Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Grace Victor Tendega

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niweze kumshukuru Mwenyenzi Mungu aliyenijalia afya na pia niwashukuru sana wote waliochangia kuhusu Wizara hii ya Afya kwa sababu bila afya hatuna hiyo Tanzania ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninazungumza kwa huzuni sana kwa sababu bajeti ya Wizara hii kwa kipindi hiki ambacho tumebakiza muda mfupi sana haijatekelezeka kwa asilimia 60; japokuwa tuna Mawaziri ambao kwa kweli wanajitajidi kufanya kazi, lakini hawapati fedha za kutosheleza bajeti yao, na tunaona afya za Watanzania zinazidi kudorora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinga ni bora kuliko tiba, nilikuwa natengemea Mheshimiwa Waziri pia aje na jinsi ambavyo tutazungumzia jinsi ya kuwakinga Watanzania kutokupata maradhi mbalimbali, ukija ukaangalia katika maendeleo ya jamii ambako ndiko wako vijana wetu wafanyakazi ambao wanaweza wakaenda na wakawasaida Watanzania, bajeti yao ni ndogo na huko tunakotoka kwenye Halmashauri hawajaliwi, wako kama wanyonge ukiwakuta kule utawaonea huruma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri vijana wetu kule wananyanyasika hawako vizuri kabisa katika hii sector, ninaona kwa mfano, kuna masuala ya afya ya mazingira ambayo unaweza ukashirikiana na Wizara ya Mazingira, mkaanza kuona ni jinsi gani mnaweza kupunguza masuala ya maabukizi mbalimbali. Kwa mfano, Dar es Salaam asilimia 90 ni vyoo vya shimo, asilimia tisa tu ndiyo ina vyoo vya kuvuta, hizi ni takwimu ambazo zimetolewa na mashirika mbalilmbali waliopita na kufanya tafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa utaona kipindi cha masika jinsi ambavyo mtiririko wa maji taka unavyosambaa katika Jiji lile. Hii inakwenda kuleta maambukizo mbalimbali. Tunaambiwa kwamba Watanzania asilimia kubwa tuna kawaida ya kutonawa baada ya kwenda sehemu za kujisaidia na sehemu mbalimbali na hizi zinasababisha maradhi mbalimbali ambayo tunayapata na magonjwa mbalimbali. Kwa mfano, UTI ambao inafikia mahali sasa umekuwa ni ugonjwa wa kawaida lakini pia unaua. Mheshimiwa Waziri uweze kulitizama hilo na kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika makubaliano ya Abuja (Abuja Declaration) makubaliano yalikuwa asilimia 15 ya bajeti mzima inaweza kutatua changamoto za afya, lakini asilimia hii imekuwa haitolewi kwa muda wote wa bajeti. Ukianzia mwaka 2015/2016 zilitengwa shilingi trilioni nne zikaidhinishwa shilingi trilioni 1.5 tu. Ambayo ilikuwa ni asilimia saba hatukuweza kufikia hata hapo. Kwa hiyo, hii inaonesha jinsi ambavyo hatuwezi kutekeleza baadhi ya mipango ambayo tumeipanga ili iweze kutekelezeka kwa Watanzania wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nizungumzie suala hili la kutokupeleka fedha vizuri ambalo linaanzia ngazi ya sera tunavyotunga sera katika Wizara ya Afya tunakwenda katika mikoa, halmashauri mpaka vijijini, jinsi ambavyo mtiririko mzima unavyochanganya. Huu mchanganyiko wa kiutendaji katika Wizara hii unatuletea shida katika utekelezaji na ufuatiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kamati tumependekeza mara zote kwamba ingewezekana Wizara ya Afya kama ilivyo Wizara ya Elimu, kuwe na mtiririko kutoka sera mpaka utendaji wake. Unakuta katika Halmashauri baadhi ya masuala hayatekelezeki tunaambiwa hii iko TAMISEMI, hii iko Wizara ya Afya, basi unakuta ni mchanganyiko na fedha zinakuwa hazifuatiliwi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Waziri aweze kumshauri Rais jinsi juu ya Wizara hii nyeti ambayo itatengeneza Watanzania ambao wenye akili timamu na nzuri, wenye afya bora wa kuweza kuendeleza na kuleta maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Menyekiti, nizungumzie kule kwangu japokuwa kuna baadhi ya mambo ambayo yalitakiwa yazungumzwe kwa TAMISEMI, kwa sababu sikupata nafasi lakini pia kwa sera yakwenda. Kwa mfano, katika Halmashauri ya Wilaya ya Iringa waliomba shilingi milioni 150 waliidhinishiwa shilingi milioni 35 na hawakupata hata shilingi moja, unategemea hawa watafanyaje kazi zao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia OC ilikuwa ni shilingi milioni 25 badala yake wamepelekewa shilingi milioni sita tu. Ukija katika Halmashauri ya Kilolo kwanza Halmashauri ile ina upungufu wa watumishi asilimia 51, waliopo ni asilimia 49 na hao tumepata wenye vyeti fake 13 bado kuna upungufu wa watumishi katika Halmashauri hiyo ya Kilolo.
Kwa hiyo, katika mgawanyo wenu wa watumishi wa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja ya Kambi ya Upinzani.