Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi, ingawa ndiyo nimeingia, lakini niseme kidogo, nisije nikakosa nafasi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma hotuba ya Mheshimiwa Rais na kabla sijasema chochote kuhusu maudhui ya hotuba hii, nimefurahishwa na jambo moja.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni mmoja kati ya Wabunge wa upande huu tulioanzisha mageuzi miaka 20 plus iliyopita na tulipoanza kuna Mzee mmoja anaitwa Ndimara Tegambwage, aliandika kitabu kinachosema kwamba Upinzani Siyo Uadui.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema hilo kwa sababu, baada ya kupitia hotuba ya Mheshimiwa Rais, nimegundua kwamba mambo mengi ambayo tumeyasema kwa muda mrefu Mheshimiwa Rais ameyazingatia katika hotuba yake na jambo hili linanifurahisha sana, linaonesha kwamba alah, kumbe sisi sote ni Watanzania na kwamba mawazo tunayoyatoa huku, siyo mawazo mabaya, ni mawazo ya kuisaidia nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukuke nafasi hii kuwaomba viongozi wengine, Mheshimiwa Nape yupo pale, Mheshimiwa Jenista na wengine, muige mfano wa Rais, siyo kwamba kila kinachosemwa upande huu ni kitu kibaya.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, mimi nitachangia mambo matatu; la kwanza ni viwanda. Wazo la kufanya nchi yetu kuwa nchi ya viwanda ni wazo ambalo limechelewa sana. Mwalimu Nyerere alijitahidi, enzi za Mwalimu Nyerere tulikuwa na viwanda karibu katika kila zao, katika kila sekta, lakini bahati mbaya ndiyo hivyo viwanda vikachukuliwa, wengine wakavifisadi, wengine wakaviua na kadhalika. Sasa wazo hili, nadhani ndiyo wazo pekee ambalo litaisaidia nchi hii, kwa sababu ukiangalia sasa hivi ni bidhaa chache sana ambazo tunauza nje na kwa sababu hiyo, hata upatikanaji wa fedha za kigeni, unakuwa wa shida, ndiyo maana hali yetu ya uchumi inayumba mara kwa mara, dola inayumba mara kwa mara.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri ambao ningependa kutoa, maana yake Mheshimiwa Rais amesema kwamba, atajitahidi kufanya nchi yetu iwe nchi ya viwanda, lakini ningefurahi zaidi kama mwelekeo ungeanza kuonekana, kwamba ni viwanda vipi tunaanza navyo ili watu waandaliwe. Tusije tukaanzisha viwanda halafu matokeo yake tukauwa kilimo. Kama tunaanza viwanda ambavyo vitawasaidia watu wetu kujiandaa ili malighafi za hivi viwanda zitoke hapa hapa, litakuwa jambo bora zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu ukiangalia sasa hivi watu wanatoka vijijini, vijana wanatoka vijijini wanakuja mijini kuja kubangaiza na wanafanya hivyo kwa sababu kilimo sasa kinaanza kudharauliwa. Kijana anaona akifika mjini akishika soksi mbili,
tatu akizitembeza, anarudi kijijini anaonekana ni wa maana zaidi kuliko wale aliowaacha vijijini.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tuangalie vile viwanda ambavyo vitawafanya wakulima waweze kupata hamasa ya kuweza kuandaa malighafi kwa ajili ya viwanda vyenyewe ndiyo tuanze navyo. Nami nasema kwamba, Mheshimiwa Rais, pamoja na Serikali yake, kama mtajitahidi kuanza kufufua Viwanda vya Nguo, Viwanda vya Pamba, kwa sababu tunajua hapo nyuma jinsi Urafiki ilivyovuma, jinsi Mwatex ilivyovuma na viwanda vingine na mkifanya hivyo ni kwamba mnawahamasisha wakulima wa pamba kulima zaidi na vilevile kuweza kuona manufaa ya kilimo kwa sababu pamba yao itapata soko hapa hapa, pamoja na viwanda vingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, kwa sababu najua muda ni mchache, nisemee kuhusu maji. Utagundua na sidhani kama kuna Mbunge atasimama hapa bila kusemea suala la maji. Ningeomba sana suala la maji liwekewe kipaumbele kikubwa sana kwa sababu ndilo
suala ambalo linawatesa watu wetu ukiacha na mambo mengine. Pale Jimboni kwangu shida ya maji ni kubwa kuliko ambavyo mtu unaweza ukaelezea na hasa inapokuja wakati wa kilimo.
Ilisemwa hapa Bungeni kwamba sasa hivi mvua zinanyesha, lakini kwa experience ya pale Rombo maji yote yanakwenda nchini Kenya. Kule wameweka utaratibu wa kuyazuia. Matokeo yake kiangazi kikija, wale wa Kenya ndiyo wanatuuzia mboga na kadhalika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nilishasimama hapa Bungeni mara nyingi nikiomba kwamba, jamani wale wanaohusika na Wizara ya Maji, sisi tuna makorongo mengi sana pale Rombo, tusaidieni tuweze kuzuia yale makorongo ambayo yanapitisha maji mengi sana wakati wa masika ili baadaye wakati wa kiangazi yatusaidie. Yatatengeneza hata ajira kwa vijana wetu, vijana watalima mbogamboga, vijana watalima kilimo cha msimu wa kiangazi na kwa sababu hiyo tutapunguza umaskini wa hali ya juu sana miongoni mwa vijana wetu na tutatengeneza ajira miongoni mwa vijana wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna Ziwa pale linaitwa Ziwa Chala, lile Ziwa niliomba hapa nikaambiwa yale ni maji ya Kimataifa, ni maji ya Kenya na Tanzania, kwa hiyo, utaratibu utafanyika ili tuweze kupata maji yale yatumike pia na kwa watu wangu pale Rombo. Sasa cha kushangaza watu wa Kenya wanatumia maji ya lile Ziwa, lakini sisi tunahangaika na uhaba wa maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana katika hii mipango mizuri ambayo Rais ameeleza kwenye kitabu chake itufikishe maeneo kama hayo, mahali ambapo tunayo maji, maji ambayo Mwenyezi Mungu ametupatia na maji ya Ziwa Chala ni maji ya Mlima Kilimanjaro.
Theluji ile pale Kilimanjaro inapoyeyuka imetengeneza underground rivers ambazo zinakwenda mpaka pale Chala. Sasa wenzetu wa Kenya wanayatumia sisi tunabaki tunayaangalia. Kwa hiyo, wakati tunapoendelea kutengeneza sera zetu, mipango yetu kufuatana na hotuba hii ya
Mheshimiwa Rais, naomba sana maeneo kama hayo yaangaliwe. Mheshimiwa Naibu Spika, nimalize tu kwa kurudia ule wito wangu kwamba, jamani wote tunajenga nchi, nchi yetu hii ya Tanzania, kwa hiyo, mawazo ambayo yanatoka pande zote tuyapokee na tuyafanyie kazi, badala ya kupigana vijembe.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi uliyonipa. (Makofi)