Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza, nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu na timu yake nzima kwa kazi na juhudi kubwa wanayofanya kuleta maendeleo ndani ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimpongeze Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuchagua timu nzuri, timu ya hapa ni kazi tu, wametuonesha kwa vitendo kasi yao mpaka wengine tunafikiria tunafanyaje na sisi twende na kasi hiyo. Wenzetu wameanza kufikiria na imebidi watoke hapa ndani waende wakajipange huko nje ili na wao waweze kwenda na kasi hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze katika maeneo machache. Serikali imedhamiria kuleta maendeleo kwa kasi kubwa. Zile sekta ambazo imeahidi kwamba zitafanyiwa kazi, moja ni sekta ya kilimo tujikite vizuri, bajeti ya kilimo ambayo tutakuja kupitisha hapa wote tuiangalie vizuri iweze kufikia katika lile lengo tulilojiwekea la Maputo Declaration la asilimia kumi. Asilimia kubwa ya wananchi wetu ndiyo wapo huko vijijini na tukitenga bajeti kubwa kwenye sekta hii ya kilimo mambo mengi yatawezekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia Wabunge wote tuunge mkono hoja ya kuongeza fedha ya kutosha katika mambo ya research and development. Bila utafiti hatutaweza kwenda mbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, na-declare interest, nipo kwenye Kamati ya Bajeti, katika hoja za awali tumeona fedha zilizotengwa upande wa utafiti ni ndogo sana, ni vizuri tujipange. Bila utafiti wetu wa ndani ya nchi iwe kwenye kilimo, mifugo, afya au jambo lolote hatutaweza kusonga mbele. Naomba Serikali kwa upande wa utafiti tuwekeze fedha ya kutosha ili tuweze kusonga mbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia upande wa pili ni kwenye masuala ya mazingira. Tumebaki kusemea tu mambo ya mazingira kama jambo la kawaida, tunalisema linapita, hakuna mpango thabiti. Ni lazima Mfuko huu wa Mazingira tuufanyie kazi. Mfuko upo kisheria ni vizuri tuhakikishe kwamba unapatiwa vyanzo vya uhakika vya mapato ili tuweze kwenda kuboresha mazingira yetu. Hali hii ambayo tunakwenda nayo kwa sasa hivi kutokana na tabia nchi ni vizuri tuwekeze pia kwenye masuala ya mazingira la sivyo sisi kila siku tutakuwa watu wa kuangalia Mfuko wa Maafa kujazia badala ya kuangalia kutibu. Bora kinga kuliko tiba na namna ya kukinga ni kuwekeza kwenye masuala ya mazingira. Kwa hiyo, naomba tujitahidi sana kuwekeza katika masuala yanayohusu mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, muhimu zaidi niishauri Serikali juu ya coordination baina ya Wizara moja na nyingine. Mwanzo ni mzuri lakini bado jitihada kubwa inatakiwa baina ya Wizara moja na nyingine coordination ile iwepo zaidi. Wasiwe kama wanashindana, wote mnakwenda kujenga nyumba moja, msishindanie fito. Kwa hiyo, mjitahidi coordination baina ya Wizara mbalimbali iwe ya uhakika na iwe lazima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi naomba katika Mkoa wa Manyara, wilaya zote masuala ya miundombinu yawekewe mikakati. Hii Mifuko yote ambayo tumeiunda tuhakikishe kwamba zile fedha mahali ambapo tumelenga ziweze kwenda. Mimi nishukuru kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu umepunguziwa kazi ya TAMISEMI sasa imepelekwa Ofisi ya Rais. Utakuwa na muda wa kutosha na ni muafaka sasa kuhakikisha unasimamia Wizara nyingine zote na kufanya kazi ya kutembea katika wilaya na mikoa yetu kuhakikisha kwamba kazi inakwenda vizuri, uratibu wako sasa utakuwa wa uhakika zaidi. Badala ya kuwa mezani na ofisini sasa utaweza kutembea na kutoa maamuzi wakati unafanya ziara zako.
Mheshimiwa Mwenyekiti, muhimu naomba Wabunge wote tuunge mkono suala la nishati na maji na hapo hapo tukiunganisha na suala la Mfuko wa Mazingira na utafiti. Bei ya mafuta iliposhuka duniani, leo bei ya mafuta ya jumla kwa diesel ni Sh.1,500. Napendekeza tuipandishe bei mpaka ifike Sh.1,700 ili ile Sh.200 inayopatikana iende kwenye Mfuko wa Maji, Umeme Vijijini pamoja na Mazingira na utafiti ili ile fedha iweze kupeleka nishati, maji na masuala ya mazingira na utafiti kwa haraka zaidi. Baada ya bei kuteremka hakuna Mtanzania aliyenufaika, hakuna nauli iliyoshuka, hakuna bidhaa yoyote iliyoshuka isipokuwa wafanyabiashara wachache wameendelea kupata ile faida kubwa na ile faida hata kodi yake hawalipi kwamba Serikali inapata kodi kutokana na suala hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Wizara ya Fedha pamoja na Mawaziri wa Maji, Mazingira, Nishati na Elimu waangalie Wizara zao zinapokuja kuleta bajeti basi fedha hizo zitumike kuongeza Mfuko wa Mazingira, Mfuko wa Maji na Mfuko huo wa Nishati na utafiti ili kasi ya maendeleo iweze kwenda huko vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi bado ni muumini wa maendeleo vijijini zaidi kwa sababu huko vijijini ukiboresha huduma mbalimbali, iwe ya maji, elimu, afya basi wananchi hawatakuwa na hamu ya kuhamia mijini na pia huku mijini tayari kuna maendeleo makubwa. Kwa hiyo, Serikali ijikite zaidi kupeleka maendeleo katika sehemu mbalimbali huko vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, nimshukuru Mheshimiwa Lukuvi, nimshukuru Mheshimiwa Mwigulu na Waziri wa Maliasili, Wilaya ya Babati ina matatizo makubwa sana ya ardhi. Tatizo hilo likiisha basi Wilaya ya Babati na Mkoa wa Manyara unaweza kuwa moja katika mikoa ya mfano ambapo maendeleo yatakuwa kwa kasi sehemu kubwa. Tunaomba mjitahidi, tunaomba ushirikiano wenu ili tuweze kumaliza migogoro hii ambayo imedumu kwa muda mrefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niendelee kusisitiza kwamba kuna haja kubwa sasa, wenzangu pia walichangia kuhusu suala la kuunganisha utawala kuanzia juu kwenda chini, hii D by D, kwa sasa chain ile kuna mahali inakatika.
Ni vizuri tujaribu kuangalia upya sera namna ya kuunganisha hiyo chain ili maendeleo yakipangwa kuanzia ngazi ya chini kuja huku juu basi yaweze kwenda kwa kasi tunayoitarajia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niendelee kushukuru na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.