Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie katika hoja hii iliyo mbele yetu. Kwanza kabisa ningependa kuzungumzia ujenzi wa Hospitali ya Serikali ya Wilaya ya Rombo. Wilaya ya Rombo ni Wilaya Kongwe lakini katika umri wake wote haijawahi kuwa na Hospitali ya Wilaya. Hospitali ambayo tunatumia ni Hospitali ya Huruma ambayo Meneja wake ni Askofu wa Kanisa Katoliki, Jimbo la Moshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali inayojengwa sasa hivi katika Kituo cha Afya Karume tumejitahidi, tayari tumekamilisha wodi zote tuna Theater tuna Mochwari lakini tunasumbuliwa na fedha za kumalizia jengo la OPD. Ujenzi umeshaanza, msingi umeshakamilika, lakini sasa hivi mkandarasi amesimama kwa sababu tumeshindwa kumlipa. Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI alitembelea jengo hili na alitoa ahadi kutusaidia. Nataka tu ku-register maombi haya pia kwa Wizara ambayo ndiyo inasimamia sera, mtusaidie ili jengo hili liweze kumalizika tuweze kuwa na hospitali ambayo itasaidia kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Hospitali ya Huruma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambasamba na hilo ningepeda kuzungumzia hitaji la watumishi kama wenzangu walivyozungumza. Tuna matatizo makubwa sana ya watumishi katika sekta ya afya kwenye Jimbo la Rombo, kuanzia Madaktari, Manesi na watumishi wengine. Wananchi
wa Rombo wamejitahidi sana kwa nguvu zao kujenga zahanati katika vijiji mbalimbali, lakini sasa ujenzi wa zahanati hizi ambazo nyingine zimekamilika na nyingine zinaendelea na ujenzi, tunapata shida kwa sababu tunawahamasisha wajenge, lakini hakuna wataalam. Kwa hiyo, ningemwomba dada yangu Ummy atakapopata fursa pamoja na Mheshimiwa Waziri wa Utumishi kwa ajili ya kuwaajiri watumishi wa sekta ya afya atukumbuke Jimbo la Rombo kwa ajili ya Madaktari na Manesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa pia kuzungumzia Chuo cha Maendeleo ya Jamii cha Mamtukuna, Mheshimiwa dada yangu Ummy alifika pale anakifahamu kile chuo, tunahitaji kubwa sana la watumishi Walimu na bajeti yake ni ndogo na kile Chuo kinasaidia sana. Tunaomba sana kama Wizara wanaweza wakaendelea kukitunza na kukiangalia kile chuo ili kuweza kufanya kazi iliyokusudiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ningependa kuzungumzia ujenzi wa jengo kwa ajili ya vifaa vya kansa pale Hospitali ya KCMC. Jitihada zimefanywa na wafadhili, jitihada zimefanywa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri, kwa ajili ya kuhakikisha kumekuwa na kituo ambacho kitasaidia pia kupunguza msongamano katika Taasisi ya Kansa ya Ocean Road.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana fedha ambazo zinahitajika kwa ajili ya lile jengo ni kama bilioni sita hivi, ambazo kwa kweli kwa hapo tulipofikia KCMC ina mzigo mkubwa sana na vifaa vimeshapatikana. Kwa hiyo ningeiomba Serikali, tusiache hivi vifaa mwishoni wafadhili wavitumie kwa namna nyingine, tungeomba sana muwasaidie jengo hili liweze kukamilika ili taasisi ile iweze kusaidia Taasisi ya Kansa ya Ocean road ili wananchi wenye matatizo ya kansa ambao sasa hivi ni wengi waweze kupata nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matatizo ambayo yameendelea kuzungumzwa ya unyanyasaji wa watoto, wazee na kadhalika, ningeomba sana Wizara iweke msisitizo kwa sababu hili na lenyewe ni tatizo ambalo ni cross cutting, liko karibu katika kila eneo. Ni kweli watoto wanadhalilishwa, ni ukweli kuna watu ambao wakishafanya mambo kama haya wanaachwa mitaani kiholela. Ningeomba sana Wizara iweke msisitizo katika jambo hili ili watoto wetu wawe salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, hayo ndiyo nilikuwa nayo.