Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Ritta Enespher Kabati

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na kumpongeza Mheshimiwa Waziri Profesa Maghembe, Naibu Waziri, Engineer Ramo Makani, Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara kwa kutuletea bajeti yao ili tuweze kuijadili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hifadhi ya Wanyama ya Ruaha National Park ni hifadhi ya pili kwa ukubwa katika Afrika na hifadhi yenye wanyama wengi sana. Cha kushangaza hifadhi hii barabara inayoenda katika mbuga hii haina lami na kiwanja cha ndege cha Iringa hakuna ndege kubwa inayotua katika kiwanja hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sijajua Wizara hii inafanya juhudi gani kuhakikisha miundombinu ya kuwezesha watalii wanaofika na kufanya matangazo ya kutosha ili tupate watalii wa kutosha? Ni kwa nini Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, Serikali haiwekezi kama ilivyo Kaskazini? Kwani kuna vivutio vingi sana. Ni vizuri Serikali ingetupatia mkakati wa kuendeleza mbunga hiyo na utalii wa Nyanda za Juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma kitabu kilichotolewa na TFS kilichotoa mwongozo wa kutoa vibali, tunashukuru kwa kutangulia kutoa kipaumbele kwa wenye viwanda na wananchi watakaozunguka msitu; lakini nitoe ushauri wangu kwa Serikali kuwa katika mwongozo wake ungeongeza na yale makundi maalum; makundi ya akina mama wajane, akina mama wenye vyama vinashughulikia makundi ya kijamii. Kwa sababu tumeshuhudia mara nyingi wananchi wanaozunguka msitu hawafaidiki na rasilimali hiyo, wakati wao ndio walinzi wakuu wa mazingira hayo, hata wakati mwingine moto ukitokea wanakuwa wakitoa msaada mkubwa. Naiomba Serikali jambo hilo liangaliwe tena na tupatiwe majibu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iangalie upya suala la fidia kwa wananchi wanaopatwa na maafa. Kwa mfano, Mkoa wa Iringa kuna wananchi walipata matatizo ya kuuawa na mamba wengine kupata ulemavu.

Pia tembo walileta uharibifu wa mali na vifo katika Kata ya Nyanzwa, lakini tunashukuru Mheshimiwa Naibu Waziri Engineer Ramo alishawahi kufanya ziara katika eneo hilo na kilio kikubwa kilikuwa ni fidia kidogo sana ukilinganisha na uharibifu unaojitokeza. Ni vigezo gani huwa vinatumika au ni lini sheria itarekebishwa ili ianze kukidhi vigezo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wetu wa Iringa una vivutio vingi sana ambavyo bado hatuoni kama Serikali inavitendea haki ya kuvitangaza ili viweze kuchangia pato na kukuza utalii katika eneo la Nyanda za Juu Kusini. Tunaona kama upo ubaguzi. Nini mkakati?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.