Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Abdallah Haji Ali

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kiwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. ABDALLAH HAJI ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa mambo yote. Pili, nakupongeza wewe binafsi kwa usimamizi mzuri wa shughuli za Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na mchango wangu katika hoja hii ya Wizara ya Afya ni kwamba kumekuwa na malalamiko ya muda mrefu dhidi ya Wizara hii kutoka kwa wananchi. Wizara ya Afya ndiyo Wizara mama inayoratibu ustawi wa afya za watu nchi nzima, na la kukumbuka ni kwamba afya ndiyo mambo yote, pasipo afya miongoni mwa wananchi hapana Taifa endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, malalamiko yapo zaidi juu ya upatikanaji wa dawa, vifaa tiba kama mashine za x–ray, vitanda na mambo mengine. Kutokana na upungufu wa mambo haya jamii inawaangalia zaidi Waziri na watendaji wake kwamba ndio wanaohusika kukidhi mambo haya ikiwemo upatikanaji wa madaktari, wauguzi na hata magari ya wagonjwa. Mheshimiwa Waziri na watendaji wake wana nia nzuri juu ya ufanisi wa mambo haya ila wamekuwa wakikwamishwa na ukomo wa bajeti na kutokupatikana kwa kile pia ambacho kimetengwa kwa ajili ya ununuzi wa vifaa hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali ili kuliweka Taifa katika hali nzuri kiafya, Serikali isilifumbie macho suala la upatikanaji wa dawa na vifaa tiba. Serikali izishughulikie changamoto hizi kwa kuipa upendeleo Wizara ya Afya kwa kuitengea fungu la kutosha litakalokidhi upatikanaji wa vifaa, dawa na madaktari ili kukidhi huduma za afya za Watanzania.

Naishauri sana Serikali kutumia vyema kodi za wananchi kwa kuziondoa changamoto za huduma za afya katika ngazi zote ili kuondoa malalamiko ya wananchi ambao ndio msingi wa Taifa. Ni imani yangu kwamba Serikali baada ya maombi mengi ya Waheshimiwa Wabunge mbalimbali itatenga pesa za kutosha na kuzipeleka zinakohusika kwa wakati na kufanya ufuatiliaji ili kuhakikisha kwamba haya yanatimizwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie suala la haki za watoto. Watoto wana haki zao za msingi kutoka kwa wazazi, ndugu, jamaa na Serikali kwa ujumla. Usimamizi huu ni jukumu la Serikali na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Jukumu hili limekuwa ni kikwazo hususan kwa wazazi kukosa elimu au uelewa juu ya haki za mtoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na idadi kubwa ya watoto wanaokoseshwa haki zao za msingi kwa kukoseshwa elimu na badala yake kufanyishwa kazi zisizowahusu, watu wanafikiri kwamba ajira ya watoto ni sehemu ya maisha yao. Kuna idadi kubwa ya watoto chini ya umri wa miaka 18 wanaofanyishwa kazi za ndani wakikoseshwa elimu ambayo ndiyo wajibu wao kwa sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali izidi kukemea masuala ya ajira za watoto hasa za kuajiriwa majumbani kwa kazi za mapishi, usafi na uangalizi wa watoto. Pia Serikali iweze kufanya sensa nchi nzima kuwatambua watoto wote wanaotumikishwa kinyume cha sheria na haki za mtoto na kuweza kudhibitiwa kwa wale wote wenye tabia ya kuwatumikisha watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu zinaonesha Tanzania ina waathirika wa HIV 1,538,382. Watanzania tuko zaidi ya milioni 50, haya ni makisio ya hivi karibuni, je, ni utaratibu gani utumikao kuwapima watu na kupata takwimu za uhakika? Ni dhahiri kwamba idadi kubwa haijafikiwa ili kupata takwimu inayowiana na idadi ya Watanzania, hivyo naishauri Serikali kuzidi kutoa elimu juu ya watu kuweza kupima kwa hiari ili kupata takwimu halisi za watu wanaoishi na HIV.