Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Abdallah Haji Ali

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kiwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. ABDALLAH HAJI ALI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu muumba wa mambo yote. Pili, nakushukuru wewe binafsi kwa ujasiri wako wa kuliongoza Bunge kwa umahiri mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia katika Wizara hii angalau kwa uchache kati ya mengi ya Wizara hii ya Biashara na Viwanda. Viwanda ni kichocheo cha maendeleo katika kila Taifa duniani, viwanda ni mkombozi wa wananchi kupitia ajira na kuimarisha biashara na ustawi wa hali za wananchi kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, uwepo na uimarishaji wa viwanda katika nchi na duniani kote unapitia hali au hatua mbalimbali, uamuzi wa nchi yetu kuja na mkakati wa kujenga viwanda ni wa busara sana ila kabla ya kufikia huko kwanza kuna hizi hali mbalimbali mpaka kufikia uchumi wa viwanda, lazima zitekelezwe ili manufaa tunayoyafikiria yaweze kupatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda vinahitaji wataalam na injinia mbalimbali ili waweze kuviendesha kwa uzalishaji, hivyo naishauri Serikali kujipanga na wataalam wazawa na wazalendo kwa kuwasomesha vijana wa kutosha ili viwanda tuviendeleze viwe na wafanyakazi wazawa na wataalam wazawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo ambalo naishauri Serikali ikubali kutenga fedha kiasi cha kutosha ili kutoa nguvu kubwa juu ya kupata elimu kwa wataalam watarajiwa, ambao watafanya kazi katika viwanda hivyo. Lakini jambo la kusikitisha ni bajeti ndogo itengewayo Wizara ya Elimu ili kusimamia mafunzo na elimu ya kuzalisha wataalam, hivyo tumekuwa hatufikii lengo kutokana na bajeti ndogo itolewayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa uchumi tunaouendea ni wazi kwamba tunahitaji mafundi mchundo wa kutosha ili kukidhi haja ya viwanda vyetu vinginevyo kama Serikali haikutilia mkazo jambo la elimu tutakuwa siku zote wa kuajiri wataalam toka nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, India ni nchi inayoendelea kama Tanzania lakini sitaki kusema kwamba tuko sawa na India lakini India imelipa uzito mkubwa suala la elimu kiasi kwamba India wanatenga zaidi ya asilimia 10 ya bajeti ya nchi yao kwa upande wa elimu, sisi Tanzania bado tuko
nyuma si zaidi ya asilimia 4.5, hivyo India imefanikiwa kuzalisha wasomi na wataalam wengi sana wametosha India na wanauza wataalam duniani kote. Mfano, katika kampuni kubwa kama Microsoft ya Bill Gates takwimu zinaonesha zaidi ya wafanyakazi mabingwa asilimia 10 ni kutoka India. Pia Madaktari Bingwa wengi walioko Marekani na duniani kote ni Wahindi.

Mheshimiwa Naibu Spika, siri ya mafanikio hayo ni mkakati wa makusudi wa kuwekeza katika elimu. Kwa hali hii ni lazima na sisi tusiwe nyuma kwa kuiweka elimu kuwa ni kitu cha chini, huwezi kuendelea katika nyanja yoyote duniani bila elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri tena Serikali itilie maanani juu ya elimu katika nyanja zote hasa katika suala zima la utafiti, jambo ambalo halionekani kupewa nafasi kubwa wakati inafahamika wazi kwamba bila utafiti huwezi kuleta ufanisi wowote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Serikali itakuwa tayari kuiwezesha elimu na sisi tutazalisha wataalam wengi kwa ajili ya viwanda vyetu na ziada tunaweza kuuza nje, vinginevyo kama hatukuwa makini kwa uwekezaji juu ya elimu baada ya kuzalisha wataalam tutakuwa tukizalisha watumishi tu.