Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi nitoe mchango wangu katika muda huu wa dakika tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maamuzi ya kuhamisha mifugo kutoka katika Mikoa ya wafugaji kupeleka Mikoa ya Kusini na hasa Mkoa wa Lindi yameleta athari kubwa za mazingira. Na kimsingi hakukufanyika upembuzi yakinifu wa namna gani mazingira yataathirika, maamuzi yale yamepelekea kuathiri sekta ya utalii, mazingira lakini pamoja na kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kijiji cha Ngea kuna zaidi ya mifugo 10,000 iko pale, lakini kijiji hiko hakiko katika mpango wa matumizi bora ya ardhi kwa ajili ya mifugo. Lakini ndicho kijiji ambacho kina hifadhi ya misitu ya Likonde na Mitalule na mifugo ile ipo ndani mle mle. Kwa hiyo sasa hivi kuna uharibifu mkubwa wa mazingira katika hifadhi ile.
Lakini isitoshe katika kile kijiji kuna Bwawa la Maliwe, bwawa ambalo linatunza viboko wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilifanya ziara kule kina cha maji katika Bwawa la Maliwe kinapungua kwa sababu lile bwawa liko jirani kabisa na Hifadhi za Misitu ile. Hivyo basi kutokana na uwepo wa mifugo maana yake mifugo inapelekea mmomonyoko wa ardhi na hivyo kina cha bwawa lile la Maliwe kinapungua. Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kuiomba Wizara ifuatilie katika maeneo hayo ninayoyaeleza kwa sababu vinginevyo mazingira ya uhifadhi wa misitu ni kama yanaenda kuharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la wakulima na shughuli zao za kilimo. Wakulima katika msimu wa mwaka huu katika kijiji cha Ngea na vijiji vya jirani ni kama hakuna watakachovuna kwa sababu mazao yote yameharibiwa na mifugo. Kwa hiyo, niiombe Serikali pia iangalie suala hilo ili basi wakulima wetu waweze kuepukana na baa la njaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kushangaza katika jitihada za kuhakikisha kwamba ile mifugo inatolewa pale Serikali ya Wilaya ya Kilwa ilifungua kesi mahakamani ili basi kuwaondoa wale wafugaji. Lakini katika hali ya kushangaza kwenda mahakamani Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Kilwa imeshindwa mahakamani na wananchi wanalalamika kwamba inaonekana kuna dalili ya rushwa. Wananchi wanalalamika iweje vyombo vya ulinzi na usalama vimeenda kuwakamata wafugaji katika maeneo ambayo hawakupasa wawepo, lakini wanapoenda mahakamani wanashindwa. Kwa hiyo niombe Wizara ifuatilie suala hilo wananchi wa maeneo hayo wanapatashida sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kuna suala la fidia kutokana na uharibifu unaofanywa na wanyama au kwa mazao au kwa binadamu. Katika jimbo langu la Kilwa Kaskazini tunapakana na Hifadhi ya Selous kuna wananchi wamejeruhiwa na wanyama, lakini taratibu zote zinazofanywa ili basi kupata fidia inachukua miaka mingi kupata fidia kutoka Wizarani. Kwa hiyo, niiombe Wizara kwamba kama ambavyo ninyi mnachukua hatua za haraka pale mwananchi anapomjeruhi mnyama au anapoua mnyama, basi iwe hivyo hivyo pale mnyama anapomjeruhi mwananchi zile fidia zipatikane kwa haraka. (Makofi)

Lakini sio hivyo tuu kuna suala zima la mashamba, kuna ekari nyingi za wananchi zimeharibiwa na ndovu, lakini taratibu zimefuatwa kupitia Maafisa wenu wa Maliasili lakini hakuna chochote kinafanyika baada ya taarifa kufika kwenu. Naomba sana hayo myazingatie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la mipaka kati ya hifadhi hizi na wanavijiji. Kuna tatizo kubwa la mipaka katika kijiji cha Namatewa na kijiji cha Ngarambe. Wananchi wako pale toka siku nyingi lakini sasa hivi inaonekana wenzetu wa Selous wanaidai katika eneo ambalo wananchi wapo wanadai kuwa ni eneo la kwao, kwa hiyo, tayari kumekuwa na migogoro baina ya hifadhi ya Selous na wananchi. Kwa hiyo, niiombe Wizara na hilo lishughulikiwe ili mgogoro uweze kuisha. Ahsante sana, nashukuru.