Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kunipa uhai, nguvu, afya njema na akili timamu na kuniwezesha leo kuchangia hoja ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa kujibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kwa heshima kubwa kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na Viongozi wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uongozi wao mahiri. Hakika Watanzania kwa ujumla wetu tumefarijika na uongozi wao mahiri ambao unaonesha nia ya dhati ya kuiwezesha nchi yetu kupiga hatua kubwa kimaendeleo na kufikia kiwango cha uchumi wa kati. Nami naungana na Watanzania wenzangu kuendelea kuwaombea afya njema ili waweze kuendelea kututumikia kwa mapenzi makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kukupongeza wewe binafsi, Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti wengine wote wa Bunge kwa kuliongoza vyema Bunge letu Tukufu. Napenda pia kuwapongeza Mheshimiwa Salma Rashid Kikwete, Mheshimiwa Dkt. Gertrude Pangalile Rwakatare, Mheshimiwa Anne Kilango Malecela na Mheshimiwa Profesa Palamagamba Kabudi, Waziri wa Katiba na Sheria walioteuliwa na Mheshimiwa Rais kuungana nasi katika Bunge hili. Nina imani kwamba sasa sote tutatekeleza kazi zetu za kuwatumikia wananchi kufuatana na kauli mbiu ya Serikali ya Awamu ya Tano ya ‘Hapa Kazi Tu’ ili tufikie malengo yetu ya kujikwamua kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwashukuru kwa namna ya pekee wapiga kura wangu wa Wilaya ya Namtumbo, kwa namna wanavyojituma katika kuhakikisha kwamba kwa pamoja tunatatua changamoto zinazowakabili. Pamoja na kwamba muda mwingi sipo nao kutokana na majukumu ya Kitaifa, wanajua nawawakilisha kwa kiwango kikubwa katika kutatua changamoto zao. Nawaahidi tena kwamba mambo yote niliyoyaahidi na yaliyoahidiwa ndani ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi nitaendelea kuyasimamia yatekelezwe kadri Mwenyezi Mungu atakavyonijalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto zote za kilimo hususan kilimo cha tumbaku na mazao mchanganyiko pamoja na masoko ya uhakika, maji, umeme, mitandao ya simu, barabara, maeneo ya kilimo na mipaka ya kiutawala zinazowakabili wakazi wa Wilaya ya Namtumbo naendelea kuzishughulikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nishukuru familia yangu, mke wangu na watoto kwa kuniunga mkono, kunivumilia na kunitia nguvu katika kutekeleza dhamira yangu ya kuwatumikia wananchi wa Namtumbo na Watanzania wote katika nafasi hizi za Ubunge na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwashukuru Wabunge wote kwa namna mlivyochangia, maoni na mapendekezo yenu kwetu ni maelekezo. Naomba sasa ndugu zangu, Waheshimiwa Wabunge wote, tuunge mkono hoja hii ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano na naomba sasa nijielekeze katika kujibu hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge wamechangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanzia, Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu ameongelea kuhusu kutotolewa kwa fedha za ujenzi wa viwanja vya ndege vya Kigoma, Mpanda, Tabora, Songwe, Mtwara, Sumbawanga na Shinyanga na vilevile Msemaji wa Kambi Rasmi ya Upinzani naye ameongelea kutotolewa kwa fedha za ujenzi wa jengo la tatu la abiria JNIA Dar es Salaam na uwanja wa Songwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa viwanja vya ndege vya Kigoma, Tabora, Shinyanga, Mtwara na Sumbawanga, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba hadi kufikia Machi 2017, ujenzi wa viwanja vya ndege tajwa ulikuwa katika hatua ya manunuzi kwa hiyo hakuna fedha iliyotolewa kwa sababu bado hatujawapata wakandarasi wa kufanya kazi zinazotakiwa kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa ukarabati na upanuzi wa kiwanja cha ndege cha Mpanda kwa kiwango cha lami ulikamilika mwaka 2012 na katika mwaka 2016/ 2017, Serikali ilitenga jumla ya shilingi milioni 700 kwa ajili ya kulipa deni la Mkandarasi. Serikali itahakikisha kuwa deni hilo la Mkandarasi linalipwa mapema. Kazi zinazoendelea katika Kiwanja cha Ndege cha Songwe ni ujenzi wa jengo kubwa la abiria na mradi unaoendelea ambapo Mkandarasi amekwishalipwa shilingi bilioni 3.3 na hadi sasa hana deni lolote analoidai Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kiwanja cha ndege cha Mtwara, zabuni ya upanuzi na ukarabati wa kiwanja hicho imeshatangazwa na inatarajiwa kufunguliwa mwezi Mei, 2017.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya 2017/2018, Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kulipa fidia kwa viwanja vya Kigoma, Shinyanga, Sumbawanga, Iringa, Musoma, Msalato, Bukoba, Umkajunguti na JNIA. Kwa viwanja vilivyobaki Serikali itaendelea kulipa fidia kadri ya upatikanaji wa fedha. Mamlaka ya Viwanja vya Ndege imeweka mkakati wa kupima na kupatiwa hati miliki kwa viwanja vya ndege 15 Mwanza, Songwe, Msalato, Dodoma, Iringa, Kilwa Masoko, Mtwara, Lindi, Lake Manyara, Songea, Tabora na Shinyanga na kwa mwaka wa fedha 2017 hicho ndicho tutakachokifanya. Maombi ya kupimiwa na kupatiwa hati miliki yameshawasilishwa kwa mamlaka husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze katika hoja mbalimbali za barabara. Wabunge wengi sana wameongelea barabara na muda ulivyo siyo rahisi sana kuzieleza zote, nitachukua moja moja kadri muda utakavyoniruhusu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na barabara ya Tabora – Sikonge – Koga – Mpanda vilevile inaunganika na barabara ya Mbinga hadi Mbamba bay, barabara hizo zote ni lot moja, ni project moja inayofadhiliwa na Benki ya AFDB na fedha za ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami tayari zimeshapatikana kutoka Benki ya Maendeleo ya AFDB. Zabuni za ujenzi wa barabara hii zimetangazwa na taratibu za kukamilisha manunuzi ya Mkandarasi zinaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Kibondo – Kasulu – Mnanila, tunatarajia kupata rasimu ya usanifu wa kina na utayarishaji wa nyaraka za zabuni mwezi Juni, 2017 kwa ajili ya kutoa maoni kabla zabuni za ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Kibondo – Kasulu – Manyovu hazijatangazwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Masasi – Nachingwea – Nanganga umepangwa kuanza mwaka wa fedha 2017/2018. Aidha, kulingana na Ilani ya CCM ya mwaka 2015 ambayo ndiyo tunayoitekeleza, barabara za Nachingwea hadi Liwale na barabara ya Nangurukuru hadi Liwale zinatakiwa zifanyiwe upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa ajili ya kujengwa kwa kiwango cha lami. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge walioongelea hili ikiwa ni pamoja na Mheshimiwa Lathifah Hassan Chande kwamba barabara hii tutaifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina katika kipindi hiki cha miaka mitano kabla hakijakwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Butengulumasa - Iparamasa – Mbogwe – Masumbwe, Serikali imekuwa ikitoa fedha kwa ajili ya kufanyia matengenezo na kukarabati barabara hii ili iweze kupitika katika kipindi chote cha mwaka. Ujenzi wa kiwango cha lami kwa barabara hii utafanyika kadri bajeti itakavyoruhusu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Kahama hadi Geita, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 12,403 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami. Barabara ya Mafia – Kilindoni – Rasimkumbi; upembuzi yakinifu na usanifu wa kina utafanyika ili barabara hii ambayo pia ipo katika ahadi za Viongozi Wakuu iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Wakati fedha za ujenzi zinatafutwa, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 1.0422 katika bajeti ya 2017/2018 kwa ajili ya kuifanyia matengenezo ya aina mbalimbali barabara ya Kilindoni – Rasimkumbi ili iendelee kupitika wakati wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa barabara ya Makutano – Mugumu hadi Mto wa Mbu na hasa kipande cha Makutano hadi Sanzate kinachoendelea kujengwa, ujenzi wa barabara ya Makutano – Nata – Mugumu, sehemu ya Makutano hadi Sanzate umefikia hatua ifuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tabaka la udongo (G 15) ni kilometa 38 ambayo ni sawa na asilimia 76; tabaka la chini la tuta (sub base) kilometa 8.5; na tabaka la juu la barabara (base course) ni kilometa mbili, lami nyepesi (prime course) ni kilometa 1.2, madaraja ya makalavati makubwa na madogo asilimia 98 yamekamilika. Maendeleo ya jumla ya mradi ni asilimia 43, mradi unatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Septemba, 2017. Aidha, Serikali inasimamia kwa karibu utekelezaji wa mradi huu ili kuhakikisha kuwa mkandarasi anapata ujuzi uliokusudiwa na barabara inajengwa kwa kuzingatia viwango kulingana na mkataba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya barabara kati ya Mugumu hadi Tabora B ambayo ni kilometa 18, mpango wa Serikali ni kuijenga barabara hii mpaka Mugumu. Aidha, ujenzi kwa sehemu nyingine ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutoka Mugumu – Tabora B – Clensi Gate– Loliondo itajengwa kwa kiwango cha changarawe ili kutunza mazingira ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti ambapo sehemu ya Mugumu hadi Tabora B Clensi Gate na sehemu ya Clensi Gate hadi Longido zitatumika kama buffer zone.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipande cha Mugumu - Natta, zabuni zilitangazwa tarehe 07/09/2016 na ufunguzi wa zabuni ilikuwa tarehe 25/10/2016 lakini ulisogezwa hadi tarehe 27/02/2017. Zabuni iliyopokelewa haikukidhi vigezo na hivyo mradi huu utatangazwa tena tarehe 03/05/2017.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi kwa kiwango cha lami kwa barabara Tanga - Pangani - Bagamoyo unatarajiwa kuanza katika mwaka wa fedha 2017/2018. Serikali tayari imetenga shilingi bilioni 4.435 katika bajeti ya mwaka 2017/2018 na inaendelea kukamilisha taratibu za kupata fedha kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika kwa kushirikiana na Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, daraja jipya la Wami kwenye barabara ya Chalinze - Segera liko katika hatua ya kumpata mkandarasi wa kuanza ujenzi. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 daraja hili limetengewa shilingi bilioni 4.351 kwa ajili ya kuanza ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu barabara ya Lindi – Morogoro, kupitia Mpango Mkakati wa Wakala wa Barabara (TANROADS) wa mwaka 2016/2017 hadi 2020/2021, Mkoa wa Lindi umepangwa kuunganishwa na Mkoa wa Morogoro kwa kuanzia na upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara ya Nachingwea – Liwale – Ilonga - Mwaya - Mahenge kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Naibu Waziri wa TAMISEMI ameongelea barabara zote za miji mbalimbali ambazo Mheshimiwa Rais aliahidi na nimshukuru kwamba majibu yake yako sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu barabara ya Kiboroloni – Kiharara - Suduni – Kidia katika mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali ilikamilisha usanifu wa kina. Katika mwaka wa 2017/2018 Serikali imetenga jumla ya shilingi milioni 811 ili kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukarabati wa barabara ya Kibosho – Shine - Mto Sere ambayo ina kilometa 27.5. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imetenga jumla ya shilingi milioni 61 ili kuanza ujenzi wa kiwango cha lami kwa barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeulizwa ni hatua gani zimefikiwa katika kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara ya Kitai – Lituhi na Lituhi -Mbamba Bay. Nimuombe Mheshimiwa Jacqueline Msongozi aondoe tishio lake la kushika shilingi kwa sababu akishika shilingi hapa mimi nitakwenda kushika shilingi Ruvuma. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara ya Kitai - Lituhi umefikia asilimia 50. Mhandisi Mshauri amekwishawasilisha rasimu ya taarifa ya upembuzi yakinifu. Kwa barabara ya Mbamba Bay - Lituhi upembuzi yakinifu na usanifu wa kina umefikia asilimia 60. Mhandisi Mshauri (M/s H.P Gauff Ingenieure) anaendelea kumalizia kazi ya usanifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa barabara inayounganisha Maramba na Makao Makuu ya Wilaya ya Mkinga yenye urefu wa kilometa 49 utatekelezwa na kukamilika kulingana na upatikanaji wa fedha. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 zimetengwa shilingi milioni 87.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Kizi - Sitalike – Lyamba Lya Mfipa, Mji wa Mpanda kupitia Sitalike unaungwa na barabara mbili za Kizi - Lyamba Lya Mfipa - Sitalike ambayo ni kilometa 86.24 na Kibaoni - Sitalike ambayo ni kilometa
71.6 ambazo zote bado kujengwa kwa kiwango cha lami. Mpango uliopo kwa sasa ni kujengwa kwa kiwango cha lami barabara ya Kibaoni - Sitalike ambayo imetengewa kiasi cha shilingi milioni 480 kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami. Aidha, barabara ya Kizi - Liamba Lya Mfipa - Sitalike itaendelea kupatiwa matengenezo ili kuhakikisha kuwa inapitika wakati wote. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, kiasi cha shilingi milioni 1,950 kimetengwa kwa barabara ya Lyamba Lya Mfipa - Mpanda - Uvinza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Kibondo – Kasulu – Mnanila, nashukuru nimeieleza. Nachoomba tu Waheshimiwa wa Kanda ya Magharibi watuamini, siyo kweli kwamba hilo eneo tumelitelekeza, mnafahamu sasa hivi nguvu zote zinaelekezwa huko na mtuamini tunachokisema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Tarime - Mugumu inaendelea na usanifu. Limeulizwa swali ni lini barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? Upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa barabara hii unaendelea na utakamilika mwezi Machi, 2018. Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara hiyo baada ya kukamilisha usanifu wa kina na kujua gharama halisi za mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Handeni – Kiberashi - Kibaya – Singida; katika mwaka wa fedha 2017/2018 barabara hii imetengewa jumla ya shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuanza maandalizi ya ujenzi kwa kiwango cha lami. Ni maandalizi siyo ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa barabara ya Amani - Muheza, Serikali itaendelea kutoa kipaumbele katika utekelezaji wa ahadi za Mheshimiwa Rais.

Hata hivyo, kutokana na uhaba wa fedha, ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami utafanyika hatua kwa hatua kutegemeana na fedha zitakavyopatikana. Katika mwaka wa fedha 2017/2018, barabara hii imetengewa shilingi bilioni tatu kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niingie kwenye barabara ya Bwanga - Kalebezo. Tumepokea shukrani na nimhakikishie Serikali kupitia Wakala wa Barabara Tanzania itaendelea kumsimamia mkandarasi ili ajenge…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. TANROADS watamsimamia mkandarasi ili ajenge barabara ya Bwanga - Kalebezo kulingana na mkataba na hivyo kukamilisha mradi kama ilivyopangwa. Aidha, Wizara itafuatilia ili kuhakikisha mkandarasi anaweka alama za barabarani na kuhakikisha usalama kwa watumiaji wa barabara na wafanyakazi wanaojenga wakati wote wa ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu minara ya simu, niwahakikishie tuna dhamira ya dhati kuhakikisha vijiji vyote Tanzania tunapeleka mawasiliano kupitia Mfuko wetu wa Mawasiliano kwa Wote, lakini vilevile kupitia Kampuni ya Halotel kwa mujibu wa mkataba tulioingia nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.