Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wote wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kazi nzuri ya kuendeleza michezo na sanaa. Pia napenda kuwapongeza kwa hotuba nzuri ya bajeti ya Wizara hiyo kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uongozi uliotukuka na hasa kuhakikisha maendeleo mazuri ya Sekta ya Habari, kuendeleza utamaduni, mila na desturi za Mtanzania, kuimarisha tija na kulinda kazi za sanaa na pia kuendeleza michezo katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, napenda kuwapongeza Mheshimiwa Majaliwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri za kusimamia shughuli za Serikali na kuhakikisha utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2015 - 2020.

Mheshimiwa Spika, Tanzania kama ilivyo kwa nchi zingine ina jukumu kubwa la utambulisho wa Taifa, kupitia Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo. Nchi yetu imesheheni vipaji mbalimbali na kinachohitajika ni kuibua hivi vipaji na kuviendeleza.

Mheshimiwa Spika, vipaji vingi vya michezo vipo vijijini na juhudi za makusudi zinahitajika kuibua vipaji vya michezo na sanaa huko vijijini ili viendelezwe. Michezo na sanaa ni ajira nzuri sana kwa dunia ya leo na pia ni utambulisho mzuri wa Taifa letu (National brand) na michezo pamoja na sanaa vinaleta heshima kubwa kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Mbeya Vijijini na hata Mkoa mzima wa Mbeya kuna vipaji vingi katika michezo hasa mpira wa miguu na riadha. Serikali ichukue hatua za makusudi za kimkakati wa kuibua hivi vipaji ikiwa ni pamoja na kuhimiza michezo mashuleni na kujenga viwanja vya michezo vijijini.

Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa kipekee wa Shirika la Utangazaji la Taifa (TBC) ambalo ni tegemeo la Watanzania walio wengi vijijini kupata habari mbalimbali kwa muda mrefu TBC haisikiki katika maeneo mengi vijijini na wananchi wanakosa fursa ya kupata habari. Pamoja na kutengewa bajeti ya shilingi bilioni moja katika Mwaka wa Fedha 2016/2017, lakini ripoti ya Kamati inaonesha bado utekelezaji na pia kiasi hiki ni kidogo ukilinganisha na mahitaji halisi ya uwekaji wa vyombo vya aina yake. Naungana na maoni ya Kamati ya kushauri Serikali kuwekeza vya kutosha katika Shirika la Utangazaji (TBC).

Mheshimiwa Spika, kutokana na tatizo la wizi wa kazi za Wasanii wakiwemo waimbaji wa Injili, nashauri Serikali iweke mkakati wa kulinda kazi za wasanii ili waongeze kipato kwa kazi zao na pia mapato ya Serikali yataongezeka.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.