Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Dr. Haji Hussein Mponda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Malinyi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE.DKT. HADJI H. MPONDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia sisi wote kuwa wazima wa afya ili kukabiliana na majukumu yetu pamoja na kazi zetu za Ubunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili naomba nichukue fursa hii kukushukuru wewe mwenyewe binafsi kunipa nafasi angalau nitoe mchango wangu katika Wizara hii muhimu sana katika Wilaya zetu za Malinyi, Ulanga na Kilombero.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nafasi hii niitumie kutoa shukrani kwa Wabunge, wakazi wa Malinyi, wakazi wa Morogoro na Watanzania nzima kwa ujumla, ndugu, marafiki na majirani kwa pole, salaam za rambimbi na dua kuhusu kifo cha mzazi wangu Mzee Hussein Mustafa Mponda lakini tunajua fika sisi wote ni wa Mwenyezi Mungu na kwake tutarejea. Innalillahi Wainna Ilayhi Rajuun.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu leo utajikita kwenye eneo moja tu kubwa ambalo kutegemea hotuba ya Waziri imezungumzia Idara ya Wanyamapori na dhana ya ushirikishaji jamii katika uhifdhi wa wanyamapori na ardhi oevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ambayo inajikuta na migogoro inayojitokeza baina ya Hifadhi, Mapori Tengefu na Mapori ya Akiba na Vijiji vinavyopakana ni hasa imetokana na mabadiliko ya Sheria ya Wanyamapori ya mwaka 2009 ambapo kwa mabadiliko hayo yalivyofanyika, Serikali walipewa maelekezo wafanye mambo mawili:-

La kwanza, watafiti kama kuna ulazima wa uendelevu Mapori Tengefu kwa wakati huo ilikuwa 42; na la pili, ni kurejea mipaka ya Mapori Tengefu au Hifadhi kwa sababu sheria ya zamani ilikuwa inawaruhusu wakazi wa maeneo yale kutumia mapori yale lakini Sheria ilivyobadilika 2009 ikakataza. Niipongeze Serikali wameanza kutekeleza kwa ukanda wa kwetu kule Malinyi, Kilombero na Ulanga kwenye lile bonde la Kilombero, ardhi oevu yake na Pori Tengefu la Bonde la Kilombero. Walichofanya mwaka 2012 walirejea wakaangalia ile mipaka, wakaweka mpaka kati ya kiini cha Pori Tengefu la Kilombero na ardhi ya kijiji, ule mpaka wakauita buffer zone.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lile ni panasana lina- range wakati mwingine kilometa mbili mpaka kilometa 25 ambayo imesababisha vijiji karibuni 23 na vitongoji vyake 18 wananchi wanaishi kihalali maeneo yale. Vijiji vile vimesajiliwa, sasa hii ni changamoto ambayo Serikali waliiona pale na baada ya kupigia kelele, kuishauri Serikali nishukuru tena wamekubali kurejea upya mipaka ile na nawashukuru uongozi wa Menejimenti ya Bonde la Kilombero walitushirikisha wadau ngazi ya Halmashauri walituita Mikumi nakumbuka ilikuwa tarehe 20.10.2016, tumewekwa semina ya siku mbili kuonyeshwa umuhimu wa lile bonde na kuonyesha namna gani bonde na namna linavyoathiriwa na nini hatima yake. Kulikuwa na option tatu:-

(i) Aidha, kisiwepo nabuffer zone;

(ii) Iwepo na buffer zone lakini kuwe na masharti maalum; na

(iii) Imeridhiwa wadau wote wa mipaka ya buffer zone ile irejewe isiwe mipana kama kiasi kile ili kuokoa vijiji vile ambavyo viko kihalali na kuokoa maeneo ambayo wananchi tayari wameshaanza kutumia ambayo sasa itatusaidia kupunguza migogoro ya ardhi na pori tengefu lile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushahidi ulikuwepo; ukirejea matokeo ya utafiti wa wanyamapori (TAWIRI 2009, 2010, 2011) na mtafiti mmoja ambaye ni mtaalam wa wanyamapori katika Mkoa wa Morogoro ni Ndugu Joseph Joachim Chuwa alifanya utafiti kwa kushirikiana na SUA waliangalia changamoto, waliangalia masuala ya kijamii na uchumi yanayosukuma uhitaji wa ardhi na uendelevu wa lile bonde na baadae tafiti ile ilihitimisha kwamba ni vyema wadau, ni vyema wananchi wahusishwe ili kulilinda lile bonde na mimi nasema wananchi wa Malinyi, Ulanga na Kilombero ndiyo tunanufaika na lile bonde, tuko tayari na tunalipenda sana maisha yetu tunategemea lile bonde.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotokea, hao hao Serikali wenyewe hawasimamii ipasavyo bonde lile kwa sababu sisi hatuwezi kulima ndani ya bonde lile karibu na ule mto ambao unakuwa protected, ni watu wanatoka mbali na Serikali wanawatazama siku zote matokeo yake wanatuathiri sisi ambao wanasema hawa wakazi wa Wilaya hizi tatu wao ndiyo waharibifu wa lile bonde owevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali kipindi hiki wamerejea tena kuweka mipaka. Niwashukuru wamechukua dhana kweli shirikishi lakini ajabu yake na hii naomba heshimiwa Waziri unisikie kwa makini sana; kwamba wataalam wale kutoka Wizara ya Ardhi, TAMISEMI na Maliasili na Utalii wanakwenda kila kijiji, wanaongea na wananchi, wanaongea na viongozi, tunafikia muafaka kwamba mpaka wa lile buffer zone uwe wapi. Tunaelewana kabisa, tunakubaliana lakini sasa kinachofanyika wanapokwenda kuweka mipaka ile kwenye beacon wanatofautiana makubaliano ya awali na wananchi wale. Sasa mimi niwahoji; mnasema shirikishi mnawashirikisha wananchi, wananchi wamechukua muda wao, wameeleza matatizo yao, wataalam wenu mumewatuma kule lakini hamtaki kusikia mnakwenda kuweka beacon kama mnavyotaka, kwa kusema hapo hamtatatua tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri niwaombe, nimeongea na wataalam hawa wanawanyooshea vidole ninyi viongozi wa Wizara. Wansema tumeongea na wananchi na tumekubaliana lakini tunapokwenda kule wanatu-monitor, wanatufuatilia kwa njia ya TEHAMA, wanasema lazima mpaka uwe hapa. Kama ni hilo ni kweli hamtutendei haki kabisa wananchi wa Wilaya hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwakumbushe Mheshimiwa Maghembe najua bado utarudi mwaka 2020 na najua bado una sifa na utapenda kuwa Waziri, sasa hapa changamoto iliyopo 2020 Mheshimiwa Rais wakati tunamnadi kwenye Jimbo la Malinyi tarehe 05.09.2015 alisimama kwenye jukwaa baada ya kuelezwa changamoto hii, aliahidi ataongeza ardhi ya kutosha, ataongeza maeneo yale ambayo wananchi wapate kuendesha shughuli zao za kila siku. Labda mimi niseme tu, hapa changamoto kubwa siyo kwamba hatutaki bonde lile tusililinde, hapana, changamoto kubwa lile buffer zone ni pana mno; wewe umeona wapi buffer zone kilometa 25? Kawaida ya buffer zone ni kilometa angalau mita 500, angalau kilometa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe basi mtusikilize buffer zone ile muipunguze badala ya kuwa na kilometa 25, kilometa 8, kilometa 12 iweke ile standard yenu kama ilivyokuwa buffer zone kwenye maeneo mengine ya kilometa mbili ambayo itatuwezesha sasa kwanza, kutekeleza ahadi
ya Mheshimiwa Rais na hiyo itakuwa njia rahisi Mheshimiwa Rais atapita tu kama barabara imewezeshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo zoezi linaendelea tuna ombi maalum watu wa Malinyi; kwamba kwa kuwa wanaweka hiyo mipaka kwahiyo watu wanaoishi kule siyo kihalali kwenye ile kiini cha pori wataondolewa na wakiondolewa kule kuna mifugo itahamia kwenye milima.

Tunaomba mtusaidie Halmashauri hawana uwezo wa kulinda ile milima na ile milima ndiyo vyanzo vya maji yanayotiririka katika lile Bonde la Kilombero na hatimae unakuwa mto unaelekea mpaka unakuwa Mto Rufiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana, ahsante.