Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ili nitoe mchango wangu katika Wizara hii ya Elimu kwa umuhimu wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya na uzima kufika siku ya leo. Vilevile nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kupunguza changamoto za madawati nchini na kutoa elimu bila malipo ya ada toka shule ya chekechea mpaka shule za upili kidato cha nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa baada ya utangulizi huu nianze kutoa mchango wangu na ushauri kwa Serikali. Halmashauri ya Morogoro ina ukubwa zaidi ya kilometa za mraba 11,700 na umbali zaidi ya kilometa 180 toka Morogoro Mjini na shule ya kwanza ya sekondari ilijengwa mwaka 2000 na nyingine wakati wa ujenzi wa shule ya kata mwaka 2006 lakini hatuna shule ya fani hata moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Halmashauri ya Morogoro ina changamoto nyingi hasa ya miundombinu na uwezo mdogo wa mapato. Ili kukabiliana na changamoto hizo naiomba Serikali Kuu itusaidie katika ujenzi wa shule ya kidato cha tano na sita katika shule ya kata ya Mkuyuni, Ngerengere ama Nelson Mandela ambazo ni makao makuu ya tarafa za Mkuyuni, Ngerengere na Mikese kama zilivyofuatana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kudhibiti utoro na mimba za utotoni; kutokana na takwimu za BEST 2016 za utafiti wa kufahamu sababu mbalimbali za wanafunzi wa shule za msingi na sekondari kuacha shule mwaka 2015 ni vifo, mimba na utoro. Kutokana na takwimu hizo, mchanganuo wake ni kama ufuatao:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujauzito ni 3,637; utoro, 139,866 na vifo ni 3,917. Kutokana na takwimu hizo, utoro ni chanzo kikubwa cha watoto kuacha shule, ni zaidi ya 94% kuliko hata ujauzito. Katika hawa wapo watoto wa kiume na wa kike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa Serikali ni kuja na mkakati maalum kama ule wa ujenzi wa shule za kata na wa utengenezaji madawati nchi nzima, kumaliza ujenzi wa mabweni katika shule zote za kata ndani ya miaka miwili ili kukabiliana na tatizo la utoro na mimba za utotoni; kwa watoto kuishi shuleni chini ya uangalizi wa walimu na waangalizi wao wawapo mashuleni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali itoe mwongozo shule zote za kata kujenga mabweni katika shule za kata kwa kutenga fedha katika bajeti zao na kushirikiana na wadau wa maendeleo na wananchi wa sehemu husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Halmashauri wapewe mwongozo na kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa mabweni katika kusaidiana na wadau kumaliza tatizo hili la utoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho nataka kutoa ushauri pia katika ujenzi wa maktaba katika kila Wilaya na Tarafa nchini ili kukabiliana na changamoto ya kushuka kwa ubora wa elimu yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Afrika ikiwemo Tanzania, tuna tatizo kubwa kama Bara na kama nchi kwamba watu wengi hawapendi kusoma na kujifunza ili kupata uelewa na maarifa mbalimbali kutakakowezesha watoto kufanya vyema katika mitihani na pia mtu wa kawaida kupata uelewa wa kukabiliana na mambo ya kidunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka wenzetu wa mataifa ya nje wanatuambia ukitaka kumficha kitu Mwafrika weka vitu katika maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata vijana na wanafunzi wengi wanasoma kwa ajili ya kufaulu mitihani na siyo kupata uelewa na ufahamu wa somo ama kwa kutopenda kusoma au kukosekana kwa miundombinu ya kujisomea na hata shule zetu zinakosa kuwapa mazoezi na mitihani ya mara kwa mara wanafunzi kwa kukosa miundombinu ya vifaa vya kuandalia mitihani hiyo mingi kwa mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ili kuinua elimu yetu na kujenga utamaduni kwa watoto kupenda kujisomea tangu wakiwa wadogo. Kwa kuzingatia uwezo mdogo wa Serikali wa kujenga maktaba katika kila kata; na kwa kuwa hakuna vitendea kazi vya kuandaa mitihani ya majaribio katika shule nyingi za umma; hivyo basi, naishauri Serikali yangu kuja na mkakati wa kujenga maktaba katika kila Wilaya na Tarafa ili zitumike kwa kujisomea. Hii itawasaidia watoto wa shule za msingi na sekondari katika tarafa husika na jamii husika, pamoja kutumia majengo hayo kama kituo cha elimu, mafunzo na miundombinu ya kuandaa mitihani, kuichapisha na kupeleka katika shule ya eneo lake kutokana na mahitaji ya shule husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiweza kujenga maktaba na vituo vya elimu kwa jamii katika kila makao makuu ya tarafa, itasaidia sana kujenga utamaduni wa kujisomea kwa watoto wetu na jamii kwa ujumla, pia kupunguza gharama za kuandaa mitihani ya majaribio na ushindani kati ya shule kwa shule, kata kwa kata na tarafa kwa tarafa ili kuongeza uelewa na uwezo wa vijana wetu kuelewa masomo yao na kujiandaa vyema kushinda na kufaulu mitihani yao katika shule za umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante.