Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi jioni hii ili na mimi niweze kuchangia juu ya sekta hii muhimu katika maisha na maendeleo ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kutoa pole nyingi sana kwa wazazi, wanafunzi na Walimu na Watanzania kwa ujumla kwa ajili ya ile ajali mbaya iliyotokea kule Karatu, iliyochukua maisha ya wanafunzi wetu wengi na Walimu. Mwenyezi Mungu aweke roho zao mahali pema peponi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna ubishi juu ya suala la umuhimu wa maji. Kila mtu anafahamu, wanyama wafugwao wanafahamu hata wale wa porini wanafahamu umuhimu wa suala hili. Hata Vitabu Vitakatifu vya Mungu vimeeleza juu ya umuhimu wa maji kwa maisha ya mwanadamu tangu uumbaji. Kwa hiyo, naomba tusilifanyie mzaha na mchezo suala la maji kwa maisha ya watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na kitabu cha Waziri. Ukienda ukurasa wa saba imeandikwa 72.5% ya Watanzania waishio vijijini wanapata maji safi na salama katika umbali wa mita 400. Mheshimiwa Waziri takwimu hizi amezitoa wapi? Uhakika wa takwimu hizi ameufanyia kazi kiasi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wewe pia umekuwa ukikaa kwenye Kiti hicho mara nyingine asubuhi, katika Kipindi cha Maswali pale asubuhi, kukiwa na swali la maji, Wabunge tunabanana kupata nafasi hiyo, hicho ni kiashiria cha kutosha kwamba eneo hili la maji lina matatizo makubwa. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri, hizi takwimu zake hebu azirejee kama kweli ziko sahihi. Haiwezekani kama 72% ya Watanzania waishio vijijini wanapata maji, Wabunge wangepaza sauti zao kiasi hiki humu ndani, isingewezekana! Kwa hiyo, takwimu hizi nina wasiwasi hazina usahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tena wanasema ndani ya mita 400. Wengi tulioko humu ndani tunatoka vijijini, hizi mita 400 zimesemwa kwenye sera lakini nadhani si kweli kwamba asilimia hiyo inapata maji kwa kiasi hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jana tumewasilishiwa bajeti hapa ambayo mwaka jana tulipoipitisha, leo hadi mwezi wa tatu utekelezaji wake ni 19.8%. Naamini kwenye jambo hili kuna mkono wa mtu. Haiwezekani kwenye bidhaa muhimu kama maji tunapata asilimia ndogo kiasi hicho. Nawaomba ndugu zangu Mawaziri hapo mjitizame na mjipime kama kweli mko sahihi kuwa hapo kwenye Wizara hii muhimu namna hii, hii asilimia ni ndogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika,kwa hiyo, Watanzania tujiandae kushuhudia sasa migogoro mingi ikitokea kwenye vyanzo vya maji kwa sababu vyanzo vya maji ni vichache. Watoto wetu waende shule asubuhi wamebeba vidumu vya maji kwa sababu shule hazina maji. Akinamama wetu watembee kilomita nyingi kutafuta maji kwa sababu maji hakuna. Afya ya Watanzania iendelee kuwa rehani kwa sababu ya kutumia maji yasiyo safi na salama na yale mengine ambayo yanafanana na hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naungana na wale ambao wanasema tuongeze tozo kwenye fedha za mafuta. Ukiangalia katika zile fedha ambazo zimetolewa shilingi bilioni 181, asilimia 57 ya fedha hii imetokana na Mfuko wa Maji. Kama tumeweza kupata asilimia 57 kutoka kwenye Mfuko wa Maji, naamini tukiongeza mara mbili tunaweza kupunguza tatizo hili la maji kwa kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia najiuliza tulikuwa tumetoka kwenye ule Mpango wa Progamu ya Maji - WSDP I sasa tumeingia kwenye WSDP II na tumeaminishwa siku za nyuma kwamba hizi ni fedha za Benki ya Dunia. Hizi fedha za Benki ya Dunia zipo wapi kama miradi tunatekeleza na fedha za Mfuko wa Maji?

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda katika bajeti ya mwaka 2017/2018, asilimia ndiyo hiyo imeshuka kutoka shilingi bilioni 900 sasa tumekwenda shilingi bilioni 600. Bajeti ya mwaka jana, Wilaya ya Karatu tulikuwa tumetengewa shilingi bilioni 1.4 lakini hadi sasa tunavyoongea tumepata shilingi milioni 540, bado shilingi milioni 610. Mheshimiwa Naibu Waziri yuko kwenye Kiti hapo naomba sasa wakati wanajumuisha watuambie, naamini tatizo hili la kutokupeleka fedha za mwaka jana haliko kwenye Jimbo la Karatu peke yake bali ni maeneo yote, katika miezi hii miwili iliyobaki fedha hizi wanazipeleka lini. Miradi haikamiliki kwa sababu fedha hawazileti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwenye jedwali 5(a) ambapo fedha zimetengwa kwa kila wilaya au kwa kila jimbo, pale utaona mambo ya ajabu sana. Ziko wilaya mwaka jana zilipewa shilingi bilioni mbili, tatu na kadhalika na safari hii zimepewa hivyo hivyo. Ziko wilaya zimepata mgao wa shilingi milioni 500, 600 au 700, kwa nini tunatofautiana namna hii? Kama sungura ni mdogo basi tugawane wote ili kila mtu apate hicho kidogo. Mbona wakati wa vile vijiji kumi vya ule Mradi wa Benki ya Dunia tulipewa kila mtu vijiji kumi kumi! Kwa nini leo hii wengine wana mabilioni na wengine wana milioni tena chache sana? Hili ni jambo ambalo halikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sitakuwa nimewatendea haki wananchi wa Bonde la Eyasi kama sitasema kuhusu mradi wao wa umwagiliaji. Nashukuru Naibu Waziri upo hapo na ulifika katika bonde lile, tuna mgogoro mkubwa wa uhifadhi wa chanzo cha maji Qangded.Bahati nzuri Waziri Mkuu alifanya ziara kule Mangola mwezi wa kumi na mbili, wananchi walimlilia kiongozi wao na kiongozi wao akawasikiliza. Waziri Mkuu alitoa kauli ya Serikali kwa kusema chanzo kile cha Qangded kihifadhiwe kwa umbali wa mita 500 na mashine zote zilizowekwa kwenye mto ziondolewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha kusikitisha hadi leo tunavyoongea bado mashine zile ziko kule mtoni zinachukua maji mengi na wananchi wanaokaa chini hawapati bidhaa hiyo. Bado zile mita zilisemwa na Waziri Mkuu hazijafanyiwa kazi. Naomba kufahamu, hivi ni nani wa kutekeleza kauli hii ya Waziri Mkuu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Mangola walimsifu na walimpongeza sana Waziri wao Mkuu kwa kutambua kero yao lakini viongozi wale wa chini wameshindwa kufanya kazi ya kupima mita zile zilizowekwa kuanzia kwenye chanzo hadi kwenye ziwa. Kwa hiyo, wakati watakopojumuisha naomba walizungumzie hili suala la chanzo cha Qangded katika Bonde la Eyasi.