Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Grace Sindato Kiwelu

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia machache katika Wizara hii. Nianze kwa kutoa pole kwa msiba mkubwa tulioupata katika nchi yetu kwa ajali iliyotokea katika Mkoa wa Arusha.

Mheshimiwa Spika, utamaduni; nchi yetu imebarikiwa kuwa na makabila 126 na kila kabila lina mila na desturi zake na kwa pamoja ndiyo zinatengeneza utamaduni wetu. Ila bado vipo baadhi ya vitu katika tamaduni hizo ambavyo vinadhalilisha wanawake. Kwa mfano, ukeketaji, kutokutoa umiliki kwa wanawake na kurithi wanawake wanaofiwa na waume zao hata kama wanawake hao hawataki. Katika jambo hili la ukeketaji ngariba wameanza kutumia mbinu mpya ya kukeketa watoto wachanga, hili jambo ni baya sana. Mambo haya bado yanaendelea pamoja na kuwa na jitihada za kupiga vita mambo haya.

Mheshimiwa Spika, napenda kujua katika bajeti hii Serikali ioneshe wazi itafanya nini kukomesha tamaduni na desturi hizi mbovu zinazomdhalilisha mwanamke na mtoto wa kike. Ufike wakati wa kuzirasimisha baadhi ya tamaduni katika mfumo rasmi ili kuziondoa zisizofaa.

Mheshimiwa Spika, michezo; kumekuwa na jitihada za kuhamasisha mpira wa miguu kwa vijana walio chini ya umri wa miaka 17, Serengeti Boys, lakini hakuna nguvu ya kutosha kuhamasisha uwekezaji kwenye mpira wa miguu na michezo mingine. Pamoja na timu hizi za Serengeti Boys na Kilimanjaro Queens kufanya vizuri, bado hazipewi kipaumbele cha kutosha wakati vipo vipaji na wana uwezo wa kufanya vizuri kimataifa na kwa sasa timu hizo zimeweza kufanya vizuri katika michezo yao. Kwa mfano Kilimanjaro Queens, hawa ni wanawake, walichukua Kombe la Afrika Mashariki na Kati mwaka jana.

Mheshimiwa Spika, ili timu zetu zifanye vizuri ni lazima tuwekeze tuwe na chanzo cha kuaminika cha kuwekeza pesa kwenye michezo na lazima kuwekeza na kuupa mwamko wa kutosha mpira wa miguu kwa akinamama. Umefika wakati sasa kuwe na chanzo cha kuaminika cha kuwekeza pesa kwenye michezo na njia rahisi wanayofanya duniani kote ni kupitia Bahati Nasibu ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, hapa kwetu Serikali haitengi pesa kwenye bajeti na hakuna njia ya kuupa pesa mchezo na mchezo wa bahati nasibu unasimamiwa na Wizara ya Fedha badala ya Wizara inayohusika na michezo. Nashauri bahati Nasibu ya Taifa iwe chini ya Wizara hii ili kiwe chanzo cha upatikanaji wa fedha katika michezo na kuwezesha timu zetu kushiriki katika mashindano.

Mheshimiwa Spika, habari, uhuru wa vyombo vya habari; sheria tuliyopitisha hapa Bungeni ina vipengele vinavyolalamika na ni vizuri Serikali ione haya na kuvipitia na ikaangalia namna ya kuvibadilisha ili kuweka uhuru wa vyombo vya habari wa kweli. Tumeona hivi karibuni vyombo vya habari vikivamiwa na viongozi wakiwa kwenye maeneo yao ya kazi, tumeona kwenye vyombo vya habari wanahabari wamepigwa wakiwa wanatekeleza wajibu wao.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha mchango wangu.