Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote namshukuru Mungu kwa kunipa uhai na nguvu za kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa. Pia namshukuru Mungu kupata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii muhimu kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa moyo wake wa dhati wa kusimamia ahadi ya kufanya Tanzania kuwa ya viwanda ili kuinua uchumi wa viwanda. Nchi zilizoendelea kiuchumi ziliwekeza sana katika uchumi wa viwanda maana hapo ndipo penye mafanikio makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mwijage, Katibu Mkuu na Watendaji wengine kwa kusimamia kikamilifu sera ya Tanzania ya viwanda, kweli kasi inayoendelea inaonekana. Nawashauri wasikatishwe tamaa na kelele za wasioitakia mema nchi yetu.

MheshimiwaMwenyekiti, ili kuinua uchumi wa nchi yetu haraka na kuwanufaisha Watanzania wengi, nashauri Wizara kuwekeza sana katika viwanda ambavyo malighafi zake zinapatikana hapa nchini mfano malighafi zinazotokana na mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi. Pia nchi yetu imejaliwa kuwa na madini mengi sana tuombe Serikali kuwavutia wawekezaji kuwekeza viwanda ambavyo tutatumia madini yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mfano Kyerwa tumejaliwa madini ya tini ambayo yanapatikana maeneo mengi ya Wilaya. Madini haya yamekuwa yakinufaisha nchi majirani zetu kwa njia ya magendo. Niombe Wizara kuwavutia wawekezaji kuwekeza Kyerwa kwa sababu mahitaji ya mabati ni mengi na hii itainua uchumi wa nchi yetu na kuwapa ajira wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa na Tanzania kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, sera na mkakati wa Serikali yetu ni kuwawezesha wananchi kwa kuwawekea mazingira rafiki wakulima wetu ili wanapolima wawe na uhakika na soko la bidhaa zao. Wananchi wetu wanajitahidi sana kulima lakini hakuna soko la uhakika. Jimbo langu la Kyerwa liko mpakani, Serikali imekuwa ikikosa mapato kwa sababu ya biashara ya magendo ya kupeleka bidhaa nchi jirani kwa sababu wananchi hawana sehemu ya kuuza bidhaa zao. Ili kuepuka kuikosesha Serikali mapato na kuwaondolea wananchi usumbufu na wale wanaopoteza maisha Mto Kagera kwa biashara ya magendo, naiomba sana Serikali kufufua masoko ya Kimataifa yaliyojengwa Murongo na Nkwenda ambayo yametelekezwa bila kukamilika na mpaka sasa hatujui nini kinaendelea na nani msimamizi wa masoko haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, masoko haya yakikamilika wananchi wetu watakuwa na soko la uhakika kitu ambacho kitainua kipato chao na uchumi wa nchi yetu utaongezeka na tutaepusha biashara ya magendo na madhara wanayoyapata. Naomba Mheshimiwa Waziri anapohitimisha awaambie Wanakyerwa nini hatma ya haya masoko.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe na kuishauri Serikali yangu tunayowavutia wawekezaji kuwekeza ufugaji na viwanda vya nyama, mfano Mkoa wa Kagera tuna mifugo mingi niwaombe Wizara kuwakaribisha wawekezaji wawekeze Kyerwa kiwanda cha nyama na maziwa tunao ngā€˜ombe wengi, mbuzi na mifugo mingine ili kuwainua wananchi wetu kimapato na uchumi wa Taifa letu utaongezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili Watanzania waendelee kuwa sawa lazima tuwavutie wawekezaji maeneo yote ili isionekane maeneo fulani ndiyo tumewekeza nguvu halafu maeneo mengine yameachwa. Nasema hili kwa sababu inaonesha mfano Mkoa kama Kagera umesahaulika kiuwekezaji wakati kuna fursa nyingi na ndiyo wazalishaji wakubwa wa ndizi, uvuvi, madini, ufugaji na kadhalika. Mkoa wa Kagera tumejaliwa kila kitu na tunaweza kulima na kuvuna zaidi ya mara mbili kwa mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuwekeza kwenye viwanda vikubwa ambavyo vinaajiri sehemu ndogo ya Watanzania lakini pia tuweke kipaumbele katika kuweka mazingira wezeshi kwa viwanda vinavyoajiri watu wengi kama viwanda vitakavyotumia malighafi zinazopatikana ndani mfano kahawa, alizeti, pamba, korosho na kadhalika. Kwa kufanya hivyo tutainua kipato cha wananchi wetu na uchumi wa Taifa na tutapata baraka maana hapa wataguswa Watanzania wengi na watanufaika sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, narudia kumpongeza Mheshimiwa Waziri hakika kazi anaiweza sana tumuunge mkono Watanzania kwa umoja wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.