Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niseme yangu katika Wizara hii ya Maji na Umwagiliaji. Awali ya yote, nachukua nafasi hii kutoa pole zangu kwa wenzetu wa Arusha kutokana na msiba wa wanafunzi. Namwomba Mwenyezi Mungu azilaze roho zao mahali pema peponi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuunga mkono wale wote wanaosema kwamba bajeti ya Wizara hii iongezwe. Kwa ukweli kabisa kama tuna kusudio la kutaka kuwatendea haki wananchi wa Tanzania, basi tuna kila sababu ya kuongeza bajeti ya Wizara hii ili wananchi wakapate maji ya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, falsafa ya kumtua mama ndoo kichwani, ililenga zaidi kwa wananchi wanaoishi vijijini. Kwa mazingira yetu, sehemu nyingi za mijini zina maji na ikiwezekana miundombinu yake, maji haya yanaenda kabisa mpaka majumbani. Sehemu ambazo bado akinamama wanabeba ndoo kichwani ni sehemu za vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukifuatilia bajeti, bado imekuwa na upendeleo zaidi kwa maeneo ya mijini kuliko maeneo ya vijijini. Jimbo langu ni la kijijini na hakuna mradi wowote wa maji uliotengwa katika bajeti hii. Nimesoma kwenye kitabu hiki hakuna chochote kilichowekwa kule. Sasa ina maana kwamba mwaka huu wa fedha unanipita hivi hivi. Namwomba Mheshimiwa Waziri, wananchi wa Jimbo la Kilwa Kaskazini awaangalie, hakuna chochote alichotenga kwa ajili yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimeangalia pale, Mkoa wa Lindi umetengewa pesa kama 1.1 billion fedha za wafadhili. Basi naomba zile pesa ziwaangalie pia wananchi wa Jimbo la Kilwa Kaskazini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nachukua nafasi hii kupendekeza kuanzishwa kwa Wakala wa Maji Vijijini, kwa sababu vinginevyo basi mgawanyo wa keki hii, wenzetu wa mijini au wenzetu wa baadhi ya Majimbo watakuwa wanapata zaidi kuliko sehemu nyingine. Kwa hiyo, basi uanzishwe Wakala wa Maji Vijijini ili vile vijiji ambako ndiko Watanzania wengi wanaishi waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo, nijielekeze katika matatizo ya maji katika Jimbo langu. Jimbo langu ambalo lina Kata 13, kuna Kata kama sita hivi, bado hazijawa na mradi wowote wa maji. Kuna Kata ya Somanga ambayo iko pale barabarani haina mradi wa maji, Kata ya Kinjumbi, Kata ya Kibata, Kata ya Chumo, Kata ya Namayuni na baadhi ya vijiji katika Kata ya Kipatimu; kuna Vijiji vya Nandete, Intikimwaga, Nandemo, Mkarango na Kijiji cha Nasaya; vyote hivi havina mradi wowote wa maji. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri ayaangalie maeneo hayo nao waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napongeza utekelezaji wa Wizara kwa Mradi wa Maji wa Mingumbi Mitete. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri, tumekuwa tukishirikiana na ule mradi umeelekea kukamilika. Ule mradi unapitia katika Kijiji cha Njia Nne. Namwomba Mheshimiwa Waziri wananchi wa Kijiji cha Njia Nne wapate maji katika mradi ule kwa sababu haiwezekani likapita bomba tu pale halafu wao waliangalie. Ule mradi unaopeleka maji katika Vijiji vya Mingumbi, Poroti, Nangambi na Ipuli, Tingi, Mtandango na Miteja, lakini wale wa Njia Nne wamesahaulika. Kwa hiyo, naomba pia na wale wa Njia Nne waweze kupata maji katika ule mradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo, nijielekeze katika matumizi ya chanzo cha Mto Rufiji. Tumekuwa tukiona hapa, vyanzo vyote vikubwa vya maji tayari vinatumika kwa ajili ya matumizi ya maji kwa wananchi wa maeneo hayo. Kuna chanzo cha Ziwa Victoria, Mto Malagarasi na sehemu nyingine; lakini mpaka sasa na nimekuwa nikishauri mara kadhaa, Serikali haijakiangalia chanzo cha Mto Rufiji kwa ajili ya wananchi wa Rufiji na Kilwa. Mpaka sasa yale maji yanapotea tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Mamlaka ya Uendelezaji wa Bonde la Mto Rufiji wanaita RUBADA. Wapo pale, lakini sioni kama kuna jitihada zozote zinazofanyika, maana hakuna mipango yoyote ya umwagiliaji inafanyika pale; yale maji yanatupita tu hivi hivi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri atakapokuja atuambie ana mpango gani wa kuhakikisha kile chanzo cha Mto Rufiji kinatumika kwa manufaa ya watu wa Rufiji, Kibiti, Kilwa, Kilwa Kusini na maeneo ya jirani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, nijielekeze katika ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali. Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali anaeleza kuwa kuna zaidi ya pesa shilingi bilioni nne zinapotea kutokana na miradi kukamilika, lakini kutotumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) na tumefanya ziara za ukaguzi wa miradi maendeleo katika sehemu mbalimbali za nchi hii. Tulichojifunza huko, kuna miradi mingi inakamilika, lakini haitumiki na moja ya miradi hiyo ni miradi ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kuna mradi kule Nachingwea, kuna mradi kule Tabora, miradi ile imekamilika lakini haitumiki. Tatizo kubwa, kuna shida kubwa kwa Ma-planner wetu wa Halmashauri. Wasanifu wetu, wanasanifu miradi ambayo baada ya kuja kukamilika wananchi wanashindwa kuitumia. Kwa mfano, kuna mradi pale Nachingwea, ili wananchi waweze kutumia ule mradi, basi inahitaji ndoo moja ya maji inunuliwe kwa sh.300/= kitu ambacho wananchi hawawezi kumudu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuna shida kubwa kwa wataalam wetu wa Halmashauri kusanifu hii miradi. Naomba wataalam wanapokaa na kusanifu hii miradi wawe makini sana na wawashirikishe wananchi kuona namna gani wao wanaweza wakaimudu hiyo miradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.