Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Afya, Maendeoe ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa hotuba nzuri ya Bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2017/ 2018. Pia napenda kumpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri na wataalam wote wa Wizara hiyo kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuhakikisha kwamba kila Mtanzania anapata huduma hiyo stahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mwongozo wake imara kwa nchi yetu hasa katika kuimarisha huduma za afya na ustawi wa jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pia napenda kumpongeza Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uongozi wao mzuri na kusimamia Ilani ya Uchaguzi ya CCM na hasa katika masuala ya afya na ustawi wa jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania wote tunatambua umuhimu mkubwa na wa mwanzo kabisa wa afya ya wananchi wetu. Afya ni suala la msingi katika ustawi na hata uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na umuhimu wa afya kwa kila Mtanzania inabidi Serikali kuangalia namna mbadala za kuhakikisha kila Mtanzania anapata huduma bora ya afya. Katika ukurasa wa 65 na 66 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Afya ameeleza kuwa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) una wanachama 792,987 hadi kufikia Machi 2017; vilevile idadi ya wanufaika ni 3,880,088 hadi kufika Machi 2017. Kwa upande wa Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) ulikuwa na kaya 1,595,651 na wanufaika wa CHF walikuwa 9,573,906

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufikia Machi 2017, Mifuko ya Bima ya Afya ya NHIF ilikuwa na wanachama (kaya) 2,388,638 zenye wanachama 13,453,994 tu. Hii ni sawa na asilimia 38 ya Watanzania wengi hasa wa vijijini wanaoendelea kukosa huduma ya afya kwa ukosefu wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya uzinduzi wa bodi mpya mwaka 2016 ya Wakurugenzi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Waziri wa Afya alisema mkakati wa Serikali ni kufikisha huduma ya bima ya afya zaidi ya asilimia 50 kwa Watanzania wote ifikapo mwaka 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza muswada huo wa bima ya afya uwasilishwe mapema iwezekanavyo ili Watanzania wengi zaidi wajiunge na bima ya afya na mazingira ya muswada yepelekee ulazima wa kila kaya kuwa na bima ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutafikia kaya 15,000,000 kwa malipo ya shilingi 30,000 kwa mwaka kwa kila kaya, mfuko utakusanya shilingi bilioni 450 kwa mwaka. Makusanyo hayo kwa mwaka yatawezesha mfuko kutoa huduma bora zaidi kwa Watanzania wengi na wanaweza
hata kukopesha Halmashauri kujenga zahanati na vituo vya afya nchi nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuongezeka kwa vituo vya afya na zahanati kutachochea ongezeko kubwa la wanachama na pia mapato makubwa kwa mfuko. Kwa mkakati huu wa kuboresha bima ya afya si tu itaboresha huduma za afya, lakini itapunguza kwa kiasi kikubwa bajeti ya Wizara ya Afya na hata TAMISEMI kutegemea mfuko wa Hazina unaotokana na kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.