016 wakulima wa Kkrosho wa maeneo ya Mtwara wanadai vyama vya msingi shilingi bilioni 30. Yaani vyama vya msingi vimechukua korosho kwa wakulima, wameenda kuuza, lakini hawajawapa pesa wananchi wale. Shilingi bilioni 30 hazijalipwa, kwa taarifa ya TAKUKURU.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Kiti chako kiamrishe hii Wizara ipeleke TAKUKURU waende kukagua kwenye Vyama hivi vya Msingi kwa sababu wanawaibiwa wakulima sana. Tulivyohoji, tulivyowauliza, wakatuambia siyo shilingi bilioni 30 ni shilingi bilioni 11, lakini taarifa zinasema
na chombo cha uhakika kabisa, TAKUKURU kwamba wakulima wameibiwa shilingi bilioni 30. Tunaomba CAG aende akakague Vyama hivi vya Msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho, kuna taarifa ambazo siyo rasmi sana, lakini zinazungumzwa na wafanyabiashara wa korosho. Naomba Mheshimiwa Waziri hapa akija atupe majibu kwamba mwaka 2016 kulikuwa na fraudulent iliyofanyika bandari ya Mtwara ili iweze kuzuiwa kusafirisha Korosho kupitia bandari ya Mtwara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na wajanja inasemekana ndani ya Wizara yake ambao walikuwa wanaweka vingingi; na inasemekana kwamba ilikuwa kusafirisha korosho kutoka Mtwara tani moja kuelekea Soko la Dunia, ilikuwa ni dola karibu 14,000; lakini kutoa mzigo kutoka bandari ya Dar es Salaam ilikuwa ni dola 400.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba tupate ufafanuzi, kama hilo ni kweli kwa nini iwe hivyo? Lengo ni nini? Kuzuia bandari ya Mtwara isiweze kusafirisha korosho au tatizo ni nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri atuletee majibu ya kina atakapokuja kuhitimisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa haya, naomba kushukuru sana kwa kunipa nafasi. Ahsante sana.