Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi hii asubuhi ya leo na mimi niweze kuchangia katika Wizara ya Elimu.

Kwanza, naunga mkono hotuba ya Wizara ya Elimu na pili naomba niwapongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa namna wanavyojituma kuhakikisha elimu ya Tanzania inainuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie dakika zangu nyingi nijikite katika mpango wa kuinua ubora wa elimu (Equip Tanzania). Nitatoa ushauri pamoja na ushauri wangu naomba Serikali nayo itanieleza imejipangaje kutatua yale ambayo mimi nitayaongea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango huu ni wa miaka minne unaotekelezwa na Serikali ili kuweza kuboresha elimu katika maeneo yaliyokuwa nyuma kielimu. Mpango huu upo katika mikoa saba na Simiyu ni mkoa mmojawapo uliopo katika mpango huu. Naupongeza sana mpango huu kwani umeweza kuinua kiwango cha ufaulu katika Mkoa wa Simiyu kwa kiwango cha asilimia 30.7. kabla ya mpango huu ufaulu katika Mkoa wa Simiyu ulikuwa ni asilimia 36.7 na Mkoa ulikuwa wa 24 kitaifa. Matokeo ya mwaka 2016 kiwango cha ufaulu kimeongezeka mpaka asilimia 67.4 na mkoa umekuwa wa 14 kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumpongeza sana Mkuu wa Mkoa wa Simiyu akisaidiana na Afisa Elimu wa Mkoa kwa namna wanavyoisimamia elimu na kutoa elimu mbalimbali kwa wananchi na wazazi wa Mkoa wa Simiyu. Pamoja na ufaulu huu bado kuna changamoto zilijitokeza ambapo watoto wa kike waliripotiwa kupata mimba na mimi ni mmojawapo niliyeshuhudia mwanafunzi amepata ujauzito akashindwa kuendelea na masomo yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la mradi huu pia ni kuinua ubora wa elimu inayotolewa hasa kwa mtoto wa kike. Mtoto wa kike katika mpango huu umemtaka amalize elimu ya msingi aendelee na elimu ya sekondari. Nikiangalia mtoto wa kike anazo changamoto nyingi sana ambazo zinaweza zikamsababisha asiweze kufaulu na kuendelea na sekondari ama akatishwe masomo yake na asiendelee na sekondari na kumaliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niweze kufahamu pamoja na ushauri wangu, je, Serikali imejipangaje kutokomeza yafuatayo katika mpango huu? Serikali imejipangaje kutokomeza mimba na ndoa za utotoni kwa kutoa elimu ya uzazi kwa wanafunzi? Nikiangalia katika shule zetu wataalam wa elimu ya uzazi ni wachache na sehemu zingine hawapo kabisa. Katika ajira hizi zinazotolewa za Serikali sijafahamu wakunga na manesi wataajiriwa wangapi. Naomba hilo pia liangaliwe wakati wa ajira. Tunao watumishi wa idara ya afya wanaofanya outreach service.
Nashauri pia waweze kufanya kazi hili kwa kwenda kutoa elimu katika shule za msingi na za sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna unyanyasaji wa kijinsia na udhalilishaji wa kingono. Serikali imejipangaje katika mpango huu kutokomeza hayo? Matukio yamekuwa yakiripotiwa kila siku. Juzi tarehe 9, Mkoa wa Mara mtoto wa miaka minne amebakwa, nasikia uchungu sana. Kwa mazingira haya bado itakuwa ni vigumu kwa mtoto wa kike kumaliza shule ya msingi na kuendelea na sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna tatizo la ukeketaji watoto wa kike. Pia napenda kupata majibu ya Serikali imejipangaje kulishughulikia tatizo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna tatizo ukeketaji wa watoto wa kike napenda kupata majibu, pia kuna tatizo la kutokuwa na usawa wa kijinsia katika elimu. Kwa mfano, shule ya Sekondari ya Itinje iliyopo Jimbo la Kisesa, Wilaya ya Meatu ilikuwa ya kwanza Kiwilaya, ya tatu Kimkoa, lakini shule hii ina tatizo la kutokuwa na matundu ya choo. Je, Serikali inaisaidiaje? Watoto wana hamasa ya kusoma lakini wana mazingira ambayo yanawakwamisha. Ninashauri, katika ule mpango wa RWSSP katika kile kipengele cha sanitation matenki ya maji yajengwe zaidi shuleni, ambapo matenki hayo yakijengwa lazima pia matundu ya choo yatajengwa. Kwa hiyo, ninaomba matundu hayo yakijengwa yapewe kipaumbele matundu ya watoto wa kike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna masuala ya adhabu yanayoweza kudhuru mwili au akili ya mtoto, tumeona juzi kuna mahali imeripotiwa watoto wamefungiwa kwenye safe mpaka wamefariki, Serikali ina mpango gani wa kumlinda mtoto katika adhabu zenye kudhuru mwili na akili shuleni, viboko visivyo na mpangilio na kufungiwa kwenye vyumba ambavyo havina hewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango, umejikita vipi katika kusaidia watoto walio katika mazingira hatari zaidi. Kwa mfano, watoto waliotelekezwa, watoto yatima, watoto walio katika umaskini wa kupindukia. Je, mpango umejikita vipi kupata mlo mmoja kwa watoto wakati wa mchana?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watoto walio nje ya mfumo rasmi wa elimu ambao wamepitwa na muda kutokana na kwamba wakati ule kabla ya elimu bure walikuwa wanashindwa kwenda shule kwa ajili ya michango na kadhalika. Je, Serikali imejipangaje katika elimu ya MEMKWA na elimu zingine ili kuweza kuwanusuru kuwatoa katika wimbi lile la ujinga?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango huu pia katika kila shule waliambiwa kuandaa business plan ili waweze kupata angalau milioni 1.5 kwa ajili ya elimu ya kujitegemea, tayari shule zimeshaweza kupatiwa mchango huu. Naomba kujua, je, katika lile darasa la mtihani la saba, hii elimu ya kujitegemea kuna watoto wa kike ambao watapata changamoto ya kutokwenda shule wakiingia katika siku zao za hedhi na katika darasa la saba naamini bado watoto ni wadogo lakini kuna one third ambao tayari wameshaingia kwenye hedhi. Je, katika elimu ya kijitegemea mpango ule umejikitaje hata kununua taulo kwa ajili ya watoto hawa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma Shule ya Sekondari ya Wasichana Weruweru toka form one hadi form four kwa kupitia elimu ya kujitegemea, tulikuwa tukipatiwa mataulo shuleni, sikujua gharama ya mataulo toka ninaanza mpaka namaliza. Kwa maana hiyo hata hili linawezekana maana yake katika mipango hii watoto wanaweza wakafanya miradi hata ya ufiatuaji matofali, kulima na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie pia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.