Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Salma Rashid Kikwete

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mchinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu. Pia nitoe pongezi kwa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya katika kuboresha elimu. Pamoja na hayo, niwapongeze Walimu wenzangu wote nchini Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya katika sekta hii ya elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, niwapongeze Walimu wenzangu, wengi wao wameweza kujiendeleza katika maeneo tofauti kuanzia ngazi za chini, hadi kufikia eneo lingine la Masters na Ph.D, hongereni sana Walimu wenzangu popote pale mlipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia suala la elimu na tunazungumzia uboreshaji wa elimu. Tunasema kwamba tunataka tuboreshe; katika maboresho haya, ninachokizungumzia, Walimu hawa wanapojiendeleza ni vema kabisa baada ya kumaliza masomo yao, wasiombe nafasi za kwenda aidha Sekondari au kwenye Vyuo. Kwa sababu tuko kwenye maboresho, msingi wowote ni muhimu sana katika jambo lolote lile. Kwa hiyo, Walimu hawa ni vema wabaki kwenye zile shule kama ni wa Msingi wamejiendeleza wamepata Diploma au wamepata Degree wabaki pale, lakini kitu kikubwa ni vema kabisa Walimu hawa waboreshewe maslahi yao kulingana na elimu yao waliyokuwanayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuje kwenye eneo la Mafunzo ya Ualimu. Nimeona Walimu wengi wamepata fursa juu ya maeneo hayo, lakini sijaona mafunzo kwa eneo la Elimu ya Awali. Sera inatuambia kwamba kwenye kila Shule ya Msingi kuwe na darasa la elimu ya awali. Sasa kama tunataka tuboreshe, ni lazima tuanzie kuboresha kwenye Elimu ya Awali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la ithibati katika ukurasa wa 19 aya ya 37. Tumeambiwa kwamba kulikuwa na suala zima la ukaguzi, Walimu 7,727 walikaguliwa; Msingi 6,413, Sekondari 1,314. Ni vema kabisa, lakini lengo ilikuwa kukaguliwa Walimu 10,818. Hawa ni baadhi tu ya waliokaguliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tukija kwenye eneo hili, ili tuweze kuboresha elimu yetu hapa nchini Tanzania, hili eneo la ukaguzi ni lazima lipewe kipaumbele. Kuwe na pesa ya kutosha na kuwe na vitendea kazi. Ili kuboresha eneo hili, ni lazima Walimu wakaguliwe mara kwa mara. Unaweza ukakuta ndani ya miaka; nazungumza haya kwa sababu nina uzoefu juu ya eneo hili, mimi ni Mwalimu kwa taaluma. Unaweza ukakuta zaidi ya miaka miwili au mitatu Mwalimu hajakaguliwa. Sasa unategemea ubora wa elimu hapa utakujaje kama hakuna mtu wa kumsimamia huyu Mwalimu? Kwa hiyo, hili eneo ni lazima lipewe kipaumbele cha namna ya pekee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyazungumza haya, napenda nizungumzie eneo la Shule ya Lindi Sekondari. Nimeona maeneo mengi wameboreshewa, wameambiwa itaboreshwa hili, itatengenezwa Shule hii, itafanya hivi, lakini Sekondari ya Lindi ilipata tatizo la kuungua moto; na moto ulikuwa mkubwa na ulipoteza karibu madarasa yasiyopungua sita pamoja na eneo la Mikutano. Serikali hapa mnatuambiaje juu ya shule hii iliyoko Mkoa wa Lindi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumzie suala la mimba. Suala la mimba ni tatizo na suala la utoro ni tatizo. Sisi kama wanawake tunawapenda sana na ni lengo letu Waheshimiwa Wabunge wanawake kuwatetea watoto wa kike na mwanamke yeyote yule ambaye anaomba nafasi ya uongozi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala hili la mimba, hasa mimba za utotoni, sikubaliani na kwamba watoto wakipata mimba warudi tena shuleni. Hili sikubaliani nalo hata kidogo! Sababu za kutokukubaliana nazo ni hizi zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tunazungumzia suala la mila, desturi, utamaduni na mazingira…(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na dini. Hakuna dini yoyote inayomruhusu mtoto wa kike kupata mimba kabla ya wakati. Biblia inasema na Quran inasema. Tunapofanya mambo yetu ya msingi tuangalie vilevile mambo yanayohusu imani zetu za dini. Suala la mtoto kurudi shuleni, tutafute njia nyingine mbadala. Sisi kama Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tuna Kanuni zetu na ndizo tunazozifuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika kwenye suala la mimba, sheria inayofuata hapa mtoto akipata mimba asirudi shuleni. Kama hapa ingekuwa sisi kama Wabunge hatuna sheria na kanuni, ingekuwa tunafanya mambo kila mtu na jambo lake, lakini sheria zinatubana. Nataka kwa hilo sheria zibane. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka sheria ibane. Mtoto akipata ujazito asirudi shuleni, atafutiwe njia nyingine ya kuweza kumsaidia mtoto huyu.

TAARIFA...

MHE. SALMA R. KIKWETE: Nashukuru sana kwa kuniunga mkono. Naomba wanawake wote waniunge mkono na wanaume vilevile waniunge mkono. (Makofi)

MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hivi? Kama hivyo ambavyo sisi tunawatetea...

MHE. SALMA R. KIKWETE: Tuwatetee katika mazingira…

TAARIFA...

MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Taarifa hiyo siikubali, naikataa…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila mpangilio)

MHE. SALMA R. KIKWETE: …pamoja na kwamba kwamba watoto hawa wanapata mimba katika umri mdogo; lakini ni lazima tuwatengenezee mazingira wezeshi. Mazingira wezeshi tukisema warudi shuleni watoto hawa, ina maana wengi watapata mimba.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila mpangilio)

MHE. SALMA R. KIKWETE: Wengi watapata mimba katika umri mdogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante.