Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Yussuf Haji Khamis

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua fursa hii muhimu na adhimu kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema ya uhai na uzima. Nikushukuru wewe Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuniruhusu na mimi nichangie ingawa kwa ufupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapambano ya UKIMWI pamoja na kuendelea ndani ya nchi yetu lakini inaonekana bado UKIMWI unaongezeka pamoja na maambukizi mapya. Kama juhudi za makusudi hazitochukuliwa basi Taifa letu litafika pabaya sana. Kwa hivi sasa UKIMWI umekuwa uko sirini sana kiasi ambacho watu wengi wamekuwa na matumaini makubwa kwamba UKIMWI umepungua kwa style za watu zilivyo. Watu ambao wanaishi na virusi vya UKIMWI si rahisi kuwatambua kama hajajieleza mwenyewe. Hii inatokana na kuitikia wito wa kujiunga na vituo vya dawa za ARV, kwa hiyo watu wengi kwa kupungua athari za kuonekana moja kwa moja wanadhani kuwa UKIMWI umepungua.

Kwa hiyo, ushauri wangu ni kwamba mkakati na juhudi ziendelee kuelimisha Watanzania kwamba UKIMWI upo na bado unaua. Wataalam wa UKIMWI wametoa taarifa kwamba Mkoa wa Njombe unaongoza kwa UKIMWI ambao una asilimia 14.8, hii ni asilimia kubwa na ya kutisha. Naomba Serikali ifanye utafiti ni jambo gani linalosababisha maambukizi makubwa kiasi hiki katika mkoa huu. Tatizo lijulikane na itolewe elimu ya uhakika ili kuondoa tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nazungumzia suala la wazee. Tunafahamu fika kwamba wazee wa sasa ndio vijana wa juzi na wa jana ambao walijituma kwa utumishi uliotukuka na mafanikio ya utumishi wao mwema ndio uliolifikisha Taifa letu hapa lilipo. Hivyo nashauri Serikali kutowasahau na kuwadharau wazee ambao ndio waliokuwa dira ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kusikitisha ni kwamba wazee hawapati huduma inavyopaswa na badala yake wazee wanaonekana kama hawakuwa na mchango wowote katika Taifa hili. Kwa mfano katika huduma za matibabu wazee wamekuwa wakisumbuka kana kwamba hawastahili kupatiwa huduma hii, wamekuwa wakitozwa malipo makubwa ambayo hawamudu lakini ni haki ambayo imeidhinishwa na Serikali kupatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kuliwekea kipaumbele suala la kuwajali wazee kwa kufuatilia huduma zinazostahiki kwao Serikali ina nia na dhamira thabiti juu ya wazee inaonekana changamoto hii inayowakumba ni utendaji mbovu usiojali mchango wa wazee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia hoja yangu napenda kugusia angalau kidogo suala la mazoezi ya viungo kwa jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mazoezi ni jambo muhimu sana kwa afya ya mwanadamu na michezo ni sehemu ya mazoezi. Kwa hiyo, michezo ni muhimu sana kwa maendeleo ya jamii na kiuchumi na hasa katika kuimarisha miili yetu kiafya na kuwa wakakamavu. Sasa hivi nchi yetu imekumbwa na magonjwa mengi sana ambayo kama tungekuwa makini tusingeathiriwa sana na magonjwa haya, mfano wa magonjwa hayo ni kama vile kisukari, moyo na kadhalika. Magonjwa haya kwa ujumla wake yanaitwa magonjwa sugu na yanayogharimu fedha nyingi za wananchi na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali na Wizara ya Afya kuhamasisha jamii na suala zima la kufanya mazoezi na kutoa misaada pale inapobidi ili kuendeleza mazoezi.