Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi kwa mara ya pili kujadili bajeti hii ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilishatoa pole kwa wale ambao walifiwa kwenye maafa mbalimbali hivyo naomba niende moja kwa moja kwenye hoja hii ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda ni lazima kwa ustawi wa wananchi wa nchi yoyote. Ninasema hivi kwa sababu viwanda na kilimo kwa pamoja ndivyo vinavyosaidia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa uchumi wa nchi na maendeleo yake, huo ndio ukweli. Kwa hiyo, kama nchi haisisitizi viwanda na kilimo hakitaendelea kwa sababu kilimo kwa kiasi kikubwa kinasaidiana sana na viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kuipongeza Serikali na siipongezi tu kwa maneno na kwa vitendo kwa sababu sekta hii imekuwa kwa asilimia 7.8 ukilinganisha na ukuaji wake mwaka uliopita wa asilimia 6.5, na imekuwa ikikuwa hivi wakati zamani ukuaji wa viwanda ulikuwa chini. Ukuaji huu umetokana na sera nzuri ambayo kuna wengine walisema imekaa muda mrefu, Sera ya Maendeleo (Sustainable Industrial Development) ya mwaka 1996 mpaka 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uzuri wa sera ni kukaa muda wa kutosha ili muda wa utekelezaji uwe unatosheleza. Kwa hivyo, ninaomba niipongeze wizara hii kwa kuendelea kutekeleza sera hii ambayo kwa kiasi kikubwa inataka viwanda visambae nchi nzima na vifike hata kule pembezoni ili maendeleo ya nchi yawe na uwiano mzuri. Kwa hivyo, ni sera nzuri ninaomba tuendelee kuitekeleza, na mwaka 2020 utakapofika tutaifanyia kazi changamoto ili tuboreshe sera nyingine itakayofuata.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kutokana na sera hii SIDO imekuwa na program inayoitwa MUVI ambapo imetaka kila mkoa uwe na viwanda ambavyo una malighafi yake na ili uwiano wa maendeleo kwenye mikoa yetu iweze kufanana. Hii programu karibu itakwisha. Ninaomba Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji ijiandae baada ya MUVI kutakuwa na nini? Kwa sababu mwenendo na mwelekeo wa MUVI ni mzuri sana. Unapokuwa na specialization kwa kila mkoa unawezesha kuwe na biashara kutoka mkoa hadi mkoa, na ndiyo baishara ya ndani itakavyokuwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nataka nitoe mfano kwa Wilaya yangu ya Hanang ambapo ilipangiwa kutengeneza kuwa na viwanda vidogo vya ngozi kwa sababu sisi ni wafugaji na mazao mengine yanayotokana na mifugo na Singida imepewa specialization ya mafuta ya alizeti kwa sababu inalima alizeti. Kwa hiyo, watu wa Singida watakuja kununua bidhaa za ngozi kwetu na sisi tunanunua mafuta kule. Tukiwa na utaratibu wa namna hii nchi nzima tutaendelea na maendeleo yatakuwa na uwiano mzuri, hakutakuwa na mahali ambapo patabaki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba MUVI ifuatiliwe ili muda wake utakapokwisha tuwe na programu nyingine nzuri, na tumeifanya program; mimi nasema hivyo kwa sababu nilikuwa Wizara ya Viwanda; ili muda wake usiishe, huu si mradi ni programu na programu haina mwisho wake. Kwa hivyo ndugu zangu ninaomba sana tufanye hivyo ili tuongeze ajira kwa watu wetu, ili tuongeze mauzo ya nje. Nilipokuwa Wizara ya Viwanda tulikazana, kuna miaka miwili tulipita mauzo ya kwenda Kenya kuliko ununuzi wa bidhaa kutoka Kenya, inawezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama mtajitahidi kutekeleza sera hii ya sustainable Industrial Development tutafika pazuri na hata tutaipita hii Kenya kwa sababu sisi tuna resources au maliasili nyingi kuliko hiyo Kenya ambayo inatupita kwa viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili viwanda vilete manufaa nchini lazima tuwe na uwiano mzuri. Kwa sasa hivi kwa mujibu wa hiki kitabu cha Mheshimiwa Waziri viwanda vidogo sana ni asilimi 85, viwanda vidogo asilimia 14, viwanda vya kati asilimia 0.35, viwanda vikubwa asilimia 0.5 uwiano huuu si mzuri. Tunataka tuwe na uwiano mzuri wa viwanda vidogo kuwa vingi kama asilimi 65; vya kati vifuate na vikubwa hata vikiwa asilimia 5 haitakuwa mbaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, uwiano huu utatusaidia sana kuona kwamba malighafi zinatumika vya kutosha, itatufanya tuone kwamba mazao ya kilimo yanapata masoko kwa sababu viwanda ndio soko la uhakika la mazao ya kilimo. Vilevile itaajiri wananchi wengi. Hata hivyo ajira imeongezeka. Mwaka 2016 viwanda viliajiri watu 146,892 ukilinganisha na mwaka jana ambapo 139,000 waliajiriwa, kwa hivyo, trend ni kukua lakini ajira hii haitoshi na ndio maana nasisitiza umuhimu wa uwiano wa viwanda.

Ninaomba niongelee kidogo Kurasini Logistic Center, sijui mtakuwa mmefika wapi jamani. Tulianzisha Logistic Center ya Kurasini ili tuweze kuagiza vitu kwa bulk purchases na wafanyabiashara wa Kongo, Rwanda waje pale ili Kariakoo iwe Hong Kong ya Afrika, hilo ni moja. Hata hivyo kuna watu wanaogopa kwamba tutakuwa tunaagiza vitu kutoka China. Kutokana na Logistic Center tutajua mahitaji ya watu na nchi ambazo zinazunguka Tanzania na viwanda vitaanzishwa kwa haraka sana.

Kwa hiyo naomba sana Logistic Center ianze. Vilevile nataka tuongeze mauzo kwenda nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru lakini ninaomba Liganga ni kiwanda mama tukisisitize kianzishwe. Ninaunga mkono na ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri wetu anafanya kazi nzuri.