Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia Wizara hii ya Habari, Utamaduni na Michezo. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri pamoja na mazingira magumu.

Mheshimiwa Spika, nianze na hili la TBC, naona wenzangu wengi wameliongelea suala hili. Bahati nzuri Spika wewe ni shahidi, nilipokuwa Mbunge kipindi cha mwanzo miaka 20 nilikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge, Katiba, Sheria na Utawala na Utawala ilikuwa ni pamoja na Waziri Mkuu na TBC ilikuwa kwenye Kamati yangu, nimetembelea mitambo yote ya TBC karibu nchi nzima. Hiki ni chombo cha Serikali, kwa nini vyombo vya watu binafsi vifanye kazi nzuri, matangazo yasikike vizuri kuliko TBC?

Mheshimiwa Spika, ni jambo la kusikitisha lakini hatuwezi kumlaumu Dkt. Rioba - Mkurugenzi wa TBC ni kwa sababu ya ufinyu wa bajeti. Kwa nini Serikali isitenge fedha za kutosha kununua mitambo ya kisasa ili TBC isikike kama redio zingine za watu binafsi? Kwa hiyo, huo ndio ushauri wangu. Wafanyakazi wa TBC wanafanya kazi usiku na mchana, waboreshewe maslahi yao na ndio maana wanahama kwenda vyombo binafsi kwa sababu ya maslahi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili nizungumzie habari, habari haziko mjini tu, ziko vijijini. Ukienda Wilaya ya Mpwapwa Vijijini utapata habari, kuna watu wanafanya kazi za kujitolea vijijini. Ukienda Wilaya ya Kongwa, Zoisa, Mlali, Kibakwe, Mpwapwa kule sehemu za Mima, Matomondo watu wanafanya kazi nzuri sana ya kujitolea lakini hawatangazwi, hawa waandishi wa habari wanazunguka mjini tu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nashauri kila wilaya iwe na mwandishi wa habari. Mheshimiwa Waziri ananisikiliza au anaongea na Naibu Waziri? Kila wilaya iwe na mwandishi wa habari wa Serikali ili aweze kupeleka taarifa hizi za maendeleo katika wilaya zetu lakini siyo kuandika taarifa za mjini tu, kila siku mjini, hapana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, uandishi wa habari ni taaluma na ina mipaka. Huwezi kuandika jambo lolote unalotaka wewe haiwezekani, lazima kuna mipaka yake, uandike kwa kuzingatia maslahi ya nchi yetu. Siyo unaandika kwa kujifurahisha upate fedha kama biashara, no, lazima uandike taarifa kwa kuzingatia maslahi ya nchi yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho ni michezo. Mimi ni mpenzi wa Simba Sports Club. Kila siku timu ya Simba ikicheza lazima utasikia Lubeleje anaipongeza Simba, anaitakia ushindi. Sasa tumenyang’anywa point tatu, Bwana Malinzi sitaki kuzisema sana hizo, lakini mimi ni Hakimu, kwenye court of law ukishakiri jambo, umekiri. TFF walikiri kwamba kweli yule mchezaji wa Kagera Sugar alikuwa na kadi za njano tatu, that is plea of guilty. Huwezi kusema kwa sababu umesemasema sana, mmekosea halafu mkamnyang’anya point zake, hilo naiachia TFF. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mpwapwa nilikuwa na Timu ya Mji Mpwapwa, imecheza ligi kuu miaka tisa na ilikuwa inaogopwa na timu za Yanga na Simba. Nikubaliane na mwenzangu aliyesema Timu ya Taifa siyo lazima wachezaji watoke Simba na Yanga tu, hapana, tunaweza kupata wachezaji wazuri hata wilayani huku. Kongwa kuna Timu ya Hengo ni nzuri sana. Kwa hiyo, nashauri Mheshimiwa Waziri

arudishe michezo shule za msingi na sekondari, UMISHUMTA na UMISETA, huko ndiko tunakopata wachezaji wazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimekuomba dakika tano na dakika tano nimemaliza, lakini nashukuru sana Wizara hii kwa kufanya kazi nzuri, waendelee hivyo hivyo ila ombi langu kila wilaya ipate mwandishi wa habari, tuache kuweka waandishi wa habari wote mjini, hapana.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.