Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya yangu kuendelea kuimarika. Nitumie fursa hii kuwatoa wasiwasi wapiga kura wa Ulyankulu, nina imani Mwenyezi Mungu atanilinda mpaka 2020 tukamalizana salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kuwapongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake Kwa hotuba iliyoletwa mbele yetu na kwa sababu Mheshimiwa Mwakyembe hana muda mrefu pale, pamoja na kwamba yeye ni mtu wa habari, lakini tumkaribishe na tuna imani naye, kazi itakwenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kumpongeza mtangulizi, Mheshimiwa Nape. Sisi wanamichezo tulifarijika sana naye na niseme tu alifanya kazi nzuri, haya mengine ni ajali za siasa. Nimtie moyo Mheshimiwa Nape, asikate tamaa na kwa sababu yeye ni msanii, basi aendelee kuwepo kwenye vuguvugu letu hili la michezo na usanii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wote tunafahamu sasa timu yetu ya Serengeti Boys kama siyo jana basi watakuwa wameshafika Gabon. Ni juu ya sisi sote kuonyesha mshikamano juu ya timu hii. Kuzijenga timu, hazijengwi kwa maneno. Kuzitengeneza timu zipate mafanikio, hazitengenezwi kwa maneno. Kwa sasa nchi nzima na familia ya wanamichezo tunachangia mafanikio na gharama mbalimbali za Serengeti Boys. Nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge, tushiriki basi kwa dhati badala ya kushiriki kwa maneno tu na kuwalaumu wenzetu wa Wizara kana kwamba kila jambo wanafanya wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata huko Hispania, Madrid, Barcelona wapo watu wanahangaika nazo. Ukienda Uingereza, Liverpool, Manchester United au timu ya wenzangu wale ambao wanaishi kwa wasiwasi Arsenal, zote hizi zinatengenezwa na watu. Tusiishie tu kusema maneno na kulaumu, tujaribu kushiriki na sisi katika kuhakikisha maendeleo haya tunayoyasema yanafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, liko jambo ambalo kila mwaka mimi nalisema, hata kabla sijaingia Bungeni nimekuwa nikilisema. Mimi kama mwanamichezo ni juu ya michezo mashuleni. Hiyo Taifa Star tunayoizungumza ya mwaka 1980 iliyocheza mpira kule Nigeria, sehemu kubwa ya waliocheza kule walitoka mashuleni, walitengenezwa.

Mheshimiwa Spika, michezo ya shule za msingi, michezo ya sekondari, michezo ya vyuo ilikuwa ni chachu ya kutengeneza wachezaji kwenye michezo yote. Iwe riadha, iwe mpira wa miguu, iwe netball ambayo sasa sijui inaelekea kufa, itabaki Bungeni tu sijui! Yote ilitengenezwa kutoka mashuleni. Sasa hatutaki kusema juu ya waliotangulia wakafuta michezo ile mashuleni adha yake tunaiona.

Mheshimiwa Spika, sasa michezo imebaki kwenye shule mbalimbali chache ambazo siyo za Serikali, wanatusaidia sana kuhakikisha michezo inakwenda vizuri. Je, Serikali, TAMISEMI, Wizara ya Habari na Wizara ya Elimu kwa nini sasa isishirikiane kuhakikisha michezo mashuleni inarudi kama zamani na iwe ndiyo jiko letu la kupika wachezaji na wanamichezo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri, hebu utakapokuwa unakuja kuhitimisha, hebu ingia kidogo pale utufafanulie mambo yalivyojipanga kwa ajili ya michezo mashuleni. Bahati mbaya simuoni Mheshimiwa Profesa Ndalichako, angekuwepo na yeye ni pamoja na Mheshimiwa Simbachawene, hizi Wizara zote tatu zishirikiane…

SPIKA: Mheshimiwa Ndalichako yuko Arusha, kutuwakilisha kwenye lile jambo la msiba ule mkubwa.

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Spika, ahaa basi.

Mheshimiwa Spika, ni kwa sababu na mimi sikuwepo.

Mheshimiwa Spika, maana yangu ni kwamba Serikali iko hapa, ione umuhimu huo. Badala ya kuwa tunasubiri mafanikio tu kama alivyosema Mheshimiwa Mtolea, kwamba tunasubiri mtu ameshinda huko, tunamleta hapa Bungeni na kupiga naye picha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimekuwa nikizungumzia juu ya Watoto, mabingwa wa Dunia wa michezo ya Watoto wanaoishi katika mazingira magumu. Timu yetu ya Mwanza na mwaka kesho tunakwenda Kombe la Dunia; je, Serikali sasa ina mpango gani wa kuisaidia hiyo timu ikafanye vizuri? Hivi karibuni timu ya walemavu ilikuwa inashiriki mashindano pale Uingereza; je, inasaidia nini kutaka kwa watoto hawa?

Mheshimiwa Spika, suala nyingine ni juu ya viwanja. Bahati mbaya sana Serikali yetu haina viwanja vya kutosha. Tunavyo viwanja hivyo; Kiwanja cha Uhuru pamoja na Uwanja wa Taifa, lakini muda sasa umefika Serikali itengeneze viwanja vyake yenyewe, kuliko kutegemea viwanja ambavyo sasa ni mali ya taasisi nyingine.

Mheshimiwa Spika, pia viwanja hivyo visitengenezwe Dar es Salaam tu. Dodoma hapa tunahitaji kiwanja, tunahitaji kiwanja Mwanza, tunahitaji Arusha, viwanja vya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni juu ya makato. Mimi nashiriki sana michezo hii, makato ni makubwa sana kwenye viwanja. Watu wanakusanya pesa lakini pesa hizi zinakusanywa na wachezaji. Wachezaji wanachapa kazi ndiyo maana pesa inapatikana, lakini makato ni makubwa kiasi kwamba yaani faida inayobaki iwe kwa TFF, iwe kwa Chama cha Mpira cha Mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ni Mwenyekiti wa Chama cha Mpira Mkoa wa Tabora. Nafahamu, yaani kinachokuja kubaki ni kitu kidogo sana. Serikali basi iangalie; je, inajenga viwanja hivi kuwakomoa wanamichezo? Je, inajenga viwanja hivi ili shughuli ibaki ya matamasha au ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, tuna michezo ya Afrika Mashariki ya Bunge. BungeSports Club imesajiliwa kwa kanuni zile zile kama za Simba, kama za Azam kama za Yanga. Tuna michezo hii lazima Wizara ioneshe kutuunga mkono kama Bunge Sports Club. Tumekuwa ni watu ambao kama vile sisi tunacheza michezo mingine tu ambayo haitambuliki. Bunge Sports Club na ninyi Mawaziri mko humu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine, BungeSports Club ni club ya Wabunge wote na wafanyakazi wote. Nawaomba Mawaziri kutumia jukwaa hili; Mawaziri fikeni basi mje mfanye mazoezi na sisi. Pia mshiriki, muwepo kutuhamasisha kuona kwamba michezo ya Afrika Mashariki inayokuja tunaweza kushinda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, ninaunga mkono hoja ya Waziri.