Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru sana kwa kunipa nafasi hii, kuchangia bajeti ya maji. Awali ya yote niishukuru sana Serikali kwa kuweza kukamilisha baadhi ya miradi ambayo ilianzishwa kwenye Halmashauri yangu ya Wilaya ya Mpanda, naipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja nashukrani za dhati ambazo Serikali imezifanya na kuonesha jitihada za maksudi za kutatua kero ya maji lakini bado Mkoa wa Katavi kwa ujumla tunatatizo kubwa sana la maji. Suluhisho la Mkoa huu katika kutatua tatizo la maji ili tuwe na uhakika wa kupata maji safi na salama ni vyema sasa Serikali ikajielekeza kupanga mipango mikakati ya kuleta maji kutoka ziwa Tanganyika mpaka Manispaa ya Mpanda sambamba na Halmashauri ya Nsimbo ili iweze kutekeleza mradi ambao kimsingi utatatua tatizo kubwa sana la maji. Mradi huu ukianza kwa kiwango kikubwa kwenye eneo la jimbo langu utasaidia sana kutatua tatizo la kero ya maji katika kijiji cha Itetemya, Kapalamsenga, Kaseganyama, Kasekese, Nkungwi, Sibwesa, Ikaka, Kabungu mpaka Mpanda Mjini. (Makofi)

Meheshimiwa Naibu Spika, tunaiomba sana Serikali ielekeze nguvu kutatua tatizo la maji kwa kuyatoa maji Ziwa Tanganyika. Kama maji yanatoka Ziwa Victoria kuja Mkoa wa Tabora, zaidi ya kilometa mia 300 itashindwaje kuyaleta maji kutoka Ziwa Tanganyika mpaka Manispaa ya Mpanda Mjini ambapo ni kilometa 120 tu? Nilikuwa naomba sana hilo tulipe nguvu ili tutatue tatizo la maji ndani ya Mkoa wa Katavi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu miradi ya maji vijijni; maeneo haya vijijini kunashida kubwa sana ya maji. Nilikuwa naomba sana kwenye jimbo langu, kata ya Muhesi ni eneo ambalo kuna tatizo kubwa sana la maji, na kuna chanzo kizuri cha kutega maji tu ambacho kingetatua sana vijiji vyote vilivyopo kwenye kata ya Muhesi vikawa havina tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tuna maeneo kwenye kata za Mishamo ambako kimsingi Serikali haikuwekeza, ni eneo ambalo kuna Watanzania wapya, eneo hili bado tunatatizo kubwa sana la miundombinu ya maji. Nilikuwa naiomba Serikali ipeleke huduma kwenye vijiji vya kata ya Mishamo, kata ya Ilangu, kata ya Bulamata ili kuweza kutatua tatizo la maji kwenye maeneo ambayo kimsingi yalikuwa yakihudumiwa na UN sasa hivi yako mikononi mwa Serikali. Tunaomba sana Serikali iongeze huduma ya maji kwenye vijiji hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ya umwagiliaji; tuna miradi ya umwagiliaji ambayo ilianzishwa na Serikali. Eneo langu tunamradi wa scheme ya Karema, Mwamkuru na Kabage. Hii miradi imechukua muda mrefu sana na imetumia fedha nyingi ambazo kimsingi zimechezewa tu na watu ambao walipewa dhamana ya kuisimamia. Miradi hii inaonekana ni mashamba ya fedha ambayo yanaliwa, lakini hayaleti tija ambayo imekusudiwa na Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii miradi imepewa fedha nyingi, lakini haisimamiwi vizuri, bahati mbaya sana hata Wizara yenyewe ambayo inatoa hizo fedha haina usimamizi, ni fedha ambazo zinachukuliwa tu kiana aina na zinaliwa bila kuwa na usimamizi wowote. Naomba Serikali iangalie kwenye maeneo haya na ninaomba Serikali ituhakikishie itakapokuwa inaleta majibu hii miradi itaikamilisha vipi ili iweze kufanya kazi iliyokusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni usimamizi wa miradi. Serikali itakuwa inatoa fedha nyingi na kutoa ndani ya Bunge na Waheshimiwa Wabunge wakashangilia kwamba wamepata miradi, kama hakuna usimamizi mzuri hakuna kitu chochote kitakachokuwa kinafanyika. Kwa sababu fedha inatoka Serikalini inaenda kwenye Halmashauri ambapo hakuna usimamizi, halafu zile fedha ukizifuatilia zinarudi makao makuu. Tunaomba hili likomeshwe, tusidanganywe tuwe tunapewa changa la macho kwamba tumeletewa fedha baadae zinarudi kule ambako zilitoka. Tunaomba hii tabia ikomeshwe na tuhakikishe kwamba imefanyiwa kazi ili iweze kutekelezwa kama ilivyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu nyingine ambayo tungependa kuchangia ni uwiano wa miradi ambayo tunagawiwa. Sehemu hii ni vyema sasa Serikali na Wizara kwa ujumla ikaangalia, kwa sababu fedha nyingi zinazotolewa ukiangalia mgawanyo ambao unagawanywa kwenda kwenye maeneo husika tunatofauti kubwa sana. Sasa tunaomba tupewe vigezo ni vigezo vipi ambavyo vinafanya maeneo mengine yanapata fedha nyingi na maeneo mengine yanapata fedha kidogo. Ukiangalia pengine maeneo ambayo yana fedha kidogo yana idadi ya watu wengi kuliko maeneo ambako yanapelekwa fedha zingine. Tunaomba Serikali iangalie ili tuweze kwenda sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la bajeti; bajeti ya Wizara ya Maji mwaka huu imepungua lakini bado Watanzania walio wengi wanahitaji huduma ya maji. Mimi niiombe Serikali, ni vyema sasa tukajipanga kuhakikisha bajeti hii inaboreshwa na tusitoe fedha kwenye zile mradi wa REA hapana, naomba tukate kwenye simu, tunaweza tukapata fedha nyingi sana ili ziweze kuwasaidia wananchi kupata maji ambayo yatawasaida walio wengi. Vijijini kuna matatizo makubwa sana ya maji, hasa kwa akina mama, ni vyema Serikali sasa ikaangalia mfumo wa kupeleka huduma ya maji vijijini ambako ndiko Watanzania waliowengi wanaishi. Inavyoonekana ukiangalia vitabu hivi, karibu asilimia kubwa ya huduma ya maji inapelekwa maeneo ya mijini, lakini tunadanganyika, asilimia kubwa ya Watanzania wanaishi vijijini na hawa ndio ambao wanahitaji huduma ili waweze kuzalisha na kuweza kulisha wananchi wanaoishi mijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, naunga mkono, lakini nitahitaji majibu ya Serikali ili tuweze kuangalia ile miradi ambayo imeletwa na Serikali.