Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizari ya Maji na Umwagiliaji

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili na mimi niweze kuchangia kwenye hotuba iliyoko mbele yatu. Nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali cha kusimama mbele ya Bunge letu Tukufu na kuweza kuwasilisha mawazo ya watu wa Mkinga.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie firsa hii vilevile kuwapa pole ndugu zangu wa Mkinga kwa maafa makubwa waliyoyapata kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha katika Jimbo letu la Mkinga na kwa Mkoa wa Tanga kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa za Kituo cha Utafiti cha Mlingano zinasema mvua zinazoendelea kunyesha sasa zimefikia milimita 316 katika span ya siku tatu. Kiwango hiki ni kikubwa sana, mvua hizi hazijawahi kuoneka kunyesha kwa miaka 40 iliyopita. Kwa hiyo, tunapozungumzia madhara yaliyotokana na mvua hii tunaiomba Seriakli ilichukulie jambo hili kwa umakini mkubwa. Hivi ninavyozungumza mabwawa yangu saba katika Wilaya ya Mkinga ambayo yanatusaidia kupata maji yamepasuka. Miradi ya maji ambayo mabwawa yamepasuka ni Bwagamacho, Horohoro border, Doda, pamoja na Machimboni na mradi wa maji Maramba mabomba yamesombwa na maji, kwa hiyo, mpaka kwenye hospitali yetu ambayo sasa tunaitumia kama Hospitali ya Wilaya imekosa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, bwawa la maji Mwanyumba ambapo sambamba na hilo kuna daraja kubwa limepsuka na daraja limekatika, kwa hiyo, mawasiliano kati ya Tarafa ya Maramba na Makao Makuu ya Wilaya ya Mkinga yamekatika. Scheme yetu ya umwagiliaji Mwakijembe imesombwa na maji, mitaro imejaa mchanga, hekta karibu 98 za mazao zimesombwa. Athari yake; takribani watu zaidi ya 10,000 hawana maji.

Naiomba Serikali ilichukulie jambo hili kwa uzito mkubwa na kwa uharaka ili huduma ya maji iweze kurejeshwa. Ninawaomba ndugu zangu wa Mkinga waendelee kuwa wavumilivu Serikali ninaamini italifanyia kazi jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo ya utangulizi naomba nianze mchango wangu kwa kunukuu taarifa ya wataalam katika jarida la World Water and Sanitation. Katika mchango wao pale wanasema na ninanukuu:-

“The world does not stand a chance without water, it spread disease, compromise safety, makes education elusive and economic opportunity further out of reach. The lack of access to safe and clean water is deadly, dangerous and major obstacle to people of developing world becoming economically empowered and it is what it is standing between billions of people and their health, safety, opportunity to unlock their potential.” Mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali yangu isikubali ukosefu wa maji ukazuia fursa za maendeleo kwa watu wetu. Naiomba sana Serikali yangu isikubali ukosefu wa maji ukawa chanzo cha vifo vya watu wetu.

Wale tuliokuwemo kwenye Bunge lililopita wanakumbuka, tulijadili mambo kwa kina hapa katika Bunge hili wakati tunazungumzia kuweka tozo kwenye mafuta ya taa ili kupata fedha za kupeleka umeme vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia watakumbuka sentiments zilizokuwepo, hofu ya kuleta mfumuko wa bei na kadhalika, lakini tuliishauri Serikali na hatimae ikakubali, tukaweka tozo kwenye mafuta ya taa na leo kila mtu anashangilia upatikanaji wa umeme vijijini. Wananchi walikubali maumivu yale na leo wanashangilia umeme vijijini. Tusiwe wazito kukubali ushauri wa Bunge hili kuongeza tozo ya mafuta ili tupate fedha za kupeleka maji vijijini, let us unlock the potential of our people, tuwape maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Makao Makuu ya Mkinga hayana maji. Nimelisema hili kwa muda mrefu, nafurahi leo katika hotuba hii nimeona Wizara imetenga fedha kwa ajili ya kutengeneza mradi wa maji pale, lakini fedha zile nimeona zinagusa maeneo mengi, nimeona shilingi bilioni mbili pale; lakini fedha zile zinaigusa Handeni na maeneo kadhaa. Hofu yangu ni kwamba inawezekana fedha zile zisiweze kutosha kukamilisha jambo lile. Shida ya maji kwenye mji wa Kasera ni kubwa mno, naomba twendeni tukatekeleze mradi ule wa kutoa maji Kinyatu ambao utagusa kata za Mkinga, Parungu- Kasera, Boma pamoja na Manza. Tusaidieni tupate maji kwenye Makao yetu makuu ili tuweze kuujenga mji wetu, tuweze kuwahakikishia watu wetu afya bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine nilisema hapa kwenye bajeti iliyopita kwamba mji wa mpakani wa Horohoro ambako tumejenga Kituo cha Biashara ya Pamoja (One Stop Border Post) hauna maji. Tunapata aibu, watu wanakwenda kuchota maji Kenya. Tulikuwa na bwawa dogo pale ambalo lilikuwa linasaidia watu, leo hii ni miongoni mwa maeneo niliyosema hata bwawa hilo limepasuka.

Mhesimiwa Naibu Spika, tunao mradi, tumeshafanya usanifu unaotoa maji Mwakikonge, mradi ule unahitaji shilingi bilioni sita, tutakuwa tumemaliza tatizo lote la maji kwenye eneo lile. Naomba Serikali tusaidieni watu wale wapate maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni yamekuwepo malalamiko ya maji ya mji wa Tanga kuchafuka. Chanzo cha maji yale yanatoka Bosha na Mhinduro…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wale hawana maji, tunaomba muwapatie maji.