Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii ili nami nichangie katika Wizara hii muhimu kwa mustakabali wa afya na uzima wa Watanzania. Naipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, hususan Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu ya Wizara hii kwa utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa ari na kasi kubwa hasa katika ongezeko kubwa la kibajeti na upelekaji fedha hususan za dawa katika Halmashauri zetu. Vilevile naishukuru Serikali kwa kuonesha nia na kutuweka katika mpango wa kuboresha huduma ya afya na upanuzi wa miundombinu katika Kituo chetu cha Afya Mkuyuni ili kiweze kutoa huduma za upasuaji na wodi za akinamama ili kuwa na uzazi salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi na shukrani hizo, naomba kutoa maombi yangu kwa niaba ya watu wa Morogoro Kusini Mashariki na Morogoro Vijijini kwa ujumla, kama ifuatavyo:-

(i) Ahadi ya Rais kuhusu gari la wagonjwa. Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, alituahidi kutupatia gari la kubebea wagonjwa katika Kituo cha Afya Mkuyuni tangu mwaka 2010 na mwaka 2014 katika Kituo cha Afya, Kinole, mbele ya aliyekuwa Waziri wa Ujenzi ambaye kwa sasa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli baada ya kupokea ombi hilo toka kwa watu wa Kinole kupita kwa Chifu Kingalu Mwana Banzi wa 14 lakini mpaka sasa magari hayo hayajapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali yangu kupitia kwa Mheshimiwa Waziri kutekeleza ahadi hii ya Mheshimiwa Rais na kutupatia magari hayo mawili ili kuokoa maisha ya watu wetu hasa akinamama wakati wa kujifungua ukizingatia hatuna hospitali ya wilaya na hali ngumu ya kijiografia katika eneo letu kutokana na milima iliyoko kule Kinole. Pia, tunategemea Hospitali ya Mkoa ya Rufaa ambayo iko mbali na jimbo na halmashauri yetu.

(ii) Ombi la Hospitali ya Wilaya. Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro ni ya muda mrefu lakini mpaka sasa hatuna hospitali ya wilaya na kutegemea hospitali ya mkoa. Ombi langu ni kuomba Serikali kutujengea hospitali ya wilaya ili kutoa huduma karibu na wananchi na kupunguza msongamano katika hospitali ya mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa ushauri wangu, wakati tunasubiri ujenzi wa hospitali ya wilaya ambao utachukua muda, naomba Serikali iteue kituo kimoja cha afya kati ya Tawa, Dutumi, Mkuyuni ama Ngerengere kuwa hospitali ya wilaya ili kutoa huduma kwa wananchi kutokana na halmashauri kwa sasa kuhamia kijijini Mvuha ambapo ni mbali na hospitali ya mkoa.

(iii) Kutokana na hali ya kijiografia ya Jimbo letu, naomba Serikali kutujengea na kuzipandisha hadhi zahanati za Mikese Station, Mkulazi, Tununguo, Seregete, Kinole, Kibuko na Kiroka kuwa vituo vya afya ili kutoa huduma kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja.