Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Natoa pole zangu kwa wote wale waliofiwa na watoto na familia ya Mzee Sozigwa, familia ya Mzee Mwambungu na wengine wote ambao wamepata maafa hivi karibuni, Mungu alaze pema roho zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwashukuru sana na kuwapongeza Wizara ya Elimu kwa hotuba nzuri, napongeza Kamati zote mbili kwa maoni yao mazuri waliyoyatoa kwa Serikali, nitashukuru na nitafurahi kuona kuwa Serikali imeyazingatia maoni yote yale ambayo yanafaa katika kuboresha huduma zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wengi wamezungumza mambo mengi na nisingependa kuyarudia. Napenda kuzungumzia suala zima la kumuendeleza mtoto anapokuwa mdogo. Wengi tumezungumzia elimu kwa maana ya shule za msingi, shule za sekondari, vyuo na vyuo vya ufundi, lakini nataka turudi katika msingi wa kumlea mtoto ili aje kuwa mwanafunzi mzuri, aje kuwa mfanyakazi mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesahau kabisa suala la kumlea mtoto, kumjengea mtoto uwezo wake tangu akiwa mdogo kwa maana ya shule za awali. Imeonesha kabisa katika tafiti mbalimbali kuwa mtoto akianza kujengewa uwezo mzuri kiafya kwa maana ya lishe, lakini vilevile kiakili kwa maana ya kumpeleka kuanza kuchezacheza shuleni na wenzake, kuanza kujifunza ku-interact na wenzake, kuanza kucheza michezo ambayo inamjenga ubongo, kumfundisha utundu wa kutumia ubongo wake, anakuja kuwa mwanafunzi mzuri anapoanza shule ya msingi mpaka kwenda sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nataka kupendekeza kuwa Serikali iwe na mkakati wa kuhakikisha kuwa nchi nzima shule za awali zinatiliwa mkazo kama ambavyo tunatilia mkazo masuala mengine ya afya na maji, vilevile mtoto aanze kujengwa akiwa mdogo. Huwezi kumtoa mtoto aliyekuwa anakaa nyumbani siku zote ukampeleka miaka saba kuanza shule kwa mara ya kwanza, atakuwa hajapata ule msingi wa kumuwezesha. Haya mambo ya pre-school siyo mchezo, ni sehemu ambayo inaanza kumjenga mtoto jinsi ya kuelewa vitu lakini kutafakari mambo na vilevile kuzoea ku-interact na watoto wa aina nyingine. Kwa hiyo, ningependa sana hili nalo litiliwe mkazo kama ambavyo tunatilia mkazo masuala mengine ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la elimu ya watu wazima; wakati sisi tunakua kulikuwa kuna elimu ya watu wazima na ilikuwa inagusa watu wazima kwa maana ya wazee au watu wazima ambao hawakupitia shule, lakini hata wale vijana ambao kwa bahati mbaya kwa mazingira fulani walishindwa kuendelea na masomo halafu waka- regress. Unajua ubongo zoezi lake ni kuutumia, kuusomea, kufanyia vitu ambavyo unau-challenge ubongo ndiyo hata ile elimu uliyokuwa umeipata inaendelea kuwepo. Unaweza ukajikuta ulisoma halafu hata kusoma gazeti ukakushindwa kwa sababu umekaa umebweteka hutumii ubongo, kwa hiyo, wale pia walikuwa wanapewa elimu. Sasa hii elimu ya watu wazima sijaiona vizuri hapa, nimesoma imenionesha tu kuwa kuna fedha na mkakati wa kujenga uwezo au kuboresha uwezo wa taasisi yenyewe. Sijaona wapi inaonesha kule chini kwa wananchi elimu ya watu wazima itaendeshwa vipi, ningependa hilo lionekane kwa sababu ni muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafika mahali ambapo sasa mzazi hajui kusoma chochote, hajui hesabu, atamsimamia vipi mtoto wake kuhakikisha kuwa anafanya kazi zake za shule? Kwa hiyo, inakuwa vigumu kwa mzazi hata kusimamia mtoto masomo kwa sababu yeye mwenyewe hajui na hajiamini kuwa anaweza akamsimamia mtoto. Kwa hiyo, hilo la elimu ya watu wazima naomba lizingatiwe na lipewe kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vifaa vya wanafunzi wanaoishi na ulemavu. Watoto wengi bado hawawezi kusoma vizuri kwa sababu wanaishi na ulemavu lakini shule hazitoshelezi kwa mahitaji ya vifaa vyao, vitabu vyao na mambo yote yanayowezesha watoto wanaoishi na ulemavu kusoma vizuri kama watoto wengine wote. Hili naomba nalo lizingatiwe, hasa sisi tunaokaa kwenye Wilaya za pembezoni, kwa kweli hili suala hatulioni kabisa. Kwa hiyo, ni kitu ambacho lazima kiwepo. Kuwachanganya watoto wakati wote siyo vibaya lakini wakati mwingine inabidi wawe segregated ili wapate kujifunza vizuri wenyewe kwa pace yao. Maana mtoto anayeishi na ulemavu wakati mwingine kwa sababu ya ule ulemavu wake ukimuweka na watoto wengine inaweza ikawa inam-challenge zaidi, kwa hiyo inategemea ni level gani unamchanganya na watoto wengine, lakini vifaa havitoshelezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu VETA sijui ni kigezo gani kinatumika kuweka VETA kwenye Wilaya zetu, Wilaya yangu ya Ileje nilifanya juhudi zangu binafsi nikapata mfadhili akanijengea VETA ambayo Serikali iliahidi kuwa itaichukua, lakini wakanipa masharti kuwa lazima ile ardhi iwe imepimwa na mambo mengine yote. Sasa kutokana na changamoto za kupima ardhi tunazozijua, mpaka leo huu ni mwaka wa pili, hatujaweza kupima ile ardhi na kwa hali hiyo VETA imesimama pale haifanyi kazi. Nataka kuwaomba, kama vile ambavyo tuliweza kuijenga bila kuwa tumepima, basi muichukue ianze kufanya kazi wakati taratibu za kupima zinafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusu vitabu; kama ambavyo tumekuwa tukiweka mkazo sana kwenye kujenga madarasa, tukajenga maabara, tukaanza kushughulikia miundombinu ya walimu na mafao yao; shule bila kuwa na vitabu vya kutosha nayo pia ni kazi bure. Imetubidi Wabunge tufanyekazi ya ziada kutafuta vitabu kwa ajili ya shule hasa vitabu vya sekondari, hii inakuwa ngumu. Vitabu ndiyo moja ya kitu ambacho ni ghali sana katika huduma za mwanafunzi. Sasa kuniambia kuwa mimi Mbunge au wazazi peke yao wakasimamie kutafuta vitabu, hasa kwa mfano vya sayansi, vya hesabu, vya lugha, inakuwa vigumu.

Kwa hiyo, naomba sana hili suala la vitabu nalo lizingatiwe, lipewe uzito ule ule tuliotoa kwa masuala ya madarasa, maabara na mambo mengine, kwa sababu bila vitabu pia kufundisha inakuwa vigumu, walimu wanapata shida sana kufundisha bila vitabu.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mabweni sijui hili nalo litashughulikiwa vipi. Wilaya yangu ya Ileje haina shule ya sekondari ya bweni ya watoto wa kike hata moja. Tunazungumzia miaka 42 tangu Wilaya ianzishwe. Tunajitahidi wenyewe sasa hivi kutafuta namna ya kuanzisha shule ya bweni ya wasichana lakini mnajua gharama za kujenga shule kwa kutegemea nguvu za wananchi labda na Mbunge wao. Tunaomba sana Wizara kama inaweza kutufikiria, watoto wa kike wengi wa Ileje wanapata mimba za utotoni na tatizo moja ni hilo kuwa wanakwenda mbali sana kusoma, wanakwenda Wilaya nyingine kwenda kusoma au wanasoma pale ndiyo wanapanga kwenye ma-gheto. Gheto za ya vijijini, imagine mjini ma-gheto yalivyo, vijijini ni mabaya namna gani. Hakuna umeme, hakuna maji, kwa hiyo wanajikuta wanasoma katika wakati mgumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika takwimu utakuta wasichana wa Ileje wanapata mimba za utotoni wengi, pengine hata Mkoa mzima wa Songwe sijui, lakini nazungumzia kule ambako nina uzoefu nako. Kwa hiyo, haya ni mambo ambayo tunahitaji sana Serikali myafanyie kazi, shule za wasichana za mabweni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi kuna suala zima la hayo Mabweni yenyewe. Mabweni yanajengwa lakini mengi hayajakamilika, mengine zile certificate contractors hawajalipwa, kwa hiyo, bado pamoja na kuwa kuna hostels chache zimejengwa lakini hazijaanza kutumika kikamilifu kwa sababu hazijkamilika na hiyo pengine ni ukosefu wa fedha au sielewi ni matatizo gani lakini kwa kweli haitusaidii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia suala zima la tafiti. Tumeona hapa fedha nyingi zinatolewa kwa ajili ya utafiti, tunajiuliza hizi tafiti huwa zinaishia wapi? Kwa sababu tukija kule kwenye Halmashauri zetu bado hatuoni mazao ya zile tafiti zikatusaidia katika kuboresha mazingira ya elimu na mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tungependa sana hizo tafiti, kwanza hata kule kule kwenye Wilaya zetu tupate hawa watu wanaokuja kufanya utafiti au watu wetu nao wachukuliwe kufanya hizo tafiti yaani wafadhiliwe kufanya hizo tafiti, vilevile matokeo ya utafiti yanapotokea basi yaletwe na kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumezungumzwa jambo la kufundisha watoto hapa masuala ya study za maisha. Nataka nitoe angalizo ndugu zangu, tuna miradi mingi ya Kimataifa inayoletwa kwenye nchi zetu ya kutufundishia watoto wetu masuala ya study za maisha. Naomba zichunguzwe kabla hazijaanza kupokelewa, watoto wetu wanafundishwa maadili ya ajabu, watoto wetu wanafundishwa...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.