Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nami nichangie kidogo kwenye hoja hii iliyo mezani.
Kwanza kabisa ningependa kupata majibu ya Waziri, barabara ya Dumila – Rudewa - Kilosa – Mikumi ya kilomita 142 tu nashukuru imetengewa shilingi bilioni 5.207 ili kumaliza kipande cha Rudewa – Kilosa kilomita 18. Je, ni lini sasa Serikali itatenga pesa za ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami kutoka Kilosa – Mikumi kilomita 78 ambayo ni barabara iliyoahidiwa na Rais aliyepita Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete na Mheshimiwa Magufuli wakati wa kipindi chao cha Kampeni. Hii ni barabara muhimu sana ili iweze kusaidia Kata zaidi ya 10 na kukuza uchumi wa watu wa Mikumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliomba barabara ya Ruaha Mbuyuni – Mololo Chabi – Ibanda – Uleling’ombe ipandishwe hadhi lakini siioni katika mpango huu wa bajeti hii ya 2017/ 2018 na hii ni barabara inayounganisha Mikoa ya Iringa – Morogoro na Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia reli ya kutoka Kiwanda cha Sukari Kilombero – Kidatu mpaka Kilosa, ilikuwa inachangia sana kuboresha uchumi wa watu wa Mikumi na kuwaunganisha na reli ya kati. Je, Serikali haioni umuhimu wa kufufua reli hii kama ilivyokuwa zamani ambapo pia kulikuwa na bandari kavu pale Mikumi ambayo ilikuwa inasaidia sana kukuza uchumi wa wananchi wa mikoani na wananchi wa Wilaya ya Kilosa kwa ujumla. Tunaiomba sana Serikali iturudishie bandari kavu ya Mikumi ili iweze kwenda na kasi ya maendeleo ya nchi yetu na kufikia uchumi wa kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa kuhusu mawasiliano, Jimbo la Mikumi limekuwa na matatizo makubwa sana ya mawasiliano, mfano Kata za Vidunda, Uleling’ombe, Chabima, Munisagala, Mhenda, Chonwe, Udungu, Itembe, Tindiga, Malangali, Nyameni na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba sana Serikali ituletee mawasiliano ya simu kwenye vijiji hivi na vingine vingi Vya Jimbo la Mikumi ili wananchi nao wapate fursa ya kupata mawasiliano na kukuza biashara zao na kukuza uchumi wao kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.