Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii ya dakika tano, nitajitahidi kwenda kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sipingi kabisa kwamba ni lazima tuhifadhi misitu; huo ni utangulizi wangu, lakini haya yafuatayo naomba niyaseme kwa masikitiko. Tunayo migogoro ya mipaka baina ya hifadhi pamoja na wananchi kule Manyoni Mashariki. Nakumbuka tarehe 27 Mei, 2016 walikuja wawakilishi 18 walikutana na Mawaziri; Naibu Waziri Maliasili na Utalii na Naibu wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi na walitoa malalamiko yao kuna tatizo la kusongeza mipaka. Kuna hifadhi inaitwa Muhesi Game Reserve hii ni hifadhi mpya, ilianzishwa mwaka 1991.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya hapo wananchi hawa walikuwa wanaishi kwenye vitongoji salama lakini baada ya kuanzishwa hii Muhesi ambayo ilianzishwa na GN Namba 531 tarehe 4 Novemba, 1991 ndipo ikawahamisha wananchi karibu vingoji vinane.Vitongoji hivyo ni Chisola, Msisi, Itovelo, Machochoroni, Mkindiria, Chigugu, Ngongolelo pamoja na Chibwee. Haya maeneo yalikuwa ni potential kwa ajili ya kilimo; kwa mfano kulikuwa na eneo linaitwa Chiumbo ni eneo ambalo ni productive kwa kilimo cha mahindi, lakini pia kuna eneo linaitwa Iluma, eneo hili likuwa ni machimbo ya madini likiwa linatoa dhahabu ambayo haijawahi kushuhudiwa katika nchi hii, alluvial.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia taarifa za Benki Kuu za mwaka 1991 zinaeleza kwamba dhahabu inayotoka kwenye eneo hili hakuna katika nchi hii katika machimbo yote ambayo tumewahi kuyashuhudia, inaitwa alluvial.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini baada ya kutangazwa eneo hili pia likachukuliwa, ambapo ilikuwa ni kitegauchumi kizuri sana kwa wananchi wa Manyoni. Vilevile kwenye mito hii ya Muhesi na Kizigo ilikuwa ni source ya maji kwa ajili ya mifugo pamoja na wananchi. Baada ya hapo hatuna maji tena wala mifugo haiwezi kunywa maji pale. Pia tulikuwa tunafuga nyuki kwenye msitu ule wa Muhesi, sasa hivi hatufugi tena nyuki. Sasa ombi letu lilikuwa ni nini; ombi letu ni kwamba irudishwe ile mipaka ya zamani kwa sababu idadi ya watu imeongezeka, idadi ya mifugo imeongezeka pamoja na shughuli za kiuchumi zimeongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana Wizara ya Ardhi tulijadili sana mpango wa matumizi bora ya ardhi. Tunashindwa nini kugawa maeneo haya kwa kushirikisha wananchi kwamba wakulima kaeni huku na wafugaji kaeni huku, kitu gani kinashindikana?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Ardhi ilipewa jukumu hilo, lakini nadhani sijui ndiyo ile Tume imeundwa lakini Manyoni kule hawajafika. Cha kusikitisha zaidi hawa wananchi walipozungumza na Waheshimiwa Mawaziri wetu hawajawahi kutoa taarifa juu ya maombi haya mpaka hivi ninavyozungumza, ili niwapelekee wananchi wa Manyoni. Hawajawahi kuniita hata mimi Mbunge wao kueleza hata kwamba tumejadili kitu gani hebu wapelekewe majibu haya wananchi wa Manyoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie jambo la Utalii. Tuna kivutio kipya kinaitwa Kisingisa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.