Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Hamoud Abuu Jumaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nichukue fursa hii ya kipekee kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia kuwepo mahali hapa. Vilevile ninamshukuru Mungu kwa kunipa nguvu na nafasi hii na mimi nichangie hotuba hii ya bajeti ya mwaka 2017/2018 ambayo inagusa moja kwa moja maisha ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawapongeza Mawaziri pamoja na wataalam wao kwa kuandaa bajeti nzuri yenye kukidhi mahitaji na kutatua kero zilizopo katika sekta nzima ya afya. Bajeti hii inatekeleza Ilani ya chama tawala, Chama cha Mapinduzi. Katika misingi hiyo ilani yetu imezungumzia utekelezaji wa sekta ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niipongeze Serikali kwa juhudi zake za dhati kabisa katika kuhakikisha huduma za afya zinapatikana kila eneo la nchi yetu, pia kuhakikisha maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto yanazingatiwa kwa mujibu wa sheria zetu na taratibu zilizopo. Kwenye kila jambo lolote la kimaendeleo halikosi changamoto na changamoto hizo yatupasa Serikali kuzichukua kama fursa katika kuhakikisha zinatatuliwa na kuboresha huduma kwa manufaa ya wananchi wetu. Bado tumekuwa na matatizo ya upungufu wa wahudumu wa afya katika zahanati zetu hasa maeneo ya vijijini. Mapungufu haya yamekuwa yakileta kero kwa wananchi wetu kwa kukosa huduma kwa wakati. Kumekuwa pia na upungufu wa madaktari ilhali tunao madaktari wengi waliomaliza vyuo na kufaulu vizuri lakini hawana kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali iajiri watumishi hawa kwa wingi ili waende katika maeneo mbalimbali kuhudumia wananchi. Nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuwapa ajira madaktari takribani 250 ingawa Wizara hii imesema haina fedha za kuwalipa mishahara, lakini Rais kafanya uthubutu ili wataalam hawa waende kuwahudumia


wananchi. Naishauri Wizara kuchukua hatua madhubuti na kutafuta vyanzo vya fedha ili iweze kuajiri wataalam wa afya wengine. Kufanya hivyo kutasaidia sana kumaliza tatizo hili la muda mrefu la upungufu wa wataalam hawa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sawasawa na hilo, Wizara iweke mkakati wa kujenga nyumba za wataalam wa afya hasa vijijini, mfano katika Jimbo langu la Kibaha Vijijini tuna changamoto kubwa sana ya uhaba wa nyumba za watumishi wa afya na imekuwa kawaida kwa watumishi hawa wakipangiwa kuja katika maeneo ya kwetu, hufika kuripoti na punde wakigundua mazingira siyo rafiki, kwa maana hakuna nyumba basi huondoka kwa kusema wanaenda kuhamisha vitu watarudi, lakini hawatokei tena. Hali hii inarudisha nyuma juhudi tunazochukua kama viongozi katika kujitolea huku Serikali ikilalamika kila siku haina fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya vijijini ndiyo kumeonekana kuna changamoto kubwa ya ukosefu wa nyumba, nafikiri watumishi hawa wanastahili kabisa kukaa sehemu nzuri, Wizara lazima iwe na mkakati wa kujenga nyumba za watumishi hawa wa afya ili kwao iwe motisha na kutoa huduma kwa mazingira yaliyo bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo ninaishauri Serikali ihakikishe inaongeza kujenga vituo vya afya ili kuepusha wananchi kutembea umbali mrefu kufuata vituo hivyo vya afya, kwani vimekuwa vikisababisha vifo vya watoto wakati wa kujifungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa Jimboni kwangu Kibaha Vijijini tumetenga kabisa maeneo ya kujenga vituo hivi, hivyo katika bajeti hii naomba Wizara kupitia Serikali kumaliza changamoto hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la watoto kuzagaa mitaani nimelisema sana humu Bungeni katika nyakati tofauti na changamoto hii bado ipo. Wizara hii ndiyo wahusika wakuu wa kuchukua hatua na kuhakikisha watoto wote wanakuwa katika vituo maalum siyo kuzagaa mitaani


kuomba omba. Hata hivyo naishauri Serikali kuwachukulia hatua baadhi ya wazazi wa watoto hawa ambao wao ndio wamekuwa wakiwatuma kwenda kuomba na wao wazazi kukaa pembeni. Ni jambo la aibu sana kwa nchi yetu kwani mambo haya yameshapitwa na wakati katika dunia ya leo.

Napenda kugusia pia suala la wazee, natambua uwepo wa vituo vya wazee maeneo mbalimbali hapa nchini, vituo hivi vimekuwa havitengewi bajeti ya kutosha na Serikali na zaidi vituo hivi vimekuwa vikitegemea misaada kutoka kwa jamii. Nafikiri ni wakati sasa Serikali ikachukua hatua kwa kutenga fedha mahsusi kwa ajili ya vituo vyote vya kulelea watoto na wazee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika awamu zote nilizokuwepo humu Bungeni, nimekuwa nikilisemea hili la Kituo cha Afya Mlandizi kupandishwa hadhi, sifa na vigezo tunavyo, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne na Awamu hii ya Tano walitoa ahadi ya kukipandisha hadhi kituo hiki na kuwa hospitali, lakini Awamu ya Nne imepita bila kituo hiki kupandishwa hadhi, sasa tuko Awamu ya Tano naomba ahadi hii itekelezwe, kwani Mheshimiwa Rais akitoa ahadi kinachofuata ni utekelezaji kwa mamlaka husika. Hivyo mimi na wananchi wangu tunashukuru sana katika bajeti hii maombi yetu ya muda mrefu na ahadi za Marais wawili zikitekelezwa.

Mimi kama Mbunge najitahidi sana kujitoa kwa hali na mali katika kuhakikisha majengo na vifaa mbalimbali vinapatikana katika vituo vyetu vya afya, kama sasa kuna ujenzi wa ukuta kwa maana uzio katika kituo cha afya Mlandizi na hizi ni juhudi zangu kama Mbunge, hivyo Serikali ikituunga mkono katika mambo mazuri kama haya basi na sisi viongozi pamoja na wananchi tunafarijika sana na kupata moyo wa kuzidi kujitolea.

Hata hivyo nimeona bajeti ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba imeongezeka kutoka shilingi bilioni 31 mwaka 2015/ 2016 hadi shilingi bilioni 251 mwaka 2016/2017, ni jambo jema na la kupongezwa ila rai yangu kwa Serikali ni mamlaka husika


kumekuwa na changamoto za upungufu wa dawa katika vituo vyetu vya afya, zaidi dawa kuchelewa kufika kwa wakati. Naamini kwa ongezeko la bajeti basi changamoto hizo hazitakuwepo tena na kuleta nafuu kwa wananchi kupata dawa kwa wakati na kuwaondolea usumbufu wa kukosa dawa pindi wanapoandikiwa dawa hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.