Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Dr. Christine Gabriel Ishengoma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nawapongeza Mawaziri wote kwa kazi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naanza na Benki ya Wanawake Morogoro. Naomba kituo cha Benki ya Wanawake Morogoro kama tulivyoongea na Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, hospitali ya Wilaya ya Morogoro ni muda mrefu mimi na Mbunge wa Jimbo tulikuwa tunaongelea hii hospitali ni lini itaanza kujengwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu hospitali ya Ifakara Kibaoni, hospitali ya Ifakara Kibaoni inatumika kama ya Wilaya, lakini kuna watoto njiti (pre mature) ambao hawana chumba cha watoto njiti, wanalazwa pamoja na watoto wengine ambao mama zao wametoka kujifungua, pamoja na wale wanaoumwa. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri aweze kuona kama tunaweza kupata chumba cha watoto hawa njiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Mkoa ya Rufaa ya Morogoro hatuna X-ray, X-ray iliyopo ni mbovu. Hili jambo lilishaongelewa tulikuwa tunaomba X-ray. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia kuongelea Hospitali ya Ulanga. Hospitali ya Ulanga wodi zao ni mbovu, kwa hiyo naomba iweze kuangaliwa. Hospitali ya Ulanga tuna X-ray pamoja na Utrasound lakini hatuna wataalam. Mheshimiwa Waziri naomba anisikilize, hatuna wataalam wa Hospitali ya Ulanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu lishe. Kwa upande wa lishe vyuo vikuu na vyuo vingine vinaendelea kutoa elimu ya akinamama lishe (nutrion officers). Naomba hawa nao muwatumie badala ya kutumia tu vidonge vya vitamin A. Wataalam hawa wa lishe nao pia watumieni kwa kuwaajiri kwa kusaidiana pamoja na TAMISEMI mpaka huko wilayani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Maendeleo ya Jamii. Ni kweli maendeleo ya jamii yameachwa nyuma, Mheshimiwa Waziri amekazia sana kwenye mambo ya afya lakini Sekta ya Maendeleo ya Jamii ameisahau, naomba aiangalie. Vile vile na wataalam wa maendeleo ya jamii waajiriwe mpaka vijijini kwani wenyewe ndio wanaosukuma maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria ya Ndoa; naomba sana hii Sheria ya Ndoa, kama wenzangu walivyosema, iletwe humu Bungeni na kufanyiwa kazi kwa sababu ya kumsaidia mtoto wa kike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bima ya Afya. Hadi kufikia Marchi ni asilimia 28 tu ndio wanaotumia Bima za Afya kama Mheshimiwa Waziri alivyosoma hotuba yake. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri aje na mkakati atafanyaje kusudi watu wote, wanawake, wanaume na vijana waweze kujiunga na Bima ya Afya kama ilivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatana na ilani ya Chama chetu cha Mapinduzi kila kata ni lazima iwe na kituo cha afya na kila kijiji lazima kiwe na zahanati na kila Wilaya lazima iwe na Hospitali. Namwomba Mheshimiwa Waziri tutekeleze hii ahadi ambayo ipo kwenye Ilani ya Chama cha
Mapinduzi kusudi tuweze kutimiza na aanze kutuambia na ni vipi atafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho wa yote naomba kuongelea jukwaa la wanawake. Namshukuru Mheshimiwa Makamu wa Rais kwa kuanzisha Jukwaa la Wanawake. Jukwaa la Wanawake la kiuchumi ni jukwaa zuri, ambalo linaunganisha wanawake wote ambapo wanabadilishana mawazo na wanaweza kupata jinsi ya kukopa kutoka kwenye taasisi zote za kukopa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na Mwenyezi Mungu akubariki. Naunga mkono hoja.