Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Salma Rashid Kikwete

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mchinga

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. SALMA J. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama ili niweze kutoa mchango wangu kwa Taifa langu. Pili, nimpongeze sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa utendaji wake mahiri wenye nia thabiti ya kuwaletea Watanzania maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, nawapongeza Waziri wa Afya, Mheshimiwa Ummy Mwalimu na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Hamisi Kigwangalla kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kusimamia sekta ya afya hapa nchini. Nina faraja kubwa kwamba juhudi wanazofanya katika kusimamia sekta ya afya zinaonesha matunda chanya. Nina imani kubwa na utendaji wao na sina shaka kwamba sekta ya afya chini yao itaendelea kuimarika siku hadi siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kuongelea jitihada katika kupambana na vifo vya wanawake na watoto. Tafiti mbalimbali zilizofanywa na taasisi za kiserikali na zisizo za kiserikali zimeonesha kuwa Tanzania imejitahidi kwa kiasi kikubwa katika kupambana na tatizo la vifo vya akinamama na watoto walio chini ya miaka mitano. Jitihada hizi ni matokeo ya hatua za dhati zilizochukuliwa na Serikali katika kuhakikisha kuwa inaimarisha huduma mbalimbali katika sekta ya afya kama vile upatikanaji wa vifaa tiba, chanjo za watoto na huduma za kinga pamoja na tiba za magonjwa kama vile kuharisha, utapiamlo, surua, malaria na maambukizi katika mfumo wa upumuaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na jitihada zilizofanyika katika kupambana na vifo vya akinamama wajawazito na watoto walio na umri chini ya miaka mitano bado kumekuwa na changamoto mbalimbali. Changamoto hizi zimebabishwa na matatizo kama vile upatikanaji wa huduma bora za dharura za uzazi kwa akinamama hasa maeneo ya vijijini ambapo akinamama wajawazito wengi hufariki kwa kukosa huduma za upasuaji wa dharura wakati wa kujifungua; upatikanaji wa damu salama kwa akinamama ambao hupoteza damu nyingi wakati wa kujifungua; hali duni ya akinamama wajawazito hasa maeneo ya vijijini ambapo huhitajika kwenda na vifaa kama vile gloves, pamba, sabuni
na vifaa vingine vya kujifungulia jambo ambalo huwafanya akinamama wengi kuamua kujifungulia kwa wakunga wa jadi ambao baadhi yao hawakupata mafunzo ya kutoa huduma za uzazi; utoaji wa mimba usio salama na kifafa cha mimba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuongeza jitihada katika kukabiliana na vifo vya akinamama na watoto vinavyotokana na changamoto zinazojitokeza katika sekta hii ya afya ya mama na mtoto, ni vyema Serikali ikachukua hatua zifuatazo:-

(i) Kuhamasisha jamii itoe taarifa kuhusu ubora wa huduma za afya kwa mamlaka ya Serikali za Mitaa ikiwa ni pamoja na kueleza hali ya upatikanaji wa wataalam wa afya na hali ya matibabu;

(ii) Kusaidia katika kujenga uwezo wa mfumo wa afya wa wilaya ili kuwezesha katika utoaji na usimamiaji wa huduma bora za afya ya uzazi, ikiwa ni pamoja na uzuiaji wa maambukizo ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto;

(iii) Wizara ihakikishe kunakuwa na dawa za kutosha kwa ajili ya kuzuia maambukizi ya VVU kwa akinamama wajawazito ili kusaidia katika kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa watoto kwa lengo la kuwezesha watoto wengi zaidi kuzaliwa wakiwa salama;

(iv) Kuhamasisha jamii na familia kuunga mkono wanawake na kuwawezesha kuwa na kauli katika masuala yanayohusu huduma zao za afya; na

(v) Serikali kwa kushirikiana na vyombo vya habari itetee kwa nguvu ongezeko la uwekezaji katika huduma za afya ya wanawake katika ngazi ya Taifa na ya Serikali za Mitaa kwa kutumia vielelezo vinavyoonesha maafa na athari ya vifo vya wanawake vinavyotokana na uzazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kampeni ya kuzuia maambukizi ya virusi vya UKIMWI toka kwa akinamama kwenda kwa watoto. Tanzania ikiwa ni miongoni mwa nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara imekuwa katika vita dhidi ya maambukizi mapya ya Virusi vya UKIMWI hasa upande wa maambukizi ya UKIMWI toka kwa mama kwenda kwa mtoto. Takwimu zinaonesha kuwa idadi ya watoto walio chini ya umri wa miaka mitano ambao wanakufa kutokana na maambukizi ya virusi vya UKIMWI kutoka kwa mama zao ni kubwa. Serikali inapaswa kufanya jitihada kubwa za kuhakikisha inaokoa maisha ya watoto hawa ambao ndiyo nguvu kazi ya Taifa la kesho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha jitihada hizi zinafanikiwa, ni vyema Serikali ikahakikisha kuwa:-

(i) Inatoa programu nyingi za uzuiaji wa maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto (na kinga nyingine) zikiwemo programu za kuwasaidia wanawake kuwa na afya kwa muda mrefu kwa msaada wa lishe na matibabu;

(ii) Kutoa mafunzo kwa wanasihi wengi, wafanyakazi wa jamii wa kujitolea na wakunga wa jadi ili kuwafikia wanawake wengi na taarifa za kuaminika na ushauri kuhusu mambo ya kufanya wanapokuwa na maambukizi ya VVU. Wanawake wanaoishi na VVU wanahitaji kujua nini cha kufanya, kwa mfano, kuepuka mimba zisizotakiwa na hatari zinazoweza kutokea kwa watoto wachanga kutokana na lishe duni na maambukizi yanayohusiana na ulishaji mbadala; na

(iii) Kuboresha hali ya huduma za afya ili kuhakikisha kuwa watoto wachanga hawaambukizwi wakati wa kuzaliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.