Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Hawa Subira Mwaifunga

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Awali ya yote ningependa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya na kuweza kusimama katika Bunge hili Tukufu ili niweze kuchangia hotuba ya Wizara ya Viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze na Mkoa wa Tabora. Siku zote mcheza kwao hutunzwa. Waheshimiwa Wabunge wa Mkoa wa Tabora siku zote wamekuwa wakipiga kelele kuhusiana na suala zima la viwanda, Mheshimiwa Waziri Mwijage anafahamu, watendaji wake wote wanafahamu na wakati wote wamekuwa wakitupa ahadi za kwamba watatuletea wawekezaji katika mkoa wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Tabora kuna Kiwanda cha Nyuzi, kiwanda hiki alipewa mwekezaji mwenye asili ya Asia. Baada ya mwekezaji huyu kupewa kiwanda kile kitu kikubwa ambacho ameweza kukifanya katika kiwanda cha nyuzi ni kuondoa mitambo yote iliyokuwepo pale kwenye kiwanda kile kuisafirisha na kuipeleka kwao na kutuachia hall pale katika kiwanda kile.

Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumza hili kwa sababu nina ushahidi nalo. Ukienda katika kiwanda kile huwezi kumkuta mfanyakazi hata mmoja zaidi ya Wahindi wawili ambao wanazunguka katika kiwanda kile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda kile hakinufaishi vijana wa Tabora, hakinufaishi wazawa wa Tabora na wala hakinufaishi wanawake wa Mkoa wa Tabora.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa masikitiko makubwa mwekezaji huyu aliamua kwenda mbali zaidi hadi kuamua kuuza majengo yaliyokuwa yanamilikiwa na kiwanda kile. Leo majengo yale yanatumiwa na Ofisi ya Uhamiaji pale juu, ukienda pale kwenye barabara ya Kilimatinde kuelekea kule njia ya kwenda Jimbo la Igalula utaona yale majengo. Juu wameweka ofisi ya uhamiaji chini yapo magofu tu ambayo haieleweki yanafanya kazi gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Mheshimiwa Waziri atuambie ni lini basi watamwondoa mwekezaji huyu, watuletee mwekezaji mwenye nia thabiti ya kuwekeza katika Kiwanda cha Nyuzi? Malighafi za uwekezaji katika kiwanda kile zipo kwa sababu Tabora tunalima pamba, lakini pia majirani zetu wa Kahama, Shinyanga na maeneo mengine yanayolima pamba tunayopakana nayo yanaweza kufikisha malighafi zile kwa urahisi na kile kiwanda kikaendelea kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri kutuletea mwekezaji imeshindikana, kiwanda tunacho, mwekezaji waliomuweka hafai, tunaomba sana waende wakapitie kiwanda kile wakiangalie, tukifufue kiwanda cha nyuzi na sisi wananchi wa Mkoa wa Tabora tuweze kunufaika na rasilimali hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Tabora kuna jengo la SIDO. Kwa masikitiko makubwa sana jengo hili haijawahi kuwanufaisha hata siku moja wakazi wa Mkoa wa Tabora. Matokeo yake leo hapa ninavyozungumza, SIDO Mkoa wa Tabora wamekodisha kwa Mratibu wa Mafunzo wa VETA bwana Kaali ambaye ameweka ofisini yake pale na kutengeneza furniture na kuziuza. Hivi ndiyo yaliyokuwa malengo ya SIDO hayo ama ilikuwa ni nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaomba Mheshimiwa Waziri aje anipe majibu ya kunitosheleza ili niweze kujua kwa nini SIDO imepewa mwekezaji eti yeye ndiye anatengeneza makochi yake pale na furniture zake halafu Watanzania wa Mkoa wa Tabora, hawanufaiki na hiyo SIDO. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuzungumzia ya nyumbani kwetu, sasa naomba nizungumze mambo mengine kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, wafanyabiashara wenye viwanda, wamekuwa na malalamiko mengi siku zote na kwa bahati nzuri mimi mwenyewe ni mmoja kati ya wajumbe wa Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira na siku zote malalamiko haya yalipotufikia tumekuwa tukiyafikisha sehemu husika, lakini bado kumekuwa na maendeleo ya kulalamika kwa wafanyabiashara hawa kwamba mambo wanayoyahitaji kwa kweli hayatekelezwi sawasawa na Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunasema tunakwenda kwenye nchi ya viwanda tunakwendaje kwenye nchi ya viwanda waliopo sasa yale wanayolalamikia hayafanyiwi kazi ipasavyo? Tutegemee kulete wawekezaji wengine ili waweze kufanya kitu gani kipya ambacho kitawavutia wale watu?

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali iweze kuangalia hawa wafanyabiashara wetu wenye viwanda nchini. Sasa hivi wafanyabishara wenye viwanda nchini ndio wamekuwa kama vile wanatakiwa wafanye kila jambo. Kosa dogo mfanyabiashara anakwenda kutozwa faini badala mfanyabiashara huyu kupewa maelekezo nini afanye lakini imekuwa wakifika NEMC ni milioni 50, akifika Waziri ni milioni 30, sasa hawa watu watafanya kazi hii kwenye mazingira yapi? Tunawakatisha tamaa, hawa wafanyabiashara wanahitaji kuwekeza, lakini wanashindwa kutokana na mlolongo wa mambo ambayo yanawakera.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfanyabiashara yoyote au mwekezaji anapotoka nje lazima apate mwenyeji kutoka ndani ajue mwenzetu amefikia wapi, anafanya nini kuendeleza kiwanda chake, sasa mwisho wa siku itafika mahali ataanza kuambiwa mabaya kwanza halafu ndipo aambiwe yale yaliyo mema. Zaidi ya amani na utulivu ambayo ataambiwa ndilo litakuwa jambo la kwanza mengine ataambiwa hapo ukifanya hivi tayari, ukifanya hivi tayari, mambo yanakuwa si mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda kilichopo hapa Dodoma (Dodoma Wine) huyu mwekezaji anafanya kazi nzuri kweli kweli, mwekezaji huyu ana wateja wengi kweli kweli, lakini anashindwa kuzalisha kwa ufanisi kwa sababu kila kukicha akifungua ofisi yake watu wa Halmashauri hawa hapa, akifungua ofisi NEMC hawa hapa, akifungua ofisi watu wa mazingira hawa hapa. Wote hawa kila mmoja anakwenda kwa wakati wake na anahitaji fedha kutoka kwa huyu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapo hapo tukumbuke huyu ameajiri, huyu anatakiwa kulipa kodi ya Serikali, huyu anatakiwa kufanya mambo kibao katika nchi hii, anafanyaje biashara zake? Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, hawa wawekezaji wetu wachache tulionao ambao ni waaminifu, waweze kuangaliwa mazingira yao ya kufanyia biashara zao ili waweze kufanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda cha General Tyre kimekuwa ni hadithi za Alfu Lela Ulea. Niseme tu Mheshimiwa Waziri tulikwenda tumetembelea na waliahidi kwamba kiwanda hiki kingefanyiwa upembuzi yakinifu. Mwaka wa jana bajeti yake ilikuwa Sh.150,000,000 kwa ajili ya upembuzi yakinifu, leo imeandikwa Sh.70,000,000, sijui ni kwa ajili ya nini, kwa sababu ni pesa ndogo sana ambayo haiwezi kwenda kufanya huo upembuzi yakinifu ambao wanasema.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo majibu mengine ambayo tumepata ni sasa hivi wanatafuta mwekezaji, kwa hiyo mwekezaji mwenyewe ndio atakayekwenda kufanya huo upembuzi yakinifu. Tunasema ni hadithi za Alfu Lela Ulela kwa sababu haya mambo yameanza kusemwa tangu tukiwa wadogo tunasikia General Tyre mpaka leo bado tunaisikia General Tyre.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wenye viwanda wana malalamiko makubwa sana kuhusiana na umeme usio wa uhakika, umeme unakatikatika wakati wowote. Sasa wale wanapokuwa wameshawasha mashine zao, umeme ukikatika kwa ghafla, ukija kurudi unawasababishia hasara kubwa sana katika mitambo yao kwa sababu umeme unavyorudi haujulikani umerudi kwa nguvu ya aina gani. Kwa hiyo nimwombe Sana Mheshimiwa Waziri kwa kushirikiana na Mheshimiwa wa Nishati waangalie kwa kiasi kikubwa ili kuona ni jinsi gani wanavyoweza kuwasaidia wafanyabiashara kwenye suala zima la umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa na ziara katika Mkoa wa Tanga. Tanga ni moja kati ya mikoa inayoongoza kwa kuwa na viwanda vingi vingi sana, lakini pale Tanga umeme wa uhakika haupo. Hizo megawatt walizopewa na TANESCO haziwatoshi kuweza kuendesha shughuli za viwanda. Kwa hiyo, naomba sana wauangalie mkoa ule ili uweze kufufua vile viwanda na tayari watu wameanza kuamka kuvifufua; waweze kuleta ajira kwa Watanzania hasa vijana na wanawake ambao hawana ajira za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wafanyabiashara wenye viwanda hasa hao wanaofanya biashara ya cement wamekuwa na malalamiko juu ya upendeleo, kwamba kuna baadhi ya wafanyabiashara wanapendelewa kwenye masuala mengine na wao hawapewi upendeleo huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanga Cement wanatengeneza clinker ambayo inatengeneza cement…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi, nimshukuru Waziri Kivuli wa Kambi rasmi ya Upinzani kwa hotuba yake nzuri. Ahsante,