Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa

Hon. Halima Ali Mohammed

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018 - Waziri wa Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa

MHE. HALIMA ALI MOHAMMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa 33 aya 46 Mheshimiwa Waziri ameelezea kuhusiana na SUMA JKT kupitia kampuni yake ya SUMA JKT Guard Ltd. kuendesha shughuli za ulinzi katika Ofisi za Serikali, Mashirika ya Umma na sekta binafsi zikiwemo Benki na Migodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walinzi hawa maisha yao ni magumu, posho ni ndogo sana, mishahara hawana na Serikali iliwaahidi itawapatia mishahara kamili kama askari wengine. Nitoe mfano, walinzi wanaoimarisha ulinzi Ofisi ya TRA Bandarini, kazi wanayofanya ni nzuri tena katika ofisi nyeti, lakini Serikali haijali kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali iangalie upya maslahi ya walinzi hawa, iwaboreshee mishahara, iwapatie vitendea kazi pamoja na stahiki nyingine, kwani sehemu ya bandari ni muhimu katika kuingiza mapato ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kuhusu malipo ya wastaafu wa JWTZ. Hawa ni watumishi ambao walifanya kazi kubwa ya kulinda nchi yetu, kuweka heshima, lakini pia kuimarisha ujirani mwema. Siyo vyema kuwa sasa hivi wao ni ombaomba. Nashauri wapewe stahiki zao kwa kuzingatia thamani ya shilingi ya Kitanzania kwa sasa au mnawasubiri wafe wote? Hilo siyo jambo zuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wako wananchi eneo la Kengeja, Jimbo la Mtambile, Wilaya ya Kusini Pemba ambao ardhi yao imechukuliwa na JWTZ. Hadi hii leo ni kimya, hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa na ni maeneo ambayo wanayategemea kwa kilimo cha chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali uthamini ufanyike kwa haraka. Mheshimiwa Waziri atoe kauli ni lini wananchi hawa watapatiwa haki zao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi ya majeshi ya JWTZ wakati wa uchaguzi kwa mfano, uchaguzi mdogo wa Jimbo la Dimani - Zanzibar ni uthibitisho kuwa na matumizi mabaya ya Jeshi letu, matumizi mabaya ya fedha za walipa kodi, lakini siyo hivyo tu, ni uminyaji wa demokrasia, kwani walikuwa wakipita njiani na silaha. Hii inawatisha wananchi na matokeo yake wapo wananchi wengi tu ambao waliogopa na hawakujitokeza kutimiza haki yao ya kupiga kura. Hii ni aibu kwa nchi inayojigamba kama ina demokrasia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe ushauri, Serikali isitumie madaraka vibaya, badala yake wanajeshi wa JWTZ waachiwe wafanye majukumu yao kwa mujibu wa sheria za nchi yetu kwa manufaa ya ustawi wa nchi yetu na wanasiasa wafanye siasa. Kutumia fedha za walipakodi kwa jambo ambalo halina msingi, ni kuwanyima wananchi kutumia haki yao ya maamuzi na kuwanyima nafasi ya kupata maendeleo. Ahsante sana.