Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 4, mwezi wa Tano, mwaka huu, 2017, nilisimama mbele ya Bunge lako hili Tukufu, nikitoa pole kwa familia ya ndugu Chanjale aliyepigwa risasi kule Ikwiriri Kata ya Umwe, na leo nimesimama kwenye Bunge hili Tukufu nikitoa pole kwa familia ya mmoja wa Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM aliyepigwa risasi zaidi ya nane jana, Ndugu Alife Mtulia ambaye ni Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Chama cha Mapinduzi kutoka Rufiji pia ni mkazi wa Jimbo la Kibiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matukio haya yanayoendelea katika eneo letu la Pwani yanadhamiria kutukwamisha kushiriki katika shughuli mbalimbali za maendeleo nami nataka niendelee kuwasihi wananchi wa Rufiji, Mkuranga na wakazi wa Kibiti kuendelea kuchapa kazi na kuendelea kuwa na imani na Serikali yao ya Chama cha Mapinduzi. Hapa nataka niwakumbushe tu kwamba hakika Mwenyezi Mungu amekadiria maisha ya kila mwanadamu, na tunaamini kabisa kwamba mwanadamu anapozaliwa miezi mitatu tu akiwa tumboni mwa mama yake tayari Mwenyezi Mungu anakuwa ameshamuandikia mambo yake yote katika dunia. Qurani inasema Kulla maagh yuswibana inna maagh katana llaahu lanah ikimaanisha kwamba hakika Mwenyezi Mungu ameshamkadiria mambo yake kila mwanadamu aliyezaliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Elimu, kwanza kabisa wananchi wa Rufiji tunatambua sana umuhimu wa elimu na umuhimu wa elimu hii kwa sisi wenye imani ya kiislamu tunatambua kwamba wahyi wa kwanza kabisa Mtume wetu Muhammad kuupokea ilikuwa inahusu elimu. Katika Sura ile ya Iqra ambayo Mtume wetu alikabidhiwa na akiambiwa asome, niseme mbele ya Bunge lako hili Tukufu kwamba umuhimu wa elimu umesikilizwa katika kila sehemu na wananchi wa Rufiji wamepata bahati kubwa ya kupata Mbunge ambaye ni msomi na ana uwezo wa kusaidia kuwapambania katika jambo hili la elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kupongeza sana Serikali, nimpongeze sana Waziri wa Elimu. Kwanza kabisa Waziri wa Elimu alivunja historia na rekodi kwa kufika Rufiji kwa mwaliko wa Mbunge, alifika Rufiji akajionea hali ya miundombinu ya shule zetu za Rufiji, wananchi wa Rufiji wamenituma nikuambie wanakupongeza sana na uchape kazi sana. Wako nyuma yako, lakini kwa namna ya kipekee kabisa wanakushukuru sana kwa kutoa shilingi milioni 259 kwa ajili ya ukarabati wa shule ya sekondari ya Utete. Wananchi wa Rufiji pia wanakupongeza Mheshimiwa Waziri kwa kukubali ombi la Mbunge la kutoa kibali cha shule ya sekondari Umwe ambacho kilikaa kwa zaidi ya miaka kumi kutosajiliwa. Wananchi wote wa Ikwiriri wanakupongeza sana na wanakukubali kweli, tunakuombea afya njema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi hawa wamenituma, wameniambia kwamba walikupa maombi ya kukarabati shule yetu ya sekondari ya Muhoro pamoja na shule ya sekondari ya Ikwiriri. Hali ya miundombinu ya shule zetu umejionea Mheshimiwa Waziri, tunakuomba sasa utusaidie. Kwa sababu katika Mkoa wa Pwani, Rufiji umeweza kutupatia shilingi milioni 259 tu, tunakupongeza. Wananchi wa Kibiti pia kupitia kwa Mbunge wao, Mheshimiwa Ally Seif Ungando, wameniambia pia nikuambie wanakupongeza sana kwa kutoa kiasi cha shilingi 1,700,000,000 kwa kukarabati shule ya sekondari Kibiti, wanaomba pia uwasaidie kukarabati shule ya sekondari Zimbwini, shule ya sekondari Bungu, shule ya sekondari Mlanzi pamoja na shule ya sekondari Nyamisati ambayo umetoa shilingi milioni 260 pamoja na shukrani kwa kutoa shilingi milioni 253 kwa kukarabati shule ya sekondari Mtanga kule Delta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Rufiji umetoa kwa shule moja, nikuombe sasa utusaidie wananchi wa Rufiji, wapo wengi hapa wanaomba wapatiwe viatu kwa kuwa wana miguu, binafsi miguu sina.

Kwa hiyo, nikuombe lile tamko lililowahi kutolewa na Mheshimiwa Rais wetu wa Awamu ya Kwanza la miaka ya 1970 la kuboresha elimu katika maeneo ya watu ambao walikuwa hawajasoma sana, leo hii tumejionea Maprofesa hapa kama Mheshimiwa Profesa Palamagamba Kabudi, ni miongoni mwa watu waliosoma wakati ule ambapo waliweza kusaidiwa na Mwalimu Nyerere na wakapata elimu kwa kuwa maeneo yao hayakuwa na mwamko wa elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakuomba watu wa Rufiji sasa utusaidie, utuletee mwamko wa elimu kwa kuboresha miundombinu ya shule zetu na wananchi wanaamini kabisa kwamba maombi yao haya utayachukua, utayapokea na kuyafanyia kazi. Pia kwa namna ya kipekee wanaomba utusaidie kwa kupitia Mfuko wa Elimu utuboreshee shule yetu ya msingi Umwe, shule ya msingi Mgomba, shule ya msingi Muhoro, shule ya msingi Ngarambe, na ninamuomba Waziri wa TAMISEMI pia alichukue hilo na aone umuhimu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunaboresha suala zima la elimu katika maeneo yetu ya Mkoa wa Pwani, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, kwa namna ya kipekee kabisa, tuwaangalie wananchi wa Pwani; kama ambavyo alifanya Mwalimu Nyerere, haitakuwa dhambi kufanya ili kuwapa manufaa wananchi wa Mkoa wa Pwani ambao kwa kweli wameathirika kwa hali na mali kutokana na tatizo la kukosa elimu. Nikuombe wakati Mheshimiwa Waziri unahitimisha hapa utusaidie suala zima la mikopo, Bodi ya Mikopo iweze kuwaangalia wananchi wa Rufiji, watu wa Mkuranga, watu wa Kibiti na watu wa Kisarawe ambao wamekosa elimu, wakati wa mgao huu wa Bodi ya Mikopo basi waweze kufikiriwa kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Rufiji wamenituma, wameniambia kwamba wanacho Chuo cha Maendeleo pale Ikwiriri (FDC), ulifika mwenyewe ukajionea, wanaomba chuo kile sasa kiwe ni Chuo cha VETA kwa sababu kutoka Rufiji kwenda Kibaha kufuata elimu hii ya VETA ni mbali sana kwa zaidi ya saa sita. Wanaomba sasa Chuo hiki cha FDC uje utuambie mtakiboresha ili kiwe ni Chuo cha VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mnaboresha elimu kwa watoto wetu, tunaomba muangalie, yapo maeneo Rufiji ambapo hakuna shule, ni umbali mrefu, kwa mfano kule Mtanange kijijini kwangu wapo watoto zaidi ya 500 ambao hawasomi kabisa, lakini yapo maeneo Kata ya Mgomba kule Mupi, wapo watoto wengi ambao hawasomi kabisa. Tukuombe Mheshimiwa Waziri tuletee wataalam wako waweze kuangalia ni namna gani wataboresha elimu. Ninaamini kabisa iwapo tutaboresha elimu tatizo hili ambalo linaendelea leo hii halitakuwepo tena kwa sababu tutakuwa na wasomi wengi eneo letu la Rufiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, zipo shule ambazo tunahitaji kukarabati, tunakuomba kupitia Mfuko wa Elimu utusaidie. Kwa mfano, ipo shule ya msingi Mchengerwa iliyopo kule Miangalaya ambayo nimeanza ujenzi wa darasa moja lakini pia tunayo shule ya msingi Kilindi ambayo imetoa madaktari wengi lakini shule hii ni shule ya miti tu na watoto wetu wanapata taabu sana inaponyesha mvua na wakati mwingine jua linapokuwa kali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona Waheshimiwa Wabunge wengi hapa wakizungumzia suala zima la kuwaruhusu watoto wetu waliopata ujauzito kuendelea na masomo. Mimi ninaomba niwakumbushe sana Waheshimiwa Wabunge kwamba suala hili iwapo wataendelea kulisogeza mbele sana wakumbuke wanavunja Ibara ya Tano ya Katiba kwa kutaka kuwaruhusu watoto wetu kushiriki kwenye shughuli za ngono.

Mimi ni muislamu, nilisema hapa, nitashangaa sana kuona Wabunge waislamu wakishabikia suala hili na kutaka watoto wetu washiriki kwenye shughuli za ngono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Qurani inatuambia nilisema hapa, nataka nirudie inasema kwamba wallah takrabu zinah inah kanah taishatan wasahalan sabilah. Waislamu tumezuiwa kabisa, na jambo hili iwapo tutaendelea kuwasaidia watoto ambao wamepata ujauzito waendelee na masomo ni sawana kwenda kuongeza mafuta katika moto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwakumbushe, wakati ule ambapo Wazungu wanaondoa biashara ya utumwa, miaka ile ya 1800 ....

TAARIFA...

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa aliyoitoa ni sahihi, suala hili syo la udini lakini nataka niseme tu kwamba suala hili ni muhimu sana kwa Watanzania wakalitambua ni vema Watanzania sasa wakalea watoto wao kwa misingi ya elimu ya dunia na elimu ya ahera, ndiyo maana nikasisitiza hapa kwamba kuliweka jambo hili ni kusisitiza na kuwataka watoto wetu washiriki katika mambo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 2 Februari, 1835, Lord Maclay, mmoja wa Wabunge mashuhuri kule Uingereza aliwahi kusema kwamba Afrika hatuwezi kuitawala mpaka pale ambapo tutaweza kudhibiti elimu yao na kuhakikisha kwamba wanafanya mambo kutokana na tunayotaka kuyafanya. Ninaamini, nimeona Wazungu wakiwepo katika Bunge lako hili Tukufu na ninaamini… (Makofi)

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila mpangilio)

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: …ninaamini suala hili wapo watu wana-engineer ambao wanalitaka jambo hili. Mheshimiwa Lord Maclay alisema maneno haya, naomba niwanukuu kwa kiingereza:

“I have travelled across the length and breadth of Africa and I have not seen one person who is a beggar, who is a thief such wealth I have seen in this country, such high moral values, people of such caliber, that I do not think we would ever conquer this country, unless we break the very backbone of this nation, which is her spiritual and cultural heritage and therefore, I propose that we replace her old and ancient education system, her culture, for if the Africans think that all that is foreign and English is good and greater than their own, they will lose their self esteem, their native culture and they will become what we want them, a truly dominated nation”

Mheshimiwa Mwenyekiti, maneno haya siyo ya kwangu ni maneno yaliyowahi kutolewa tarehe 2 Februari,1835. Ninaomba niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge iwapo wanasisitiza jambo hili wakumbuke Bunge lililopita tulifanya marekebisho ya sheria hapa, Sheria Na. 253. Kwa mujibu wa marekebisho haya ya Sheria Na. 353, kifungu cha 61 ambacho kilitoa mamlaka kwa Serikali kuhakikisha kwamba watoto wote wanaoshiriki katika masuala ya uasherati pamoja na ngono wadhibitiwe. Kuliruhusu jambo hili ina maana kwamba tunakinzana na kifungu hiki cha Sheria Na. 61 ambayo Bunge hili lilitunga kifungu hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa wa Sheria ya Elimu, kifungu cha 60(b) ambacho kimetoa mamlaka…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.