Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Awali ya yote nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi anavyoongoza nchi yetu na kwa jinsi anavyosimamia utendaji wa Serikali tangu aingie madarakani. Ni kiongozi wa mfano na katika mifano yake halisia ameweza kuipeleka nchi na kuweza kuongoza na kutoa dira sahihi kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue pia nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia kufika wakati huu wa sasa sisi Wabunge wote. Pia nichukue nafasi hii kwa niaba ya Waheshimiwa Wabunge wenzangu wote na mimi mwenyewe, wana-Mbulu na Watanzania kwa ujumla kutoa pole nyingi kwa ndugu zetu, marafiki na jamaa wote waliopatwa na hali mbalimbali ya kupoteza ndugu zao katika nyakati tofauti kwa matukio ambayo hatujaweza kuyazoea. Mwenyezi Mungu aendelee kuibariki nchi yetu tuweze kupata hatua nyingine nzuri kwa baraka zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu, Baraza la Mawaziri, Mheshimiwa Spika, wewe mwenyewe na watendaji wote wa Serikali kwa jinsi ambavyo wanajitahidi kutekeleza majukumu yao na kuwapa Watanzania fursa sahihi na nia njema ya kuweza kufanikisha malengo mahsusi kwa Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kutoa mchango mchache ambao natarajia kuzungumza katika Bunge hili kwa nafasi hii ya viwanda. Kwanza kabisa, nichukue nafasi hii kuiasa Serikali; uanzishwaji huu wa viwanda tunaouanzisha hivi sasa ningependa kushauri Serikali ijikite katika hali halisi ya kila Kanda kuwa na kiwanda ili maendeleo yetu yaweze kuendana na sehemu mbalimbali ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa kuna baadhi ya maeneo yatakuwa yamekosa fursa ya kupata viwanda kutokana na hali halisi ya jiografia, rasilimali zilizoko na fursa nyingine za hali ya kupatikana kwa malighafi. Niseme tu kwamba kwa namna yoyote ile tufanye pia utafiti katika nchi yetu ili pia tuweze kuona ni maeneo gani kwa nchi yetu yanaweza kuwa na malighafi ili yale maeneo ambayo hayatapata uwekezaji wa viwanda na fursa za kujengewa viwanda basi waweze kuzalisha na kupata fursa ya kuwa na malighafi ambayo itaendeleza nchi yetu katika hali hii ya viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, mifumo yetu iboreshwe katika uzalishaji na uingizaji wa bidhaa. Nizungumze tu kwamba tukio lile la kuondolewa kwa simu feki katika nchi yetu liliumiza Watanzania wote, Watanzania walikuwa wanahangaika, wakapata simu, wakawa wanamiliki lakini mwishoni tukajikuta simu nyingi zinazomilikiwa hazitaweza kukidhi haja. Pamoja na pombe zingine zilizofutwa katika ile hali ya kawaida ambayo ilionekana si nzuri kwa matumizi ya Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, hali hii ambayo tusipoidhibiti katika uanzishwaji wa viwanda hivi na tusipoboresha mfumo wa Mamlaka ya Chakula na Dawa nchini, tutakuta tumeanzisha viwanda vingi lakini bidhaa ambayo inazalishwa itakuwa ni bidhaa ambayo pia Watanzania watakuwa wametumia katika hali ambayo si sahihi. Hivi sasa si kweli, hata tuliotumia simu na wale Watanzania wote na waliotumia viroba na pombe mbalimbali na madawa lazima wamedhurika. Si rahisi kwa mara moja tukatambua madhara yake ni kwa kiasi gani, lakini ni vizuri tutakatazama upya mifumo yetu, tukafanya vizuri na tukaweza kuona viwanda vyetu vya ndani vinahimili mashindano au ushindani wa bidhaa kutokana na ubora unaotakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi bila viwanda haitawezekana, lakini kuwa na viwanda bila kuwa na watu wenye taaluma ni kazi moja ngumu pia. Nitoe rai kwa Serikali, tuweze kupitia vyuo vyetu vya VETA, vyuo vya ufundi stadi kuandaa watumishi wa kada za kati na kada za chini ili waweze kupata nafasi za ajira na waweze kunufaika kama watumishi katika viwanda ambavyo tunatarajia kuanzisha. Bila kuwa na Watanzania hawa wenye taaluma ya chini na ya kati, basi viwanda tutakavyoanzisha vitakuwa vinamilikiwa na watu wa nje na pia tutakuwa tunatafuta watumishi wa kada za chini kutoka nchi zingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, niweze kusema tu kwamba, kwa ujumla usimamizi wa kodi haujakaa vizuri kwenye viwanda ingawa suala hili ni la Wizara ya Fedha. Viwanda vyetu vingeweza kuzalisha bidhaa nzuri zenye kuhimili ushindani zikaingia kwenye mfumo na mfumo wa ukusanyaji wa kodi ukatazamwa, basi Tanzania ingeweza kuwa nchi ya mfano katika kukusanya na nchi ya mfano katika kuelekea uchumi kupitia viwanda ambavyo tutaanzisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pengine utafiti ufanyike ili tujue ni maeneo gani yanakuwa na malighafi na maeneo gani yanaweza kuwa na fursa za uanzishwaji wa viwanda kutokana na rasilimali zitakazokuwepo katika maeneo hayo, pia katika yale maeneo ambayo kwa namna moja au nyingine tunaweza tukawa tumepata mwingiliano wa kiuchumi kwa maana ya yule anayezalisha, yule mwenye malighafi na yule mwenye kutokewa na fursa hii ya kupatikana kwa kiwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii pia kusema kwamba, Watanzania si kwamba hawapendi mali inayozalishwa Tanzania, ni pale baada ya mtumizi anapoona mali au bidhaa iliyotoka nje ina thamani kubwa kuliko ile iliyoko nchini. Kwa vyovyote, lazima yule ambaye ananunua au mlaji au mtumiaji atakuwa na taswira nyingine tofauti ya kuona kwamba pengine ile ya nje ni bora zaidi kumbe hata sisi tuna bidhaa bora na nzuri zaidi, tatizo ni pale tu tunaposhindwa kudhibiti ubora unaotakiwa katika hali ya uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tutazame pia wakati huu tunafufua viwanda, je, ni kwa kiasi gani tumefanya utafiti kwa nini viwanda hivi awali vilipotea au vilishindikana kuendeshwa au vilipata kukwama na hatimaye kushindwa kujiendesha? Kwa vyovyote vile bila utafiti, bila mapitio tunaweza tukaanzisha na mbele ya safari kukaja tena wimbi lingine la viwanda hivi kupotea na hatimaye nchi yetu kupiga mark time au kutokuwa na hatua ambayo si nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pengine kwa namna moja au nyingine naweza nikazungumza jambo lisiwafurahishe Watanzania. Tukiwa watu wa kuamini mambo mepesi, yasiyo na tija, ambayo hatuyafanyii utafiti, mambo ambayo rasilimali wataalam hawatumiki kama sehemu ya Watanzania waliopata fursa ya kupata taaluma hiyo, basi kwa vyovyote vile si rahisi tukawa na viwanda ambavyo ni endelevu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kumpongeza kwanza Mheshimiwa Rais na vilevile kuwapongeza Wizara kwa jinsi wanavyohangaika. Pia tunaomba sekta hii muhimu sana itakayoajiri Watanzania wengi, ipate fedha katika Bajeti ya Mwaka huu kwa asilimia 100 ili fursa hii ya viwanda kupanda na kupata nafasi nzuri, iweze kuwafikia Watanzania na Watanzania waweze kunufaika na fursa hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunapitisha bajeti, mwakani tunatarajia kuona kwamba angalau kile tulichopitisha kuna asilimia pengine 100 au 80 kwenda mbele ipelekwe kwenye malengo mahsusi yaliyoanzishwa au yanayoanzisha viwanda ili tuweze kusonga mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, lakini nikitegemea yale yote yaliyokusudiwa yanapata fursa ya kutengewa fedha na kufanikiwa. Ahsanteni sana.