Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie, pia namshukuru Mwenyezi Mungu na ninaendelea kuwapa pole wenzetu wa Lucky Vincent, shule ambayo ilipoteza wanafunzi, Mwenyezi Mungu azilaze mahali pema roho za marehemu. Amen.

Naendelea kuwashukuru wananchi wa Urambo kwa ushirikiano wa wanaonipa. Nichukue nafasi hii kuwapongeza Mheshimiwa Profesa Ndalichako na Mheshimiwa Injinia Stella Manyanya kwa kazi kubwa wanayoifanya. Wizara ya Elimu ni kazi kubwa na tumewaona jinsi ambavyo wanachakarika, ninawapa pongezi sana. Naomba tu yale tunayowapa myapokee ili yale mnayoyafanya yaendelee kuwa mazuri zaidi. Hongera, akina mama wanaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza Kamati ya Huduma za Jamii inayoongozwa na Mheshimiwa Peter Serukamba kwa kweli kwa taarifa yao ambayo inatusaidia wote tunaounga mkono suala la watoto wa shule wanaopata mimba warudi shuleni. Katika taarifa yao kwa ruhusa yako, ukurasa wa 29 unasema hivi; “Kamati inashauri Serikali kutoa tamko rasmi kwamba mwongozo huo unaoruhusu wanafunzi wa kike wanaopata mimba kurudi shuleni utangazwe, uanze kutumika ili wanafunzi wa kike ambao wamekuwa wakifukuzwa shule kutokana na kupata ujauzito kurudishwa shuleni ili kuendelea na masomo yao. Hii itasaidia Taifa liweze kunufaika na usomaji wa watoto wa kike.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, tuunge mkono kauli hii ya Kamati. Ninavyofahamu Kamati husika huwa inakaa pamoja na Wizara, kwa hiyo, naamini kabisa kumeshakuwa na mashauriano kati ya Wizara na Kamati kwa hiyo kilichobaki, tuiunge mkono Kamati ambayo inafanya kazi kwa niaba yetu. Tunategemea Waheshimiwa Mawaziri wakati wa kuhitimisha mtoe tamko kama mlivyoombwa na mlivyoshauriwa na Kamati husika, watoto wetu wa kike warudi shuleni baada ya kujifungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikwenda Kenya, tunapokwenda kwenye nchi nyingine tunajifunza. Unayachukua yale ambayo unaona kwako yatakufaa. Tulipozungumzia wenzetu mnafanyaje kuhusu watoto wa kike wanaopata mimba, walitushangaa, wakasema jamani kwao ni historia, walishaamua zamani, Watanzania na sisi tufanye hivyo kwa sababu ni jambo zuri ambalo na litatusaidia ikikumbukwa kwamba watoto wa wasomi kama sisi tuliopo hapa na viongozi, mtoto akipata mimba tu anarudishwa shule. Wanaopata shida ni watoto wa wakulima na wasiokuwa na uwezo, tuwasaidie. Ndugu zangu, hilo halina ubishi tuunge mkono tu Azimio la Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wengine labda niongezee kidogo tu kuongelea mazingira wanayopatia mimba hawa watoto sisi tunayajua, ni wenzetu wajanja, wenye hela basi, halafu hao hao wanakataa, watoto lazima warudi shuleni. Kwa msingi huo tuombe, tumesikia changamoto zinazowapata watoto wa kike pamoja na umbali wa shule, tunaomba katika maazimio mengine ambayo tupitishe hapa kwamba kama Serikali ilivyochukua hatua ya kujenga maabara ichukue nguvu ile ile kuhakikisha kwamba shule ziwe na mabweni ya watoto wa kike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukitaka hili suala pia liende vizuri, ndugu zangu tuulize Wizara ya Elimu imejipanga vipi kuimarisha elimu ya kujitambua katika shule. Wazazi wengine wanaogopa kuongea na watoto wao ili wajitambue kwamba ukifikia umri huu utaona haya na haya. Nawapongeza wazazi wanaofanya hivyo, kwa wale ambao hawafanyi hivyo naomba Serikali ijikite katika kuimarisha elimu ya kujitambua katika shule ili waweze kujua. Of course elimu hii ikitolewa itazingatia pia umri wa watoto, Serikali imejiandaa vipi kuhusu elimu ya kujitambua katika shule? Je, kuna walimu ambao wameandaliwa? Mimi naelewa, kuna walimu wengine ukiwaambia wafundishe somo hilo hawawezi, yeye mwenyewe anaona aibu. Je, kuna walimu ambao wameandaliwa kwa somo hilo ili litolewe vizuri?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda upande wa walimu; mimi pia ni mwalimu, ndugu zangu ualimu sio mchezo, inahitaji moyo mkubwa sana, changamoto nyingi walizonazo walimu wa nchi hii ninaamini zinaweza zikatatuliwa kama chombo kilichoundwa mwaka 2015, TSC, chombo cha kuhudumia walimu kitafanya kazi kama ipasavyo. Najua kipo chini ya Ofisi ya Rais, Waheshimiwa Mawaziri ninyi mnaelewa, ndiyo mnaosimamia mafanikio ya elimu, kwa hiyo mshauriane na TAMISEMI jinsi gani mtaimarisha TSC ambayo itasaidia lakini kama TSC itakuwa kama ilivyo sasa hivi ndugu zangu TSC haijaanza kufanya kazi vizuri. Kesi nyingi za walimu hazifanyiki kwa sababu hazipati fedha za kutosha, ofisi hakuna na wakati mwingine mahali ambapo Halmashauri nyingine zinafanya chini ya Ofisi ya DC, tunaomba Halmashauri zote zipewe uwezo na TSC ziweze kuimarika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba mshirikiane na TAMISEMI ili TSC ifanyekazi, lakini tukiichukulia kama ilivyo definition au maana ya mwajiri, mwajiri wa walimu ni nani? Mpaka sasa hivi ninavyojua waajiri ni 139 kutokana na idadi ya Halmashauri, TSC haijawa mwajiri. Sasa tunapokuwa na waajiri 139 hatuwezi kuwasaidia walimu, huwezi kujua changamoto zao kwa pamoja. Hata hii ya walimu fake, wangeweza kutambuliwa sana kama kungekuwa na TSC ambayo inampima mwalimu kabla haijampa mkataba, naomba TSC iimarishwe.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana tulimaliza Wizara ya Maji, nawaomba Wizara ya Elimu nayo kabla haijasajili shule kwanza iitake shule iwe na miundombinu ya kukusanya maji. Watoto wa shule wanapata taabu sana, unakutana nao barabarani wanabeba vidumu kwenda kutafuta maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusu shule binafsi nami na-declare interest, shule binafsi zinasaidiana na Serikali kuimarisha watoto wetu, kodi zimezidi. Kodi ni muhimu lakini zimezidi, tunaomba kodi wanazotozwa shule binafsi ziangaliwe ili na wao watoe mchango wao kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba labda nisimalize kuzungumza kabla sijasema suala la VETA. VETA ni muhimu sana kwa wanafunzi wowote wale wa kidato chochote kile. Urambo ilikuwa na VETA, Wilaya ilipogawanywa VETA imejikuta ipo Kaliua, kama Urambo tulikobaki hatuna VETA. Nawasihi wapenzi wangu, Waheshimiwa Mawaziri mtufikirie Urambo nasi tuwe na VETA kwa sababu naamini kwamba watoto wanaomaliza kidato cha nne, wanaomaliza darasa la saba ambao hawakupata nafasi ya kuendelea kwingine, mafunzo ya ufundi yatawasaidia sana kujiajiri na kuajiriwa na hasa kipindi hiki ambacho tunataka uchumi wa viwanda, Mafundi Mchundo na wengineo wote watapatikana kupitia VETA. Nawasihi VETA ziimarishwe zaidi ya yote mtusaidie na Urambo tupate VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaamini sana Waheshimiwa Mawaziri, najua kabisa mengi mnayafanya mazuri, lakini naomba mpokee yale yote yanayochangiwa na Waheshimiwa Wabunge kwa lengo la kuimarisha yale ambayo mnayafanya. Nawatakia kila la heri, akina Mama wanaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunisikiliza.