Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii nami nichangie kwenye hotuba hii ya Wizara ya Viwanda. Namshukuru sana Mungu kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuzungumza katika Bunge lako Tukufu. Nianze kwa kusema naiunga mkono hoja iliyoko mbele yetu, nikiwa na reservation kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpongeze ndugu yangu Mheshimiwa Mwijage kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuleta hamasa kwa Watanzania kuona umuhimu wa kumiliki viwanda. Amefanya kazi kubwa ya kuwahamasisha Watanzania kubadili mitazamo ya uwekezaji ili wajielekeze kwenye kumiliki viwanda; viwe viwanda vidogo, viwanda vya kati, lakini vile vile viwanda vikubwa. Hongera sana, ameitendea haki taalum yake ya Masoko. Naomba sasa hili lisiwe jukumu lake peke yake, Wizara ilichukue hili kwa ujumla wake. Ongezeni nguvu katika kuhamasisha Watanzania wabadilishe mitazamo katika umiliki wa viwanda katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, nataka nieleze masikitiko yangu; pamoja na nia nzuri ya kuanzisha viwanda, lakini yapo mambo yanakwamisha sana ukuzaji wa viwanda katika nchi yetu. Ukifuatilia mijadala na sisi tunaopitia pitia tafiti zinazofanyika katika nchi hii, moja kubwa ni lack of coordination. Kuna maeneo tunakwenda hatua moja mbele, tunarudi hatua mbili nyuma; na nitatoa mfano.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nataka nizungumzie Sekta ya Maziwa. Utafiti wa wenzetu wa ESRF unaonesha kwamba mwaka 2010 tulikuwa tunaingiza maziwa kutoka nje takriban lita milioni 40 zenye thamani ya dola milioni 20. Ilipofika mwaka 2014 uingizaji wa maziwa ukaongezeka kutoka lita milioni 40 ukapanda mpaka lita milioni 70 zenye thamani ya dola milioni 40. Unaweza kuona ni jinsi gani tunapoteza fedha kwa kuingiza maziwa kutoka nje. Wakati tukiingiza maziwa kwa kiasi hicho, sisi tunazalisha takriban lita bilioni mbili, lakini zinazosindikwa hazifiki lita 150,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia 62 ya maziwa tunayoingiza yanatoka Kenya, asilimia 32 yanatoka South Africa, asilimia nne Uganda. Hata haya yanayopitia South Africa, kuna walakini mkubwa. Tunaambiwa ni uchochoro wa kukwepa kodi. Nitayasema baadaye haya. Masikitiko yangu ni yapi? Kiwanda cha Tanga Fresh ambacho ndiyo kinazalisha kwa wingi sasa, kinazalisha lita 50,000 kwa siku. Ni kiwanda ambacho tulitakiwa kukilinda kwa nguvu zetu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda hiki miaka minne iliyopita, walitaka kuongeza uzalishaji kutoka lita 50,000 kwenda lita 120,000 na tulikuwa tumepata grant ya kuweza kufanya jukumu hilo. Wenzetu wa Bodi ya Ushindani wakawapiga faini ya shilingi bilioni nne wakisema walinunua assets kinyume na utaratibu. Assets zilizonunuliwa zilikuwa za kiwanda kilichokufa, kwa hiyo, hoja ya kuua ushindani haipo. Tumeminyana, faini ile imepungua mpaka sasa hivi bado imeng’ang’aniwa shilingi milioni 400. Hiki ni kiwanda ambacho kingeongeza uzalishaji katika nchi yetu. Fedha ile imepotea! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanga Fresh wameamua kukopa sasa. Wanataka kutumia assets zao, majengo yao waende wakakope. TRA wanakuja wanazuia wanasema hawawezi kutumia majengo yale kukopa kwa sababu aliyewauzia hakulipa kodi stahiki. Vitu vya ajabu sana! Yaani aliyekwepa kodi yupo, anajulikana; anaendelea kufanya biashara kwenye nchi hii, TRA, hawaendi kumbana, wanaenda kumbana Tanga Fresh ambaye hahusiki. Mambo ya ovyo sana! Tunashindwa kukuza viwanda vyetu kwa mambo ya ovyo kiasi hiki! Leo hii ninapozungumza, vituo 28 vya kukusanya maziwa kule Morogoro vimefungwa, wananchi hawana sehemu ya kuuzia maziwa yao kwa sababu hayawezi kupokelewa Tanga Fresh. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanga Fresh wananunua maziwa Mkoa mzima wa Tanga; Tanga Fresh wananunua maziwa kutoka kwa wakulima Mkoa wa Pwani; Tanga Fresh wananunua maziwa kutoka Morogoro. Hivi ninavyozungumza, Tanga Fresh wameombwa na wakulima kutoka Mbeya wanunue maziwa yao, wanashindwa! Maziwa yanamwagwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaingiza maziwa ya mabilioni haya kutoka Kenya, halafu tunakuja hapa tunasema tunataka kuendeleza viwanda, hii haiwezi kuwa sawa. Napiga kelele kwa Mheshimiwa Waziri wa Viwanda kwa sababu sera ya ukuzaji wa viwanda iko kwake, lakini najua mchawi wetu hapa ni Wizara ya Fedha. Najua jitihada alizofanya ndugu yangu Mheshimiwa Mwijage ili jambo hili liishe, lakini barua ile aliyoandika mpaka leo imekaliwa pale Wizara ya Fedha hakuna kinachoendelea. Tutaendelea namna hii namna gani? Lazima tubadilike. Naiomba Serikali yangu jambo hili lishughulikieni, tuondoleeni aibu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kichekesho kingine, tulipitisha hapa Sheria ya VAT kwenye bidhaa za maziwa, tuliingizwa mkenge na wenzetu Kenya lakini Kenya wananchi walipopiga kelele, wenzetu wakafuta kodi ile, sisi tumeendelea nayo. Wabunge tukisimama tukisema hapa, tunaonekana vituko. Tuliyasema hapa kwenye Sekta ya Utalii hatukusikilizwa, Sekta ya Maziwa nayo imeingiliwa, hebu tuwe smart; tunapokubaliana na hawa wenzetu, tukiona wamekiuka makubaliano, mara moja na sisi tugeuke. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu korosho; nilikuwa Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Viwanda, kipindi kilichopita, tuliahidiwa viwanda sita vya Korosho, leo hii havipo. Ndugu yangu Mheshimiwa Mwijage, taarifa za Bodi ya Korosho wanatuambia mwaka huu, tani zilizouzwa korosho ghafi, tani 260,000 tusiendelee kuangalia jambo hili, tutumie Mfuko ule wa Export Levy kujenga viwanda. Nendeni mkafanye utafiti tujue, kama tunataka korosho yetu ibanguliwe hapa, angalau nusu ya tani hizi, tunahitaji viwanda vingapi, tutengeneze Mfuko wa Mikopo kutokana na Export Processing Levy tuitangaze, watu waje wakope fedha zile tujenge viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru na naunga mkono hoja.