Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Othman Omar Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Gando

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. OTHMAN OMAR HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi hii ya kuchangia katika Wizara hii ya Elimu. Pia napenda nifikishe salamu kwa Mheshimiwa Waziri kutoka kwa Mkuu wa Idara ya Fizikia pale Dar es Salaam kwamba aende akawatembelee. Kuna maabara yao imechoka, vifaa vyao vimechoka, kwa hivyo aende wakashauriane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nieleze tu kwamba mimi ni Mwalimu, nafundisha masomo ya sayansi na hisabati. Nakumbuka katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu alizungumzia kuhusu tatizo la masomo ya sayansi katika nchi yetu. Akasema kwamba uchumi wa viwanda unategemea kwa kiasi kikubwa rasilimali ya watu wenye ueledi wa masomo ya sayansi na hisabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile akasema kwamba changamoto tuliyonayo hapa Tanzania mpaka sasa hivi ni vijana wetu kutopenda kusoma masomo ya sayansi na hisabati. Akienda mbali zaidi Mheshimiwa Waziri Mkuu kusema kwamba changamoto tuliyonayo ikiwa wanafunzi na vijana wetu hawatajitahidi iko hatari ya viwanda vyetu kuja kuwategemea wataalam kutoka nje na hivyo Watanzania kubakia watazamaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa napitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri nilifikiria angalau angetoa mwelekeo au kujibu hii hotuba ya Waziri Mkuu, jinsi gani anajipanga kwenda kutoa suluhisho la matatizo ya masomo ya sayansi lakini naona hotuba iko kimya. Kama Waziri mwenye dhamana wa Wizara hii tunapenda awaeleze Watanzania changamoto hii ya vijana wetu kutopenda kusoma masomo ya sayansi anakwenda kuitatua vipi? Ukitilia maanani wajibu wa Wizara yake ni kuainisha mahitaji ya nchi katika ujuzi na mahitaji tuliyonayo ya nchi sasa hivi ni vijana waliosoma masomo ya sayansi na hisabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wajibu wa pili ni kuimarisha matumizi ya sayansi na hisabati. Tatu ni kuendeleza wataalam wa ndani wa sayansi na hisabati. Haya ni majukumu ya Wizara ambayo yameandikwa katika kitabu hichi lakini mpaka sasa hivi pamoja na changamoto hizo sijaona vipi anakwenda kulitatua tatizo hili la wanafunzi ambao hawapendi kusoma masomo ya sayansi na hisabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimjulishe Mheshimiwa Waziri na Watanzania ni kweli usiopingika kwamba vijana wetu kusoma sayansi sasa hivi hawataki. Tatizo kubwa linalowasibu ni kwamba wale ambao wanajaribu kufuatilia masomo ya sayansi hawapendi kusoma hisabati. Huwezi ukaisoma sayansi ikiwa utaiacha hesabu, unaweza ukaisoma hesabu ukaiacha sayansi lakini huwezi ukasoma sayansi bila hisabati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusiwalaumu sana Walimu wetu wa sekondari, kwa sababu wanafunzi hawa japokuwa wakifika pale sekondari wanaanza kuchanganyikiwa, kwa sababu hawa wanafunzi wameanza kupoteza mwelekeo kutokana na primary waliyotoka walikuwa hawana msingi mzuri wa masomo ya hisabati. Kwa hiyo, msingi wa hisabati unajengwa pale ambapo wanafunzi wako primary wakifika sekondari ikiwa hawana msingi huo wa hesabu basi masomo haya ya sayansi watayasikia tu na ikiwa watayafuata yatawaangusha njiani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka nijielekeze kwenye dhima nzima ya Wizara ya Elimu. Waziri kasema katika kitabu chake hiki hapa kwamba, moja ya dhima ya Wizara yake ni kuinua ubora wa elimu na mafunzo, pia kuweka mifumo na taratibu zitakazowezesha kupata idadi kubwa ya Watanzania wenye kuelimika lakini pia wanaopenda kujielimisha zaidi ili waweze kuchangia katika maendeleo ya Taifa hili. Nataka kupata maelezo ya Mheshimiwa Waziri hapa kwa sababu kuna idadi kubwa ya Watanzania hasa walio katika sekondari wanapenda kujielimisha lakini taratibu zilizowekwa zinawarudisha nyuma kupata elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukulia mfano mimi mwenyewe mwaka 2009 nilipata nafasi ya kwenda kusoma Shahada ya Uzamili pale chuo kikuu na tulikuwa wanafunzi 11, kati ya hao wanafunzi saba walikuwa ni Tutorial Assistance kutoka vyuoni, mmoja alitoka Arusha. Hawa walikuwa wanapata mikopo kutoka elimu ya juu Mheshimiwa Waziri tulibakia wanafunzi wawili ambao tulitoka sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulijiuliza kwamba wenzetu wanatoka kwenye vyuo, sisi tunatoka sekondari sote tuna lengo moja la kulitumikia Taifa hili lakini wenzetu wanasoma pale vyuoni kwa raha kabisa. Tulibakia wanafunzi wawili ambao tumetoka sekondari hatuna msaada wa aina yoyote, kwa hiyo, tukabakia tunabangaizabangaiza mpaka tukamaliza chuo. Ukiangalia hii siyo haki kuona kwamba wanafunzi wote tuna lengo moja la kujenga Taifa hili wengine wakapewa msaada huu lakini wengine wakanyimwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo hilo lililotukuta lilitupelekea sisi wawili kusoma kwa shida kubwa sana mpaka ulipofika wakati wa kuandika dissertation ilibidi tutafute njia nyingine ya kukabiliana na maisha. Mimi nilitafuta school ya karibu pale iko Kawe ambapo viongozi wengi mnapeleka watoto wenu pale. Nataka nikupe siri kidogo ya ile shule ya private ambayo iko top ten katika kiwango cha Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilichokigundua kinachozingatiwa pale kwanza ni ubora wa Walimu. Maslahi ya Walimu yanazingatiwa, unapoingia pale unasomesha kwa raha kabisa, unaondoka nyumbani umeacha chakula unakuja pale huna tatizo la aina yoyote. Suala la pili ni idadi ya vipindi havizidi 20 kwa wiki, ni vipindi vinne kwa siku moja. Ina maana ukiwa unafundisha vipindi vinne kwa siku moja unapata wakati wa kutosha wa kumsaidia mwanafunzi, unapata wakati wa kutosha wa kusahihisha madaftari, unapata wakati wa kutosha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. OTHMAN OMAR HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.