Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nianze kwa kupongeza sana juhudi zinazofanywa na Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi. Kwa hakika maneno haya hata kama kuna mtu anasema kwake hayajafanyika, lakini Chalinze wanaopita kwenye barabara wameshayaona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo nimeona kwenye TV hapa wawekezaji wangu wamekuja. Ningependa nitambue uwepo wa bwana Jack Feng na ndugu yangu Beda kwa kweli, wananifanya leo hii ninaposimama hapa na ninapotazama kitabu hiki natamba na Mheshimiwa Mwijage anatamba ni kwa sababu yao. Nawashukuruni sana. Kama mnavyoona kwenye TV pale bwana Jack Feng na bwana Beda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mambo mazuri ambayo Serikali yangu imeendelea kufanya, lakini bado zimebakia changamoto na yako maeneo ambayo mimi kwa nafasi yangu kama Mbunge ningependa nitoe ushauri maana maongezi yangu leo yamejikita sana kwenye ushauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, viwanda na maji. Kule kwangu mimi viwanda vyangu vyote ninavyotengeneza vyote vinahitaji maji. Tunapozungumzia viwanda vya vigae, mahitaji ya maji ni makubwa sana, lakini pia, nazungumzia viwanda vya mazao yanayotokana na matunda, mahitaji ni makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri ameeleza katika Hotuba yake ya Bajeti juu ya ukubwa wa viwanda hivi na vitu ambavyo vitaendelea kuchukuliwa pale. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri na huu ni ushauri wa dhati kabisa toka moyoni mwangu Wakae na Waziri wa Maji waulizane juu ya jinsi gani lile jambo linalokabili Kiwanda cha Sayona Fruits Processing pale Mboga, watakavyoweza kulimaliza. Mheshimiwa Waziri wa Maji ametoa ahadi alipokuwa anafanya majumuisho ya hotuba yake akisema kwamba jambo hilo tutaliangalia.

Mheshimiwa Naibu Spika, najua Mheshimiwa Waziri anaweza kwenda mbio sana, hebu ajaribu kukamatana na Mheshimiwa Waziri wa Maji ili tuweze kulifikisha jambo hili pazuri na ile ahadi ya kusema kwamba mwezi wa 10 Mungu akijalia Mheshimiwa Rais aje Chalinze kuja kuzindua kiwanda kile iwezekane. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo pia, tulifanya mazungumzo na wenzetu wa TWYFORD ambao wanaonekana kwenye TV hapo; kwamba kubwa zaidi ambalo wao wanalitaka ni Serikali iwape ruksa ya kuweza kuchukua maji kutoka Mto Ruvu ili waweze kuyavuta mpaka pale kwenye kiwanda chao, lakini pia waweze kutengeneza maji ambayo watayafikisha katika maeneo mengine ya Chalinze.

Mheshimiwa Naibu Spika, najua Mheshimiwa Waziri ni binadamu sana, najua kwamba katika kuwapa kibali hicho hatowasahau wananchi wa Kata za Vigwaza, Pera pamoja na Bwilingu kwa sababu maji hayo yanayohitajika yakienda kiwandani kama hayatakwenda kwa wananchi huenda tukakuta siku moja mwekezaji analalamika kwamba, maji hayaendi kwa sababu wananchi wametoboa mabomba. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri jambo hili aliwekee mkakati mzuri ili tuweze kufanikisha haya mambo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo liko jambo la Bandari ya Bagamoyo. Mheshimiwa Waziri nimetazama kitabu chake chote hiki, hakuna sehemu ambayo amezungumzia Bandari ya Bagamoyo na viwanda vinavyotakiwa vijengwe katika Special Economic Zone. Si hilo tu, Mheshimiwa Waziri wakati anatoa pale ambayo mimi naiita summary ya kitabu hiki amejitahidi kuielezea Bagamoyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka nimuulize swali Mheshimiwa Waziri niamini yapi, niamini aliyoyasema akiwa pale au niamini ambayo amendika kwenye kitabu hiki? Hili ni jambo ambalo Wanabagamoyo wangependa sana kulijua kwa sababu, uchumi wa maeneo ya Bagamoyo na Tanzania kwa ujumla wake unategemea sana uwepo wa bandari ile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, si hilo tu, Mheshimiwa Waziri amezungumza kwamba mwekezaji yuko tayari kwa ajili ya kulipa lile, lakini kwa maelezo aliyoyatoa Mheshimiwa Waziri nabaki na maswali ya kuuliza lini fidia hizo za wananchi wale wa Pande, Mlingotini na maeneo mengine ya Kata ya Kiromo wataweza kulipwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hata kama wanataka kulipa ni jinsi gani anakuja kulipa mtu huyo? Kwa sababu fedha hizi ambazo tunazungumza hapa ni fedha za mwekezaji, lakini mwekezaji huyu anapata wapi taarifa juu ya mahitaji ya watu wale? Vile vile anaweza vipi kutambua watu wale kwa sababu niliposikiliza maneno yake naona kama kuna utaratibu wa Serikali kujitoa na kuliacha eneo lile ambalo sisi Wanatanzania tunategemea kwamba, liwe ndio sehemu ya ukombozi mkuu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Mheshimiwa Waziri amezungumza juu ya mambo mengi ambayo nchi yetu inafanya. Hata hivyo, viwanda hivi vinavyojengwa katika eneo la Chalinze in particular ni viwanda vikubwa sana, lakini mwekezaji wangu, kwa mfano Sayona ambaye anajenga kiwanda kikubwa cha matunda ambapo ndani ya kitabu chake ukurasa wa 23 ameeleza juu ya ukubwa huo, lakini pia ameeleza juu ya umuhimu wa kiwanda hicho, lakini mwekezaji huyu anahangaika mpaka leo kutafuta Strategic Investment Certificate. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri anajua, kwa wawekezaji ambao watahitaji bidhaa za Tanzania nzima, kwa wawekezaji ambao watatoa ajira zaidi ya watu 29,000, kwa wawekezaji ambao watachukua matunda na watatoa production ya lita zaidi ya milioni mia mbili kwa mwaka, huyu mtu ana kigezo chote cha kupewa Certificate ya Strategic Investment. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufanya majumuisho yake atueleze sisi Wanachalinze na Watanzania kwamba, amejipangaje katika kuhakikisha kwamba, mwekezaji huyu anapewa hiyo Certificate ili mambo yaende vizuri katika eneo lile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho lakini sio mwisho kwa umuhimu, Mheshimiwa Waziri kuna Kiwanda cha Nyama cha Ruvu, kimekufa na hakuna dalili ya kufufuka. Mheshimiwa Waziri anajua wakati kaka yangu, rafiki yangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba akiwa kwenye Wizara ya Kilimo, nilipata nafasi ya kwenda naye pale kwenye kiwanda akaona.

Mheshimiwa Naibu Spika, si hilo tu, Serikali katika kuonesha kwamba, iko tayari kuhakikisha kwamba kiwanda kile kinafufuka ilinunua mashine nzuri kwa ajili ya kuja kufunga ili kiwanda kiweze kufanya kazi, lakini la kushangaza kiwanda kile na mashine zilizopo pale havifanani. Kwa hiyo, kukawa na mapendekezo ya kukipanua lakini mpaka sasa hivi hakuna juhudi zozote wala maelezo yoyote katika Kitabu cha Bajeti cha Mheshimiwa Waziri ambayo yanaeleza juu ya mkakati wake kama Waziri au kama Wizara juu ya kuhakikisha kwamba, kiwanda kile kinafufuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nimwambie tu Mheshimiwa Waziri, tunapolia vilio vya mifugo katika Jimbo la Chalinze, tunapolia vilio vya mifugo katika Tanzania, jibu lake ni kuwa na viwanda vya kusindika na kuchakata nyama kama hivi ambavyo vinatakiwa vifanye kazi. Mheshimiwa Waziri aisaidie nchi yake, akisaidie chama chako, tunahitaji kuweka utaratibu ulio mzuri ili mambo yaweze kwenda vizuri katika Tanzania yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, maana sisi Wanasiasa tuna mwisho na mwisho kabisa! Sasa hapa mwisho kabisa, Mheshimiwa Waziri katika uwekezaji lazima kuwe na utayari wa Serikali. Utayari huo nimeuona, lakini nataka niuone kwa vitendo. Mheshimiwa Waziri…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono sana hoja ya Mheshimiwa Waziri. Ahsante sana.