Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Amina Nassoro Makilagi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na hizi dakika za Mgimwa najua utanipatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba nikushukuru wewe na nimshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa yote aliyenipa nafasi ya kuweza kusimama na kutoa mchango wangu katika sekta hii muhimu ya Wizara ya Afya na Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuunga mkono hoja na sababu zangu ni mbili zifuatazo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, hotuba imeandaliwa vizuri sana, pili, dhamira ya Serikali chini ya Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Mawaziri na watendaji wote wa Serikali hasa katika sekta hii ya afya na maendeleo ya jamii kwa kweli wamejipanga. Wanaonesha kabisa dhamira nzuri ya kuhakikisha Watanzania wanakuwa na afya bora. Kwa msingi huo naunga mkono kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nitoe ushauri kwamba kwa kuwa Wizara imejipanga vizuri na kwa sababu changamoto za Wizara ya Afya na changamoto za Wizara ya Maendeleo ya Jamii ni kubwa, nimefurahi leo nimemuona Waziri wa Fedha yupo hapa, ninaomba Serikali ipeleke fedha katika Wizara hii kwa sababu bila afya hakuna kilimo, uchumi wala chochote katika Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ya Fedha ijitahidi kupeleka fedha kwenye sekta ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, nimejaribu kupitia kitabu hiki kila kitu inaonekana kama taasisi hii hakuna kitu. Taasisi hii ni mtambuka; bila Wizara ya Maendeleo ya Jamii kwa kweli hakuna chochote. Ninafurahi Waziri wa Fedha ananisikiliza na katika mwaka wa fedha ujao tunataka kuona sasa percent inaongezeka katika sekta hii ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe ushauri kwa Serikali iboreshe maslahi ya wafanyakazi katika sekta hii. Wanafanya kazi ngumu sana ma-nurse wetu, madaktari na watumishi wetu katika huduma za maendeleo ya jamii, bibi na bwana maendeleo ya jamii, lakini kwa bahati mbaya ni kundi ambalo wakati mwingine linasahaulika.

Nimefurahishwa na hotuba ya Rais juzi wakati wa Mei Mosi kwamba anakwenda kuboreshwa maslahi ya wafanyakazi. Naomba sekta hii ya afya hebu angalieni ma- nurse wetu wanavyofanya kazi kwa tija, angalieni madaktari wetu wanafanya kazi usiku na mchana, wanafanya kazi saa za ziada, hawana kupumzika wala kuchoka lakini zile stahili na posho zao hawazipati kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa Serikali ipeleke vifaa tiba kama ambavyo imeanza kununua dawa, ipeleke vifaa tiba katika vituo vya afya na ipeleke wataalam wa kutosha na hasa kutokana na hili sekeseke lililotokea juzi, watalaam sasa wamepungua katika taasisi zile. Naomba Serikali iwe makini ihakikishe hakuna kituo kinachopungukiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishauri kwenye ujenzi wa vituo vya afya. Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia wanawake wanafariki kwa kukosa huduma, watoto chini ya miaka mitano wanafariki. Ni ukweli usiopingika kwamba vituo vya ya ni vichache, tunaomba Serikali sasa ije na mkakati maalum na hapa naomba nitoe ushauri kwamba sasa Serikali kila Halmashauri tujenge kila mwaka vituo viwili, ukipiga mahesabu kwa Halmashauri tulizonazo 183, kama tutajenga vituo viwili, viwili kila mwaka na inawezekana, tutaweza kufika mbali; mara baada ya miaka mitatu tunaweza kuwa tumejenga vituo zaidi ya 1,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna vituo vya afya vipo ni maboma, vimejengwa hakuna mabaara, havijakamilika, nguvu za wananchi zimeishia pale. Ninaomba sana Wizara ya Fedha hebu tafuteni fedha zozote hata kama ni kwa mkopo, pelekeni ili hivi vituo vianze kwa sababu wananchi wamejikusanya wameishia pale kwa kushirikiana na Wabunge kupitia Mifuko ya Majimbo. Sasa Serikali ni jukumu lake kuhakikisha vituo hivi vinakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hii pia iweke utaratibu wa kuhakikisha inaongeza fedha katika maeneo mbalimbali na hasa katika Hospitali yetu ya Mkoa wa Mara. Ameongea Mheshimiwa Bonny Hospitali ya Rufaa ile ya Mkoa Mwalimu Nyerere Memorial Centre ni kituo ambacho kitakuwa ni ukombozi kwa watanzania na hasa wa Kanda ya Ziwa. Bugando sasa imeelemewa, tukipata kituo hiki na Serikali ikipeleka fedha za kutosha kila mwaka badala ya inavyofanya hivi sasa shilingi milioni 200 kila mwaka hakitakwisha leo.

Ninaomba Serikali ikiwezekana ipeleke hela kwa mkupuo shilingi bilioni 10 mwaka mwingine shilingi bilioni 10 ile hospitali ijengwe iwe ni ukombozi kwa hospitali za Kanda ya Ziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto wanaofariki kabla ya kufikisha miaka mitano. Ninashukuru jitihada za Serikali vifo vimepungua. Kuna tatizo la watoto wanaozaliwa njiti. nimejaribu kupitia kwenye hotuba ya Waziri sikuona eneo hili. Katika vifo vya watoto wanaofariki chini ya umri wa miaka mitano miongoni mwao ni watoto wanaofariki wakiwa njiti ni asilimia 40 na ni sehemu ya pili ya watoto wanaofariki. Ukiangalia takwimu kila siku watoto 100 wanafariki na kila mwaka watoto 9,000...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.