Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Halima Ali Mohammed

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. HALIMA ALI MOHAMMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 37, aya ya 65 inazungumzia kuhusu Bodi ya Mikopo kwa Wanafunzi wa Elimu ya Juu. Ninaishauri Serikali kwanza, iongoze bajeti ya Wizara hii ya Elimu ili wanafunzi wengi waweze kunufaika na mikopo hiyo na pili, kwa kuwa takwimu zinaonesha ufaulu wa wasichana katika elimu ya juu ni mdogo ukilinganisha na wavulana, basi naishauri Serikali hawa wasichana waliojitahidi kufanikiwa wapewe mikopo kwa asilimia 100 ili iwe ni motisha kwa wengine wajitahidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu madeni ya walimu, elimu ni walimu, chonga mzinga ule asali. Walimu wasikilizwe vilio vyao ikiwepo mishahara, kupandishwa madaraja pamoja na posho za wale wanaofanya kazi katika mazingira magumu. Jambo hili ni kero ya muda mrefu na linapunguza ari ya kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la shule za bweni, uzoefu unaonesha wanafunzi wa shule za bweni ni dhahiri wanakuwa na mazingira rafiki ya kuwawezesha watoto wetu kutumia muda mwingi kujisomea kuliko wale wa day ambao huondoka nyumbani alfajiri na kurejea usiku. Jambo hili si tu linawasababishia uchovu na kushindwa kujisomea, lakini pia kwa wasichana usalama wao ni mdogo wanapokuwa njiani. Naiomba Serikali iwaangalie wasichana wetu kwa jicho la karibu kwa kuwajengea shule za bweni za kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu miundombinu ya shule zetu; miundombinu ya shule zetu nyingi si rafiki kwa wasichana wetu kuhusiana na matundu ya vyoo ambavyo vitakuwa havina maji ya uhakika, haviwezi kuwa ni msaada kwa watoto wa kike wakati wa hedhi zao. Nusu ya watoto wa kike waliopo shuleni wanakabiliwa na changamoto ya kupata maambukizi ya UTI. Magonjwa haya ni hatari kwani yana tabia ya kujirejea lakini pia kupata magonjwa ya figo ambayo ni hatari zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali ifanye utafiti kuhusiana na magonjwa ya UTI. Halmashauri zijiwekee malengo mahsusi ya kujenga matundu ya vyoo na maji ya uhakika. Shule zisipewe vibali vya kufunguliwa kwanza bila ya kuwepo mfumo mzuri wa maji ya uhakika, viongozi husika wakishindwa kulisimamia hilo, basi wawajibishwe kwa mujibu wa kanuni zilizowekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iangalie uwezekano wa uwepo wa nesi mwanamke katika shule za msingi angalau mara mbili kwa wiki ili wasichana wawe na fursa ya kupeleka malalamiko yao yanayohusu afya zao, lakini pia wapate ushauri unaohusu mabadiliko ya maumbile yao na nini wafanye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu malezi; wazazi tuna wajibu wa kwanza wa kulea watoto wetu kimaadili kabla ya muda wa kwenda shule. Kambale mkunje angali mbichi, ukichelea mwana kulia mwisho utalia mwenyewe, inawezekana, timiza wajibu wako kwa faida ya Taifa. Ahsante.