Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii na mimi niweze kuchangia bajeti ya Serikali. Kwanza kabisa nianze kusema ninaunga mkono hoja kwa asilimia mia moja na ninaunga mkono hoja kwa sababu bajeti hii imeitendea haki sekta ya elimu, na bajeti hii inalenga katika kuondoa kero ambazo zimekuwa zikiwasumbua Watanzania kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, naomba nipongeze hatua ya Serikali ya kuanzisha mfumo wa ukusanyaji wa mapato (e- government payment gateway) ambayo kwa kweli inalenga kuondoa upotevu wa mapato ambao unasababisha Serikali isiweze kuwahudumia wananchi wake ipasavyo. Vilevile napongeza kodi ambazo zimeondolea katika sekta ya elimu katika katarasi za kujibia maswali, lakini vilevile napongeza hatua ya kuondoa kodi kwa ajili ya vifaa vya wanafunzi wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizo, sasa naomba nijikite katika kujibu hoja ambazo zilihusu sekta ya elimu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa kumekuwa na hoja ambayo imejitokeza kuhusu namna ambavyo Serikali imejipanga katika kuhakikisha kwamba inatatua kero za wanafunzi wenye mahitaji maalum.

Mheshimiwa Spika, nilihakikishie tena Bunge lako Tukufu kwamba utatuaji wa kero za wanafunzi wenye mahitaji maalum ni kipaumbele namba moja cha Serikali ya Awamu ya Tano, na tayari hatua za kutatua matatizo hayo zimekwisha chukuliwa.

Mheshimiwa Spika, katika bajeti iliyopita tulinunua vifaa ambavyo vimesambazwa katika shule na Waheshimiwa Wabunge wanaweza wakaangalia katika kitabu changu cha bajeti kielelezo namba 8 hadi10 kimeonyesha mgao wa vifaa vilivyonunua na kwa Waheshimiwa Wabunge ambao hamkuapa katika awamu hii ni wahakikishie kwamba katika bajeti hii ambayo leo tunaipigia kura zimetengwa fedha kwa ajili yakuhakikisha kwamba ile mikoa na shule ambazo hazijapata zitapatiwa vifaa.

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala la Ukaguzi. Limezungumziwa hapa suala la kuboresha ukaguzi ili kuwa na ufanisi zaidi. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali inatambua kwamba Idara ya Udhibiti Ubora ndiyo jicho la Serikali katika sekta ya elimu; kwa hiyo kwa namna yoyote ile Serikali itahakikisha kwamba inaboresha. Hatua ambazo tumezichukua ni pamoja na kuhakikisha kwamba tunanunua vitendea kazi, tunafahamu kwamba mazingira ya Wadhibiti Ubora hayakuwa mazuri. Katika bajeti ya sekta ya elimu tumetenga fedha kwa ajili ya kujenga ofisi 50 pamoja na kununua vitendea kazi.

Mheshimiwa Spika, vifaa peke yake haviwezi kuleta ufanisi inatakiwa pia na watu ambao ni mahiri katika kufanya kazi. Mfumo mzima wa Ukaguzi katika sekta ya elimu tutaungalia kwa kuhakikisha kwamba tunakuwa na ufanisi zaidi. Kwa sababu mfumo wa sasa ambapo Mkaguzi wa Shule za Msingi hawezi kukagua shule za sekondari umepitwa na wakati kwa sababu kila ilipo shule ya msingi jirani yake kuna shule ya sekondari. Kwa hiyo, tunaangalia mfumo mzima na tumetengeza kihunzi cha ukaguzi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunakuwa na mfumo ambao ni fanisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambayo imezungumziwa katika sekta ya elimu ilikuwa inahusiana na mazingira ya miundombinu katika sekta ya elimu. Nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba Serikali ya awamu ya tano imeweka dhamira ya dhati na katika bajeti hii tumeweka mikakati ya kuhakikisha kwamba tunaendelea kuboresha mazingira katika sekta ya elimu kuanzia vyuo vya ualimu pamoja na vyuo vyetu vikuu. Kama tulivyofanya katika kujenga mabweni katika Chuo Kikuu cha Dar es salaam tutaendelea na katika taasisi zetu nyingine za elimu ya juu ili kuhakikisha kwamba vijana wa Kitanzania wanapata elimu yao katika mazingira ambayo ni mazingira tulivu na ni rafiki katika kujifunza.

Mheshimiwa Spika, vile vile kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa tutaendelea kuimarisha mazingira katika sekta ya elimu. Niwatoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge wanaozungumzia mazingira ya wanafunzi wenye mahitaji maalum kwamba tuna mpango wa kujenga shule maalum ya kisasa katika Chuo chetu cha Walimu cha Patandi kwa ajili ya wanafunzi wenye mahitaji maalum ili chuo kiwe karibu na mahali ambapo mafunzo ya walimu yanatolewa kwa lengo la kuhakikisha kwamba mafunzo ya walimu ambao wanahudumia wanafunzi wenye mahitaji maalum yatolewa kwa vitendo.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo limeongelewa ni suala la kuimarisha mafunzo ya ufundi stadi. Niseme kwamba jirani yangu hapa Mwijage ambaye anajenga viwanda hawezi akafanikiwa kama sijampa raslimaliwatu ya kutosha. Wizara yangu inalitambua hilo na tumeweka mikakati madhubuti ya kuhakikisha kamba tunakwenda sambamba na dhamira ya Serikali ya kujenga uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Spika, hivi tunavyo ongea Chuo cha Ufundi Arusha kimesha andaa kozi mahususi kuhakikisha kwamba Watanzania wananufaika na fursa ya kujenga bomba la mafuta ambazo nchi yetu imepata katika mazingira ya ushindani mkali. Kwa hiyo, tunaanda kozi ya kuwezesha vijana wetu kuwamahiri katika ujenzi wa bomba na vilevile katika nyanja nyingine zozote ambazo zinahusiana na viwanda vinavyoanzishwa. Tunafanya kazi kwa karibu na Wizara ya Viwanda na Biashara wanatupatia mahitaji na Wizara yangu hatulali tunahakikisha kwamba tunaweka mazingira fanisi ya kuweza kuhakikisha kwamba tunatoa mafunzo yanayoendana mahitaji.

Mheshimiwa Spika, suala la ujenzi wa VETA katika wilaya na katika maeneo yetu limekuwa likuzungumzwa, sana na niseme kwamba zile VETA ambazo zilikuwa zijengwe kwa ufadhili wa ADB tangu mwaka 2015 kulikuwa na changamoto ambazo Wizara yangu ilikuwa inapatia uvumbuzi na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba zile VETA zote ambazo ziko katika mchakato wa kujengwa tutahakikisha kwamba katika mwaka huu wa fedha 2017/2018 tunazikamilisha ili tuweze kupata fursa ya kuweza kujenga maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, kwa uchache hayo ndiyo ambayo yalizungumziwa katika sekta ya elimu. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja kama nilivyosema ni bajeti nzuri ni bajeti ambayo inaenda kuondoa kero katika sekta ya elimu lakini pia ni bajeti ambayo itawezesha kuimarisha mifumo ya elimu. Nakushukuru.