Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kunipa nafasi hii ili nichangie katika Wizara hii ya Maji.

Kwanza, nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyenipa uhai na uzima nimefika siku ya leo. Pili, niishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa inayofanya hasa kwa hiki kidogo ambacho kimekuja. Wengi hapa tumesimama tunalaumu kweli pesa ni ndogo,ni kweli nami nakubaliana kabisa pesa ni ndogo, hata ile bajeti tuliyopanga haijaenda ni kweli lakini nilikuwa najua kwa sababu pesa ni ndogo basi tungekuja na mawazo mengi zaidi ya kuishauri Serikali namna gani inaweza kuongeza pesa. Kwa kusema hayo, nami niungane na wenzangu waliotangulia, pamoja na mambo yote kutokana na umuhimu wa maji ni vizuri tukaongeza bajeti katika mafuta ile ya shilingi 50 kwa lita ili tuongeze Mfuko wa Maji uweze kuwa na fedha ya kutosha twende tukaongeze bajeti ya maji ili kutatua tatizo la maji nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo niende kwenye ukurasa wa 71 wa kitabu cha Waziri kuhusu Bwawa la Kidunda. Hili Bwawa la Kidunda mwaka jana tulipitisha bajeti hapa na tulilitengea shilingi bilioni 17 na baada ya kufuatilia mimi mwenyewe Hazina walishatoa shilingi bilioni 10. Madhumuni makubwa ya hiyo shilingi bilioni 17 ilikuwa ni kujenga ile barabara ya Ngerengere - Kidunda kwenda kwenye mradi lakini pia kulipa fidia ya shilingi bilioni nne kwa watu walioathirika kupisha barabara na sehemu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa masikitiko makubwa sana, mpaka hivi tunavyoongea pesa hizo zimetolewa Hazina lakini hata senti tano haijalipwa kwa hao waathirika wa Kidunda, Chanyumbu na sehemu nyingine.

Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri akija anieleze, bahati nzuri Mheshimiwa Naibu Waziri ni shahidi, wiki mbili zilizopita watu walikuwa hawaamini kama Mbunge wao anafuatilia fedha hizi, walikuja hapa bila taarifa mpaka Wizara ya Maji kufuatilia hela hizi. Tulikutana na Waziri tunamshukuru sana alitupa ushirikiano na alituambia kwamba zipo hela nusu shilingi bilioni mbili. Cha kushangaza mwaka jana tulikwenda Wizara ya Maji, tuliambiwa ziko nusu shilingi bilioni mbili hizo hizo, mwaka huu tena mwezi wa tatu tumefika ziko shilingi bilioni mbili hizo hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunaomba Serikali ije ituambie kwamba hizi shilingi bilioni mbili zitapatikana lini na hawa watu watalipwa lini ili waweze kuendelea na shunghuli zingine na pia hizi shilingi bilioni mbili zilizobaki Serikali ituambie itatoa lini ili mradi huu uweze kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini baada ya fidia hiyo kulipwa, pia huu mradi ni wa muda mrefu sana na una umuhimu mkubwa sana kitaifa, ni vizuri sasa tupate kauli ya Serikali. Kila kitabu cha bajeti kinachokuja, cha mwaka jana kimekuja wanasema tunatafuta fedha, mwaka huu kimekuja wanasema tunatafuta fedha, fedha zipo kwa watu binafsi. Kama pesa hakuna, tuishauri Serikali ikaingia ubia na private sector kutekeleza hii miradi mikubwa kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu nasema hivyo mradi huu umeanzishwa tangu mwaka 1955 na wakoloni. Baada ya kupata uhuru mwaka 1962, Mwalimu Nyerere kutokana na umuhimu wake aliona tuendelee na mradi huu. Mwaka 1982 likaja tena andiko tuendelee, nashangaa sana mwaka 1994 Serikali kwanza imeupunguza mradi wenyewe kwa sababu wakati ule mradi huu ulikuwa ni zaidi ya lita milioni 430 leo umepunguzwa ni lita milioni 190.

Naomba niishauri Serikali, kutokana na umuhimu wa maji, kutokana na kilimo cha kubahatisha, kutokana na mabadiliko ya tabianchi ni vizuri tukazingatia andiko lile lile la mwanzoni ili huu mradi uwe multi-purpose badala ya single use kwa ajili ya matumizi tu ya binadamu. Ni vizuri tukarudisha kule ili tuweze kutumia kwa ajili ya umwagiliaji pamoja na matumizi ya binadamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, niende sasa kwenye suala la Jimbo, hii ilikuwa ni mradi wa kitaifa. Sisi mwaka jana hapa tunashukuru Serikali tulipata mradi mmoja pale Mikese ambao ulikuwa unachukua zaidi ya shilingi bilioni mbili na mwongozo Serikali ikautoa yenyewe wakasema hawawezi kutuma pesa mpaka kwanza mkandarasi aanze. Tunamshukuru sana huyu mkandarasi ameshafanya kazi zaidi ya asilimia 40 na juzi ameshusha zaidi ya semi-trailer tatu ya mabomba yote ya mradi ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali, tushaandika certificate zaidi ya tatu lakini bado hatujapata majibu, Mkurugenzi wangu hajapata majibu na pesa hazijakuja. Nimeona kwenye kitabu cha Waziri kwenye bajeti mwaka huu imeshushwa hii bajeti imewekwa shilingi bilioni
1.7 wakati mradi ule peke yake una shilingi bilioni mbili.

Kwa hiyo, naiomba Serikali yangu Tukufu, ni vizuri tukaleta hela hizi mapema kabla hii bajeti haijaisha kwa sababu kama hizi hela hazijaletwa kabla bajeti haijaisha mkandarasi atasimama baadaye mtakuja kutuletea hizi hela shilingi bilioni 1.7 kama zitapatikana mwakani zitakuwa haziwezi kutosheleza kutekeleza mradi huu wala miradi mingine. Kwa sababu hii tunayotumia ni cash budget, naomba sana Serikali ikazileta hela hizi za kumlipa huyu mkandarasi ili ule mradi wa Mikese aumalizie kabla ya mwaka huu wa fedha haujaisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nataka nichangie kwenye mradi wa Chalinze Awamu ya Tatu. Mradi wa Chalinze Awamu ya Tatu na sisi watu wa Morogoro Kusini Mashariki na Morogoro Vijijini ni wanufaika kwani kuna vijiji kama saba vitapata maji katika mradi huu...

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, nataka kujua tu Serikali mradi huu itaumaliza lini ili vijiji vyangu vya Bwawani, Ngerengere, Kidunda na Kidugalo na kambi zetu zote zile za Jeshi kwa maana ya Kinonko zipate maji.