Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa fursa hii. Naomba nichangie kidogo Hoja hii ya Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia kwenye maeneo mawili, eneo la kwanza linahusu hoja ambayo ipo katika kitabu cha Msemaji Mkuu wa Kambi Rasmi ya Upinzani kwa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, ambapo kwenye ukurasa wa 17 na kuendelea anazungumzia kuhusu uteuzi wa wanajeshi, ama wanajeshi ambao bado ni wanajeshi au wanajeshi waliostaafu kwenye nafasi mbalimbali za kiuongozi kama wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Msemaji huyu wa Kambi Rasmi ya Upinzani anazungumzia kwamba hii ni sawasawa na dhana ya politicization of the Army. Napenda kupingana naye kwa sababu politicization of the Army haipo katika zama hizi kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema haipo kwa sababu kinachofanyika kwa sasa kimsingi ni kwamba Mheshimiwa Rais anatumia mamlaka yake ambayo yamekuwa provided for kwenye Katiba yetu kuteua watu ambao anaona watafaa kwenye maeneo mbalimbali ya uongozi na kuwapa madaraka ya kumsaidia kazi ya kuongoza nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna maeneo yamekaa kimkakati (strategic regions) kama Kigoma ni mpakani, Kagera pamoja na maeneo ya Ruvuma. Maeneo ambayo yamekaa kimkakati kwa maana ya kiulinzi zaidi Mheshimiwa Rais anaona watu ambao wana inclination ya kijeshi aidha ni wanajeshi au ni wanajeshi wastaafu wanafaa kwenda kumsaidia kuongoza katika maeneo yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa napenda kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayofanya.

T A A R I F A . . .

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kitabu hakuna mahali ambapo wanaelezea mwanajeshi hata mmoja ambaye ameteuliwa na Mheshimiwa Rais kuwa Mkuu wa Mkoa ambaye amekiuka taratibu anazozizungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi, tunachokiona ni kwamba Mheshimiwa Rais amewateua watu ambao anaona watafaa kumsaidia kutekeleza majukumu yake ya kuongoza nchi yetu na kulinda mipaka yetu na kuleta amani ndani ya nchi na kusaidia kuleta amani kwa watu ambao wanatuzunguka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msingi huo nashindwa kuelewa wanatoa wapi dhana kwamba Jeshi letu linakuwa politicized. Kwa sababu hawezi leo hii Mheshimiwa Waitara kuweka Mezani hapa hata photocopy tu ya kadi ya mwanajeshi hata mmoja ambaye amejiunga na CCM, hawezi kuweka Mezani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachoweza kuzungumzika ni kwamba anahisi kwa sababu kwenye Katiba ya CCM ukiwa Mkuu wa Mkoa ama Mkuu wa Wilaya unakuwa Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya Chama cha Mapinduzi anahisi na hao wanajeshi pengine baada ya kuteuliwa kushika haya mamlaka mbalimbali kama Mkuu wa Wilaya ama Mkuu wa Mkoa basi wanaingia kwenye vikao vya Kamati ya Siasa ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna ushahidi wowote wa hilo na naweza kusema kwamba kwa sababu Ilani inayoongoza Taifa letu ya mtu ambaye amechaguliwa na wananchi, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ni ya Chama cha Mapinduzi na ili ilani hii isimamiwe na chama ambacho kinaongoza dola ni lazima wale ambao wamepewa nafasi ya kusimamia utekelezaji wa ilani hiyo waweze kutoa taarifa ndani ya chama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama italazimika Mkuu wa Mkoa kwenda kutoa taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi kwenye Kamati ya Siasa na yeye ni mwanajeshi, atakwenda kutoa taarifa hiyo. Kwa sababu huwezi kutenganisha uongozi wa nchi hii ambao Chama cha Mapinduzi kimepewa dhamana na wananchi kupitia kura kwa kumchagua Mheshimiwa Rais anayetokana na Chama cha Mapinduzi na utendaji wa kila siku wa chama, haiwezekani, ni dhana ambayo haipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na kwamba, Chama cha Mapinduzi kilimsimamisha Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Rais akachaguliwa na wananchi na baada ya kuchaguliwa sasa anatekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama chake, watu aliowateua ni lazima waende wakakieleze chama nini wanafanya kwenye nafasi mbalimbali walizopewa kwenye maeneo yao. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.