Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Naibu Spika nikushukuru kunipa fursa hii ya kuchangia katika hoja iliyokuwa mbele yetu, na nitangulie kwa kuunga mkono hoja. Naomba kuchukua fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri ya bajeti pamoja na utekelezaji mzuri wa Ilani wa Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kuchukua fursa hii kuipongeza Serikali kwa utekelezaji wa mkakati wa ujenzi wa viwanda ili Tanzania iweze kufikia hadhi ya nchi ya uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025. Hili ni jambo jema sana ni jambo lenye tija kwa uchumi wa nchi yetu Tanzania lakini ni ukombozi kwa mamilioni ya vijana wa Tanzania wa kike na wakiume.

Mheshimiwa Naibu Spika, shida kubwa ya vijana wetu wa kike na wa kiume wanaoingia kwenye soko la ajira sasa hivi ni ukosefu wa kazi, ujenzi wa viwanda maana yake viwanda vingi maana yake ni ajira nyingi. Tutawapa hadhi vijana wa Kitanzania watajisikia binadamu, watajisikia kuwa na heshima na wataweza kuchangia maendeleo ya nchi yao kwa kiasi kikubwa iwezekanavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri katika Jimbo langu la Bagamoyo Serikali imetenga ardhi, jumla ya hekta 9,080 ama kwa kipimo cha ekari 22,700 hili ni kwa ajili ya ujenzi wa viwanda katika kata ya Zinga na kata ya Kiromo jumla ya vijiji vitano vitahusika na mradi huu. Tathmini imefanywa mwaka 2008 jumla ya wafidiwa 2,180 na kwa kipindi hicho thamani ya fidia ilikuwa shilingi bilioni 60, mpaka hivi sasa Serikali imelipa bilioni 26.4 kwa wafidiwa 1,155. Kwa hiyo, kuna wafidiwa 1,025 ambao bado hawajapata fidia.

Mheshimiwa Naibu Spika na Mheshimiwa Waziri mwaka 2008 mpaka leo mwaka 2017 ni jumla ya miaka kumi sasa. Mheshimiwa Waziri ungekuwa kule kijijini ujifanye wewe ni mzee kijijini kule Kagera mwaka 2008 shamba lako na nyumba limezuiliwa na Serikali ili liweze kufanywa mradi wa EPZ na ukazuiliwa kufanya maendelezo katika nyumba ile, ukazuiliwa kufanya maendelezo katika shamba lako, usubiri fidia kwa miaka kumi, fidia usiione. Mheshimiwa Waziri saa hizi baada ya miaka kumi hali ya nyumba yako ikoje, hali ya shamba lako ikoje, hali ya maisha yako kwa ujumla na familia yako ingekuwa namna gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hayo ndiyo madhira ya wananchi wa Bagamoyo ambao tangu mwaka 2008 wamezuiliwa maeneo yao kwa ajili ya ujenzi wa viwanda, wako katika hali mbaya sana. Mimi kama Mbunge nashindwa kupita hawanielewi, hakuna jambo ambalo naweza nikawaambia wakanisikiliza. Sasa hivi Mheshimiwa Waziri una fursa kubwa hii ya azma nzuri ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kujenga viwanda, viwanda havijengwi hewani vinajegwa ardhini lazima ardhi hii iweze kulipiwa hivi sasa baada ya miaka kumi ili wananchi nao wajisikie nao wako katika nchi yao huru na wanaweza wakaendeleza maisha yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri utakapokuja kujumuisha hoja yako unipe, ama utupe majibu mazuri na ya uhakika kwamba ni lini wananchi hawa wa Zinga, Kondo, Pande na Kiromo watalipwa fidia zao kwa sababu Mheshimiwa Waziri kwa madhira haya, wewe ni rafiki yangu na mimi nilishawahi kuwa kwenye Serikali nitaona aibu sana lakini nitakuwa sina namna nyingine bali kutangaza azma yangu ya kushikilia shilingi kama sitapata majibu ya uhakika, kwamba lini wananchi hawa watalipwa fidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri amesema pia katika hotuba yake kwamba fidia hizi inategemewa zitalipwa na mwekezaji mwenyewe jambo zuri, lakini Mheshimiwa Waziri niulize, kwa nini Serikali imebadilisha utaratibu, utaratibu ambao tumejiwekea kwamba fidia za ardhi ya wananchi wetu tulikuwa tunazilipa sisi wenyewe kama Serikali, mwaka 2012/2013 kwa ajili ya mradi wa EPZ, tulitenga shilingi bilioni 50 lakini zilitoka bilioni 10.9, mwaka 2013/2014 tulitenga bilioni tisa zikatoka bilioni tatu, mwaka 2014/2015 tulitenga shilingi bilioni saba, zikatoka bilioni saba zote na huo ndiyo ulikuwa utaratibu wakati wote tunaposema kwamba mwekezaji alipie fidia ya ardhi maana yake tunapunguza vivutio kwa wawekezaji hao na mitaji inatafutwa dunia nzima, unapopata mtu ana mtaji basi huyo ni wa kumshikilia na kimojawapo ni kigezo hiki ambacho Serikali inaweza ikalipia fidia zake kama tulivyokuwa tunafanya lakini pia nimuambie Mheshiwa Waziri hata kama mwekezaji atalipa fidia katika eneo hili eneo la EPZ ni hekta 9,080 na mwekezaji yule amesema ata develop hekta 3000 peke yake, hizi hekta 6000 zingine nani atalipia? miaka 10 baadae nani atalipia?

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi hao wataendelea kuteseka, wananchi hawa wataendelea kuchukia Serikali yao, wananchi hao watashindwa kujiendeleza katika maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa Mheshimiwa Waziri atakapofanya majumuisho atueleze vizuri kwa nini tumefanya mabadiliko haya na uhakika upi utakaotuwezesha wananchi hawa waweze kulipwa fidia zao kikamilifu na mapema.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa pia kuelezea kwamba mradi huu wa Special Economic Zone Bagamoyo unajumuisha pia ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo. Bandari mpya ya Bagamoyo, bandari yenye uwezo mkubwa zaidi kushinda bandari yoyote katika mwambao wa Afrika Mashariki na kusema kweli ni mwambao wa Afrika nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2002 ndiyo kwa mara ya kwanza mwezi Septemba tulisaini MoU ya ujenzi wa bandari, na mwaka 2013 Machi, Rais Xi Jinping wa Serikali ya China na aliyekuwa Rais wa Tanzania, walishuhudia kutiwa saini kwa framework agreement ya ujenzi wa bandari hii, mwezi Machi 2013 mpaka leo ni mwaka wa tano sasa na ni mradi ambao umeshuhudiwa kuwekewa saini na Rais Xi Jinping, tena wakati ule ana wiki chache tu baada ya kuteuliwa kuwa Rais wa Taifa kubwa lile, huo ni mradi muhimu sana kwa nchi ya China. China ni rafiki zetu, China wamekubali kutusaidia, pesa ni ya kwao na tumesaini framework agreement Machi 2013 lakini mpaka sasa hivi miaka Mitano ni muda mrefu hatupaswi kukaa muda huo wakati mtaji tumeushikilia, mtaji huu kila mmoja ndani ya Bara la Afrika na nje ya Afrika wanautafuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipindi hiki tunaongea na China Merchant Port kipindi hiki hawa wa China Merchant Port wamekamilisha maongezi na Serikali ya Sri Lanka sasa hivi wanaendesha Colombo International Container Terminal wamekamilisha maongozi na Togo, wanaendesha Lome Port Container Terminal, wamekamilisha maongezi na Nigeria wanaendesha Tincan Port Island Container Terminal na wamekamilisha miradi kadhaa mingine ambayo kwa ukosefu wa muda sitaweza kuisema, kipindi hiki tangu 2012 mpaka leo tunajadiliana nao mpaka lini?

Mheshimiwa Waziri nakuomba utakapokuja hapa uweze kusema kwamba ni lini bandari hii itajengwa, lini tutakamilisha maongezi na China Merchant Port?

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili la bandari nalo pia lina mgogoro wa fidia, wananchi 687 walipunjwa fidia zao, Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo alithibitisha hivyo na Mthamini Mkuu wa Serikali ameshafanyia tathimini tayari. Mheshimiwa Waziri ndani ya bajeti yako hakuna pesa za kuwalipa hawa wananchi, naomba utakapotoa majumuisho utuambie hawa wananchi 687 waliopunjwa fidia yao watalipwa lini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala kubwa zaidi, katika kipindi hiki cha maandalizi Serikali iliwaahidi wananchi hawa jumla ya kaya 2000, kwamba itawahamishia mahali pengine na shule yao ya msingi ya Pande itajengwa huko, zahanati yao waliyojenga kwa nguvu zao wananchi na nguvu za wahisani itahamishiwa kule, Ofisi ya Serikali ya Kijiji itahamishiwa kule, nyumba zao za ibada, makanisa na misikiti itajengwa kule ili wawe na makazi mapya. Nyumba watajenga wenyewe lakini miundombinu hii ya jamii itajengwa kule, hili jambo halijatokea mpaka hivi sasa, na wananchi hawa wanaishi kwa wasiwasi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara yako ya Viwanda ambaye wakati ule alikuwa DG wa EPZA anakumbuka safari zangu nyingi ambazo nilikuwa nimeenda kule EPZA kufuatilia jambo la makazi mapya.

Mheshimiwa Waziri utakapofanya majumuisho tafadhali chonde chonde uwaambie wananchi wa Bagamoyo hao wanaopisha bandari lini watapata makazi yao mapya ili waondoke pale na nchi yetu iweze kujenga bandari mapema iwezekanavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa muda ulionipa na naunga mkono hoja, ahsante sana.