Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami nichangie katika hoja iliyopo mezani. Pia namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na nawashukuru pia wananchi wa Urambo kwa kunipa ushirikiano. Aidha, naipongeza Serikali ya Mheshimiwa Rais Magufuli kwa kazi kubwa wanayofanya akisaidiana na Mawaziri wake, hongereni Mawaziri kwa kazi kubwa. Vilevile pia nawapongeza wanawake wenzangu walioshinda uchaguzi jana, hongereni akinamama mnaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudi kwenye maji. Naomba nianze mchango wangu kwa kuuliza maswali manne. Kila ninapozungumzia suala la uhaba wa maji Urambo naambiwa subiri mradi wa maji kutoka Malagarasi kilomita 200 kutoka Urambo. Swali la kwanza, Mheshimiwa Waziri anayehusika aniambie ni hatua gani za dharura zitachukuliwa ili wananchi wa Urambo wapate maji wakati wakisubiri mradi kutoka kilomita 200? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kama kweli mradi wa Malagarasi umetiliwa maanani, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuwa ana-wind up aniambie ametenga shilingi ngapi za kuanza mradi huu katika mwaka huu wa fedha 2017/2018. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la tatu, je, Serikali haioni kwamba ni rahisi kuchukua maji kutoka Lake Victoria kuyapeleka Tabora na kuyafikisha Urambo kilometa 92 badala ya kusubiri maji kutoka kilometa 200? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la nne, kama kweli Wizara imejipanga kutatua tatizo la maji, naomba waniambie kwa nini hadi leo shilingi milioni 647 zilizotengwa kwa ajili ya kutafuta vyanzo vingine vya maji na mradi maalum wa Kijiji cha Izimbili mpaka leo hazijapatikana? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeuliza maswali hayo kwa makusudi kwa lengo zuri tu la kuonesha kwamba tukisubiri utaratibu wa fedha uliozoeleka kila siku hatuwezi kupata maji. Ndiyo maana ukiangalia bajeti ya mwaka jana shilingi bilioni 900 zilitengwa hatimaye tukapata shilingi bilioni 181 tu na kati ya hizo shilingi milioni zipatazo 90 zilitokana na Mfuko wa Maji. Ndiyo maana unaona Wabunge wengine wote waliochangia wanasema hivi, tutunishe Mfuko wa Maji kwa kuongeza Sh.50 ziwe Sh.100 kwa sababu kwa bajeti ya kawaida imeshindikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, natoa ombi kwa Serikali, kwanza ianzishe Mfuko wa Maji Vijijini kama ilivyo umeme. Tunaamini kukiwa na Mfuko wa Maji Vijijini itakuwa rahisi kusambaza maji. Kwa msingi huo, Serikali ikikubali kupata shilingi 50 zaidi kutoka kwenye petroli au dizeli, sawa, cha maana hapa tupate tu shilingi 100 kuchangia Mfuko wa Maji. Hata hivyo, iwapo Serikali itaona kutoa shilingi 50 kwenye petroli na dizeliinaweza kuathiri sehemu nyingine basi ile shilingi 50 itokane na Mfuko wa REA tuchukue kidogo na Mfuko wa Barabara ili tupate Mfuko wa Maji Vijijini wenye fedha ambazo zimechangiwa kwa shilingi 100. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna asiyefahamu umuhimu wa maji, kila mtu anafahamu umuhimu wa maji. Kwa msingi huo, naomba Waziri atakapokuwa ana-wind- up hebu atoe kauli ya kuwapa moyo wananchi wa Urambo kwamba mwaka huu ni nini kitafanyika ili wapate maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la tatizo la maji la kudumu katika shule za msingi. Shule za msingi na sekondari nyingi ukipita, mimi juzi nimezungukia kwenye shule hawana maji. Sasa napendekeza, hii nipamoja na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia waone umuhimu wa kutokusajili shule hadi pale shule imeshawekewa miundombinu ya kuvuna maji ya mvua pamoja na taasisi nyingine. Kwa sababu kwa utaratibu ulivyo hata kama maji yatatoka Lake Victoria, Malagarasi mpaka maji yafike kwenye shule na nyingine ziko mbali sana, kwa kweli ufumbuzi wa kudumu ni kwamba shule au taasisi za aina hiyo zisipate usajili mpaka zioneshe miundombinu ya kutega maji ya mvua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumalizia napenda kusema kwamba Serikali ikikubali ombi la kuongeza Sh.50 ili kutunisha Mfuko wa Maji. Pia ianzishe Mfuko wa Maji Vijijini ili kumtua mwanamke ndoo. Bila hivyo kwa bajeti ya kawaida imeonekana haiwezekani. Naamini Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Magufuli ni sikivu kwa upande wa maji mtakubali hilo kuwe na Mfuko wa Maji Vijijini. Hii itasaidia wanawake kuondokana na kubeba maji kutoka mbali jambo ambalo linawasababisha washindwe kufanya kazi nyingine za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kupata nafasi hii